DECEMBA 19, WIKI
YA 4 YA MAJILIO
Zab: 71:3-4a, 5-6ab, 16-19
Injili: Lk 1: 5-25
Nukuu:
“Palikuwa
na mtu mmoja wa Sora, wa jamaa ya Wadani; jina lake akiitwa Manoa; na mkewe
alikuwa tasa, hakuzaa watoto,” Amu 13:2
“Malaika wa Bwana
akamtokea yule mwanamke, akamwambia, Tazama, wewe sasa u tasa, huzai; lakini
utachukua mimba, nawe utamzaa mtoto mwanamume,” Amu 13:3
“Na wote wawili walikuwa wenye haki mbele za
Mungu, wakiendelea katika amri zote za Bwana na maagizo yake bila lawama,” Lk
1:6
“Nao walikuwa hawana
mtoto, maana Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili ni wazee sana,” Lk 1:7
“Lakini yule malaika akamwambia, Usiogope,
Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti atakuzalia mtoto mwanamume,
na jina lake utamwita Yohana,” Lk 1:13
“Zakaria akamwambia malaika, Nitajuaje neno
hilo? Maana mimi ni mzee, na mke wangu ni mkongwe wa siku nyingi,” Lk 1:18
TAFAKARI:
“Hakuna lisilowezekana kwa Mungu. Mungu anahitaji kilicho bora zaidi kutoka kwako.”
Wapendwa
wana wa Mungu, tangu kufariki kwa Nabii Yoshua, hali ya makabila ya Waisraeli
haikuwa nzuri na yautulivu. Wafilistia waliyanyanyasa sana makabila haya ya
Waisraeli. Katika safari yake ya kumkomboa mwananadamu, Mungu anakisikia kilio
chao, na anamsimamisha mmoja kati ya wana wa Israeli, na kuwarudishia furaha
tena. Hakika kila afanyacho Mungu kina makusudi yake makubwa ikiwa ni
udhihirisho wa Utukufu wake, na furaha na amani kwa waliosetwa. Mungu
humuhusisha mwanadamu Mipango yake kwa sababu mwanadamu huyu ndiye kwenye chapa
yake, yaani, kamuumba kwa sura na mfano wake, Mwan 1:27.
Hivyo
basi, kwa tendo hili lenye matokea makubwa kwanza kabisa linakuwa furaha na
amani kwa mke wa Manoa ambaye alikuwa tasa. “Palikuwa na mtu
mmoja wa Sora, wa jamaa ya Wadani; jina lake akiitwa Manoa; na mkewe alikuwa
tasa, hakuzaa watoto,” Amu 13:2. Malaika wa Bwana akiwa ni mjumbe wa Mungu, wa
mambo muhimu ya Mungu, na yamuhusuyo Mungu, anamtokea Mke wa Manoa na
kumwambia, “Tazama, wewe sasa u tasa, huzai; lakini utachukua mimba, nawe
utamzaa mtoto mwanamume,” Amu 13:3. Hakika, lisilowezekana kwa mwanadamu kwa
Mungu linawezekana. Mungu anataka kilicho bora kutoka kwetu. Bila shaka familia
hii, yaani, Manoa na Mkewe walikuwa na hofu kubwa sana, na nini hatma ya maisha
yao. Mungu kamwe
hamtupi mja wake hasa pale anapojiachia kwake bila kujibakiza.
Kwa vile kitakachozaliwa lazima kijibu mahangaiko ya
watu wa Mungu, Malaika anatoa masharti yake kadiri ya matakwa ya Mungu. Huku
ndiko kule kuwa Mnadhiri wa Mungu kama tusomavyo kukoka kitabu cha hesabu
6:2-8. Na haya ndiyo anayoyasema Malaika kwa Mke wa Manoa, kwamba, “Basi sasa,
jihadhari, nakuomba, usinywe divai wala kileo, wala usile kitu kilicho najisi; kwani tazama, utachukua mimba, nawe
utamzaa mtoto mwanamume; na wembe usipite juu ya kichwa chake; maana mtoto huyo
atakuwa mnadhiri wa Mungu tangu tumboni; naye ataanza kuwaokoa Israeli na
mikono ya Wafilisti,” Amu 13:4-5. Mtoto huyu anatengwa
rasmi kwa kazi ya Mungu na yanayomuhusu Mungu. “Basi yule mwanamke akamzaa
mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana
akambarikia,” Amu 13:24. Samsoni anachukua jukumu kubwa kutoka kwa Mungu, na
anashirikishwa kazi Takatifu ya Mungu, yaani, mpango wa wokovu wa mwanadamu.
Jambo lingine kubwa lenye mfanano kama
huu linatokea pia kwenye Injili yetu ya leo. Mungu anavunja ukimya kwa kuingia
katika historia ya mwanadamu kwa kuleta furaha na Amani kwa wale waliosetwa, na
kuudhihirisha Utukufu wake. Zakaria na Mkewe Elizabeti hawakufanikiwa kupata
mtoto kwa muda mrefu sana. Kwa hali ya kibinadamu matumaini yao yalianza
kutoweka. Maandiko Matakatifu yanatuambia hivi, “Nao
walikuwa hawana mtoto, maana Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili ni wazee
sana,” Lk 1:7. Pamoja na hali hii isiyowezekana kutokana na mipaka yetu
kibinadamu, bado Mungu anahitaji kilicho bora kutoka kwetu. Kilichobora kutoka
kwa Zakari na Elizabeti ilikuwa maisha yao ya uaminifu na Imani thabiti. “Na
wote wawili walikuwa wenye haki mbele za Mungu, wakiendelea katika amri zote za
Bwana na maagizo yake bila lawama,” Lk 1:6. Hakika, Mungu kamwe hamtupi mja
wake anapojiachia kwake bila kujibakiza!
Hivyo Zakaria akiwa
katika shughuli zake za kila siku hekaluni, “Akatokewa na malaika wa Bwana,
amesimama upande wa kuume wa madhabahu ya kufukizia,” Lk 1:11. Tukio hili
linamshtusha sana Zakari. Halikuwa jambo la kawada kwake. “Lakini yule malaika
akamwambia, Usiogope, Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti
atakuzalia mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yohana,” Lk 1:13. Hii ni
habari njema kwa Zakaria na Mkewe Elizabati. Mungu ameamua kuwatoa aibu na
kuwapa hadhi yao kama wazazi.
Hadhi hii ambayo kwa
msingi na mtazamo katika jamii ni heshima kubwa kwa wazazi wote wawili, na kwa
namna ya pekee kwa upande wa mama. Ujumbe huu ni habari njema na siyo adhabu.
Ni habari njema kama tusomavyo kutoka kitabu cha Nabii Sefania, “Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; Furahi
na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu. Bwana ameziondoa hukumu zako, Amemtupa
nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa
uovu tena. Katika siku ile
Yerusalemu utaambiwa, Usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee. Bwana, Mungu wako, yu katikati yako
shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha kuu, Atakutuliza katika upendo
wake, Atakufurahia kwa kuimba,” Sef 3:14-17
Malaika anaendelea
kuufunua ujumbe wa Mungu kwa kile kitakachozaliwa, ikiwa ni pamoja na kazi
atakayoifanya kwa sifa na utukufu wa Mungu. Atakayezaliwa atatengwa kwa kazi ya
Mungu, “Kwa sababu atakuwa mkuu mbele za Bwana; hatakunywa divai wala kileo;
naye atajazwa Roho Mtakatifu hata tangu tumboni mwa mamaye,” Lk 1:15. Hakika
ataongozwa na Roho Mtakatifu kabla hata ya kuzaliwa kwake. Jambo hili
litajidhihirisha kwenye maamkio kati ya Mariamu na Elizabeti baadaye.
Huyu atakayezaliwa,
yaani, Yohana, na baadaye kama Yohona Mbatizaji, atakuwa na kazi hii ifuatayo,
“Naye atatangulia mbele zake katika roho ya Eliya, na nguvu zake, ili kuigeuza
mioyo ya baba iwaelekee watoto, na kuwatilia waasi akili za wenye haki, na
kumwekea Bwana tayari watu waliotengenezwa,” Lk 1:16-17. Kwa ufupi kazi yake
itakuwa kuwaandaa watu na kuiandaa njia ya mwokozi, yaani, Yesu Kristo. “Sikiliza, ni sauti ya mtu aliaye, Itengenezeni nyikani
njia ya Bwana; Nyosheni jangwani njia kuu kwa Mungu wetu,” Isa 40:3. Huyu ndiye
Yohane Mbatizaji na kazi ile atakayoifanya.
Lakini
pamoja na Malaika kumwambia Zakaria asiogope juu ya ujumbe huu, bado anakuwa na
mashaka na kumwiya vigumu kuamini. Zakaria anautazama zaidi uchakavu wake wa
nje na kusahau utu wake wa ndani. “Zakaria akamwambia
malaika, Nitajuaje neno hilo? Maana mimi ni mzee, na mke wangu ni mkongwe wa
siku nyingi,” Lk 1:18. Katika mahangiko haya, mazingira na hali yake, Mtume Paulo anatuambia, “Kwa hiyo hatulegei;
bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa
upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16. Hivyo hakuna
lisilowezekana kwa Mungu. Mungu anahitaji kilicho bora zaidi kutoka kwako.
Zakaria
anashindwa kumpa Mungu kilicho bora zaidi kutoka kwake, yaani, ‘Imani yake ya
kweli’. Hivyo jambo hili linakuwa chukizo kwa Mungu, na hivyo “Malaika
akamjibu akamwambia, Mimi ni Gabrieli, nisimamaye mbele za Mungu; nami
nimetumwa niseme nawe, na kukupasha habari hizi njema. Na tazama!
Utakuwa bubu, usiweze kusema, mpaka siku ile yatakapotukia hayo, kwa sababu
hukuyasadiki maneno yangu; nayo yatatimizwa kwa wakati wake,” Lk 1:19-20.
Hata pamoja na tukio
hilo la kutokuamini kwake Zakaria, Mungu hakusitisha mpango wake na nia yake
njema katika safari hii ya ukombozi. “Hata baada ya siku zile mkewe Elisabeti
alichukua mimba akatawa miezi mitano, akisema, Hivi ndivyo
alivyonitendea Bwana katika siku zile alizoniangalia ili kuniondolea aibu yangu
mbele ya watu,” Lk 1:24-25. Huyu ndiye Mungu asiyeshindwa. Huyu ndiye Mungu
anayetutoa katika vifungo vya mateso na aibu zetu. Ndugu yangu tuliyesafiri
wote katika tafakari hii, tunaalikwa wewe na mimi kutokukata tamaa hata pale
tunapoona giza tupu mbele ya maisha yetu. Mungu huyaona mahangaiko yetu yote.
Bado anahitaji kilicho bora zaidi kutoka kwetu, yaani, ‘Imani thabiti.’
Tumsifu Yesu Kristo!
“Jaribu
halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni
mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile
jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie nguvu na Imani thabiti ya kustahimili majaribu, na kuyashinda.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario