DECEMBA 20, WIKI YA 4 YA MAJILIO
Somo: Isa 7:10-14
Zab: 24:1-2, 3-4ab, 5-6
Injili: Lk 1:26-38
Nukuu:
“Jitakie ishara ya Bwana, Mungu wako; itake katika mahali
palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana,” Isa 7:11
“Kwa
hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa
mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli,” Isa 7:14
“Akaingia
nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe,” Lk 1:28
“Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa
maana umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto
mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa
Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki
nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho,” Lk 1:30-33
“Mariamu akamwambia
malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume?” Lk 1:34
TAFAKARI: “Litakuwaje neno hili,
maana sijui mume?”
Wapendwa
wana wa Mungu, Nabii Isaya na Mfalme Ahazi wanakabiliana uso kwa uso juu ya
hatma ya Taifa na wana wa Israeli. Mfalme Ahazi anaomba ushauri ili aweze
kuwashinda maadui zake. Badala yake Nabii Isaya anachokonoa dhamiri, mawazo, na
mtazamo wao juu ya yule wanao paswa kumwamini na kumtumikia. “Naye akasema, Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Daudi; Je! Ni
neno dogo kwenu kuwachosha wanadamu, hata mkataka kumchosha Mungu wangu pia?”
Isa 7:13. Nabii Isaya mtu wa Mungu na mtu
wa imani, anawapa ishara ya kweli. “Kwa
hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa
mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli,” Isa 7:14. Mungu pamoja
nasi! Katika utabiri huu, Mtoto huyu aweza kuwa kihistoria kadiri ya nyakati
zile kuwa ni mtoto wa Mfalme, atarajiwaye kuzaliwa.
Ila katika maudhui ya
Kinabii na hasa nyakati tarajiwa, ilimaanisha kuwa ni Masiha. “Jitakie ishara ya Bwana, Mungu wako; itake katika mahali
palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana,” Isa 7:11. Mtoto huyu ni
zawadi ya wazi kabisa wakati ulipotimia na wa Imani. Ishara hii ndiyo
tunayoiona ikisemwa na Nabii Isaya, 9:5-6, Nabii Mika, 1:18-25, Mwinjili
Mathayo, 1:18-25.
Kutangazwa
kwa Yohana kulitokea katika hekalu kule Yerusalemu, na mpokeaji wa ujumbe huu
alikuwa kuhani, yaani, Zakaria Baba yake. Hapa tunaona nyumba ya unyeyekevu,
kijiji kisichojulikana na nchi isiyojulikana na kudharauliwa. Mungu haitaji
chochote kutoka kwa kiumbe chake alichokiumba ikiwa kiumbe hicho hujifunua
kwake. Ni kwa maana hiyo basi tunaona kazi kubwa za Mungu hufanyika katika ukimya na kwa kujificha
sana. Bikira Maria anakuwa muhimili wa fumbo zima hili kwa matendo haya Makuu
ya Mungu. Malaika “Akaingia
nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe,” Lk
1:28. Maneno haya hayakusemwa kwa Zakaria wala Elizabeti katika kutangazwa
kwake Yohana.
Kama binadamu kwenye
mipaka yake kadiri ya kuumbwa kwake, na maumbile yake, Bikira Maria anamuuliza
Malaika uhalisa wa jambo lile. “Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake,
akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani?” Lk 1:29. Mungu huyakamilisha yote
kadiri ya mapenzi yake licha ya udhaifu wa yule anayependa na kuchagua kufanya
naye kazi hiyo au mpango huo. “Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana
umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume;
na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa
Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki
nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho,” Lk 1:30-33.
Huyu ni Mungu
asiyeshindwa na mweza wa yote. Akiujua mfadhaiko na mahangaiko ndani ya Maria,
“Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake
Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa
kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu,” Lk 1:35. Kuthibitisha Ukuu wa Mungu na
mpango mzima wa wokofu wa mwanadamu, Malaika anaifichua siri kuhusu hali ya
binamu yake Elizabeti na kusema, “Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua
mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye
aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu,” Lk 1:36-37
Huu ni wakati wa
Kimasiha utarajiwao kuwasili. Ishara zilizobeba uwepo huu wa Kimasiha ni pamoja
na unyenyekevu, ukamilifu, na furaha. Bwana na Mungu wetu anakuwa jirani wetu
wa karibu. Bikira Maria anakuwa Yerusalemu mpya, hekalu jipya; Utukufu wa Mungu
una kaa ndani yake. Kwa Imani ya Bikira Maria, agano jipya linaanza. “Mariamu
akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha
malaika akaondoka akaenda zake,” Lk 1:38. Kama Tusomavyo habari hii kutoka katika
kitabu cha Mwazo sura ya 12, na Barua ya Mtume Paulo kwa Warumi sura ile ya 4.
Huu ni wakati wa kuanza upya na Mungu kwa kila mmoja wetu kadiri ya nafasi yake
na wito wake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Matendo
ya Bwana ni makuu, Yafikiriwa sana na wapendezwao nayo,” Zab 111:2
Tusali:-Ee Yesu na
Mkombozi wetu, anza nasi upya na iandike tena historia yetu upya. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario