JUMAPILI YA 2 YA MAJILIO YA MWAKA-A
Somo
I: Isa 11:1-10
Zab:
72:1-2, 7-8, 12-13, 17
Somo
II: Rum 15:4-9
Injili:
Mt 3:1-12
Nukuu:
“Basi
litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi
yake litazaa matunda,” Isa 11:1
“Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa
ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali
pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu,” Isa 11:10
“Tubuni; kwa maana
ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 3:2.
“Kwa sababu huyo ndiye aliyenenwa na nabii
Isaya, akisema, Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana,
Yanyosheni mapito yake,” Mt 3:3.
“Na Mungu mwenye saburi na faraja awajalie
kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; ili kwa moyo mmoja na
kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo,” Rum
15:5-6
“Kwa maana nasema, ya kwamba Kristo amefanyika
mhudumu wa agano la kutahiriwa kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe
ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya
rehema zake; kama ilivyoandikwa, Kwa hiyo nitakushukuru kati ya Mataifa, Nami
nitaliimbia jina lako,” Rum 15:8-9
TAFAKARI:
“Kristo amefanyika mhudumu wa agano la kutahiriwa kwa ajili ya kweli ya Mungu,
kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya pili ya Majilio ya Mwaka “A” wa
Kanisa. Masomo yetu yote matatu ya leo yanaufunua mpango mzima wa Mungu kumkomboa
mwanadamu kutoka hali yake ya utumwa, mwili na roho. Ikiwa wewe na mimi ni
tokeo la upendo wake, na tendo hilo kuufunua Utukufu wake, na hivyo kuibeba
chapa yake ndani yetu, Mungu asingependa tupotee katika hali ya dhambi.
Na
kulikamilisha hili, yaani, kumkomboa mwanadamu kutoka hali yake ya mateso,
mahangaiko na dhambi, Mungu huyu aliye Kweli, Haki, Amani, na Upendo kwa
makusudi makubwa anapenda kuanzisha uhusiano na yule aliyemuumba kwa sura na
mfano wake, Mwa 1:27. Tendo hili la kuujenga uhusiano wa karibu nasi
linamshusha Mungu chini kabisa katika hali ya mwanadamu. Huu ni upendo mkubwa
sana kwetu. Kipindi hiki cha majilio ni kipindi cha kutafakari upendo huu wa
ajabu Mungu anaokwenda kutufanyia. Ikiwa zawadi hii ni kubwa sana kwetu hatuna
budi kujiandaa vizuri mwili na roho ili atakapokuja atukute tupo safi na wenye
afya njema hasa roho zetu.
Kufanikisha
mpango huu, Mungu huyu aliye Alfa na 0mega atachukua hali yetu ya kibinadamu,
na hivyo atazaliwa ikiwa ni moja ya kushiriki hali yetu ya kibinadamu. Jambo
hili linatabiriwa na Nabii Isaya. “Basi
litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi
yake litazaa matunda,” Isa 11:1. Je huyu
atakayezaliwa ataongozwa na mamlaka gani? Hakika kwa vile anakuja kuusimika
ufalme wa kweli, haki, amani, na upendo, “roho
ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza,
roho ya maarifa na ya kumcha Bwana,” Isa 11:2. Hivi ndivyo vitendea kazi vyake.
Ujio wake kwetu ni hukumu pia ambayo itasimama katika haki. Hivyo, “kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya
wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake,
na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya,” Isa 11:4
Ujio wa mfalme huyu ni
ujio wa neema na baraka. Anakuja na kusimika ‘mfumo wema’ na kuufifisha ‘mfumo
uovu.’ Anakuja kuondoa sintofahumu zetu kati yetu wanadamu na viumbe vingine
alivyoviumba. Huyu hakika ni Mfalme wa Amani. Hakutakuwa tena na sintofahumu
kati ya wanyama aliowaumba. “Mbwa-mwitu
atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na
mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza,” Isa 11:6.
Mwanadamu ataishi kwa amani na hofu haitakuwepo tena. “Na
mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia
mkono wake katika pango la fira,” Isa 11:8.
Uwepo
wa Mfalme huyu wa kweli, haki, amani na
upendo utajidhihirisha kwa utukufu wake.
Mataifa yote watamfuata alipo kwa sababu kuna Utukufu. “Na itakuwa katika
siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye
ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu,”
Isa 11:10. Haya ndiyo atakayoyafanya na kuujenga tena uhusiano wetu
ulioharibiwa na dhambi zetu.
Wapendwa
wana wa Mungu, pamoja na hayo mazuri yote yaliyotabiriwa na Nabii Isaya kuhusu
Mfalme huyu tunayemsubiri kwa hamasa kubwa, yatawezekana tu kama tutakuwa
tayari kutoa ushirikiana naye. Mungu atukokoti kama Jemedari katili na mwenye
silaha za kutisha. Utawala wake ni utawala wa Upendo. Mungu hapendi kuondoa
uhuru na utashi wetu wa kumfuata. Ametuachia haya yote akijua kabisa kwamba kwa
kuyatumia vizuri ni njia rahisi ya kumfikia, hata pale tutakapoyatumia vibaya
itakuwa njia rahisi pia ya kumrudia tukifanya toba ya kweli na majuto.
Kama ilivyo kwa utawala
mpya kuonyesha tofauti na utawala au tawala zilizotangua, tofauti hiyo
ujionyesha katika kauli mbiu yake. Mfano: Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Kabarage Nyerere, na sasa Mtumishi wa Mungu, alikuwa na kauli mbiu hizi
kuonyesha utofauti wa utawala wake na ule wa kikoloni (Uhuru na Umoja, Uhuru na
Maendeleo, na Uhuru na Ujamaa). Na alicho kilenga hapa Mwalimu Nyerere ni Uhuru
wenye kuleta Umoja, Maendeleo, na Undugu, bila kujali tofauti zetu kiitikadi,
kiimani, kifamili, kikoo, kikabila, na hata kijiografia. Dhima hii ndiyo
inayotushikamanisha hadi leo kama Taifa licha ya kwamba kwa sasa twaziona
nyufa.
Aliye mridhi, yaani,
Rais Ali Hassani Mwinyi, kadiri ya
mazingira yake, na mabadiliko ya kiulimwengu katika maana ya kimfumo, yaani,
ujio wa soko huria, akawa na kauli mbiu yake, “Ruksa.” Milango na madirisha
yalifunguliwa na kila kitu hasa, kiuchumi vilikubaliwa. Mtoto mdogo mwenye pesa
nyingi nyakati zile alipewa jina la MZEE, yaani, anazo! Aliye mfuata, ‘Mzee wa
Ruksa,’ yaani, Rais Benjamin William Mkapa, naye hakuwa nyuma kuhusu kauli
mbiu. Dira yake iliongozwa na haya: (Ukweli na Uwazi, Nguvu za Masikini ni
mtaji wake mwenyewe, na ubinafsishaji wa mashirika ya Umma, ingawa vuguvugu
hili lilianza kwa mtangulizi wake).
Baada ya kauli mbiu hii
kupita, tulipata pia kauli mbiu nyingine kutoka kwa mrithi wa Rais Mkapa,
yaani, Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Dhamiri yake iliongozwa na upyaisho, yaani,
kuleta nguu mpya. Na bila shaka wote tunaikumbuka kauli mbiu hii; “Nguvu mpya,
kasi mpya, na hari mpya.” Na leo chini ya Rais wetu John Pombe Magufuli
tunaongozwa na kauli mbiu hii; “Hapa kazi tu!”
Ndugu yangu, maisha
yale yote yenye mwelekeo chanya hayakosi kuwa na msukumo wake, yaani, kauli
mbiu yake. Na leo kwa namna ya pekee, ujumbe wa Yesu umebebwa na kauli mbiu
hii: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 3:2. Kutubu ni
dhamiri ya ndani yenye kukutaka kuyaanza yote upya katika maana ya kukataa
kutoka ndani kuongozwa na yale ya kale, na yasiyo na upeo wa huko utakako
kufika, na kwa maana hii, maisha yale ya umilele.
Alisemalo Yesu ‘Ufalme
wa Mungu umekaribia,’ haikuwa mbwembwe za kisiasa ambazo mara nyingi kile
kisemwacho majukwani sicho kimaanishwacho. Yesu anamaanisha kweli kile
akisemacho, yaani, ukaribu huo wa ufalme wa Mungu ni uwepo wake mwenyewe kama
pendo la Mungu lililo wazi, na Ufunuo wa Mungu usio na shaka. Na hii ndiyo
maana ya maneno haya ya Yesu yaliyolandana na kile alichokisema katika kauli
mbiu yake, kwamba, “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana
amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia
wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru
waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19.
Ndugu yangu tunaye
safiri sote katika tafakari hii, ujio wa Yesu sio wa kugushigushi au
udanganyifu kama tuonavyo leo kwa wale wote wanaojitwalia mamlaka bila
utaratibu. Ujio wa Kristo na Mkombozi wetu, ni mpango wa Mungu mwenyewe ulio
jikita katika dhima nzima ya kumkomboa mwanadamu. “Kwa sababu huyo (yaani,
Kristo) ndiye aliyenenwa na nabii Isaya, akisema, Sauti ya mtu aliaye nyikani,
Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake,” Mt 3:3. Kuyanyoosha
mapita,’ ndicho kilicho beba kauli mbiu ya Yesu. Na hapo tutakapo yanyoosha mapito
yetu, yaani, vilema vyetu, ndipo penye, neema na huruma ya Mungu. Nasi
tunawajibu wa kufanya ili yale yote aliyoyaazimia Mungu ndani yetu yatimie.
“Aliye kuumba wewe pasipo wewe hawezi kukukomboa wewe, pasipo wewe,” Mtakatifu
Agustino wa Hippo.
Wajibu huu muhimu
kuelekea neema na huruma ile ya Mungu ni kuukiri ukweli na kusimama katika
kweli hiyo. Yohana Mbatizaji anawaongoza watu wake katika njia hiyo, kama
maandalizi kwa ujio huo wa Mwokozi wetu. “Ndipo walipomwendea Yerusalemu, na
Uyahudi wote, na nchi zote za kandokando ya Yordani; naye akawabatiza katika
mto wa Yordani, huku wakiziungama dhambi zao,” Mt 3:5-6. Leo na katika
mazingira yetu, Mama Kanisa anachukua nafasi hii ya Yohana Mbatizaji katika
kuwaongoza wana wake katika kweli na haki, na kusimama katika kweli hili, bila
kutetereka na kuishuhudia Imani ya kweli.
Furaha ya Mama Kanisa
siyo kuona mtiririko wa watu waikimbiliayo njia hii kama ng’ombe waswagwao
kuelekea zizini, bali furaha ya Mama Kanisa ni kuona kila aifuataye njia ya
kweli anatambua sababu ya kufanya hivyo, na kuwa tayari kuishuhudia sababu hiyo
mbele za watu. Hii ndiyo Imani ya kweli. Ni katika mazingira haya Yohana
Mbatizaji anatoa angalizo kwa wale waliofuata mkumbo pasipo kujua maana ya
kufanya hivyo. “Hata alipoona wengi miongoni mwa Mafarisayo na Masadukayo
wakiujia ubatizo wake, aliwaambia, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya
ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?” Mt 3:7. Kumbe, lengo siyo kuukimbilia
utukufu ule ulio mbele yako, bila kufuata njia ile ikupelekeayo kwenye tamanio
hilo la utukufu. Kristo ndiyo mfano wenyewe, kwa sababu katika Kristo Yesu
tunajifunza kwamba hakuna Utukufu pasipo Msalaba, na hakuna Pasaka bila Ijumaa
Kuu. Na ukitaka kujua Mungu ni nani, Msalaba unasema yote kuhusu Mungu.
Utafakari Msalaba!
Hivyo angalizo la
Yohana Mbatizaji, na leo Mama Kanisa, ni kufanya toba, ili tuyapate matunda
yake, yaani, neema, baraka, na huruma ya Mungu. “Basi zaeni matunda yapasayo
toba; wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana
nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia Ibrahimu watoto,”
Mt 3:8-9. Ndugu yangu, ingawa Kristo Yesu kesha inyoosha njia kuelekea maisha
yale ya uzima wa milele, safari hiyo siyo mteremko mchirizo, bali kila mmoja
lazima afanye sehemu yake, na katika ukamilifu wake, ingawa udhaifu upo.
Bila kufanya hivyo,
sahau ndoto na tamaa ya uzuri huo wa umilele. Ukweli ni kwamba, mwenye kuijua
siri hii aelewe kwamba, “shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi
kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni,” Mt 3:10. Kuijua
kweli, na kutokuifanya au kuiishi kweli hiyo, kwa maanisha tarajio la epuko
lile ambalo ndilo likutakalo kuifanya kweli hiyo ili uwe huru. Na usipo utaka
ukweli huu ni kukubali epuko hilo ambalo katika lugha hii ya picha ni kutupwa
motoni, mateso yasiyo na ukomo.
Licha ya kwamba Yohana
Mbatizaji anaijua siri hiyo na kuwaongoza watu katika kweli hiyo, kwamwe
hajiinui kwa lolote lile. Yohana anafahamu nafasi yake, na anatimiza wajibu
wake katika ukamilifu wake. Naye anasema, “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa
ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala
sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na
kwa moto,” Mt 3:11. Ndugu yangu, Kanisa kama nafasi hii ya Yohana Mbatizaji, ni
jumuiya ya Wakristo Wabatizwa, na mabao ndani yake wapo wadhambi na Watakatifu.
Pamoja na ukweli huu, Kanisa ambalo ni mwili wa Kristo nasi viungo vya mwili
huo, haliachi kuwa Sakramenti ya wokovu
wa mwanadamu.
Nguvu na uwepo huo wa
Kristo katika udhaifu huu wa wana wa Mungu, yaani, wanadamu, Kristo uliongoza
Kanisa katika kweli na haki, naye ubaki kuwa mizania ya kweli, na hakimu mwenye
haki, “Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake;
na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto
usiozimika,” Mt 3:12. Huyu ndiye Masiha tunayemsubiri kwa hamu, na huyu ndiye
Mkombozi wetu ambaye kila uvutapo pumzi yake Mungu, anakupa fursa ya kumgeukia
na kuyaacha yale yote ya kale, na kuanza yote upya pamoja naye. Na hili ndilo
tumaini hai, “kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili
kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na
tumaini,” Rum 15:4
Wapendwa katika Kristo,
kipindi hiki cha majilio kinatutafakarisha pia kuhusu sala ya utakatifu. Sala
ya utakatifu haina ubinafsi wala kujitanguliza. Ni sala inayotambua wengine
walio na shida kama yako, na hata zaidi. “Na Mungu mwenye saburi na faraja
awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu; ili kwa moyo
mmoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu
Kristo,” Rum 15:5-6.
Hata pale tunapojisikia
kuwa tumeachwa na kusahauliwa, hatuna sababu ya kulalamika zaidi ya kufurahia
utukufu ule ambao tutaupata tukilishida jaribu hilo kwani Mungu anajua lazima
tutashinda tunapoutumia uhuru wetu vyema bila kumuasi Mungu. “Jaribu
halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni
mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile
jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13.
Na tendo hilo la
kuutumia vizuri uhuru aliotupa Mungu bila kumsaliti Mungu, linatuweka karibu
zaidi na Mungu tunapojitoa bila kujibakiza kwa wengine na hasa wahitaji wakati
huo huo bila kujisahau katika sala na ukaribu na Mungu. “Kwa hiyo mkaribishane
ninyi kwa ninyi, kama naye Kristo alivyotukaribisha, ili Mungu atukuzwe,” Rum
15:7.
Mtindo huu wa maisha ndio aliouishi Yesu
Kristo angali hapa duniani ingawa Yeye alikuwa Mungu na Mwanadamu. Alijitoa bila
kujibakiza katika mila na desturi ambayo waliokuwa na uwezo walijiinua na
kuwasahau wale wote wasio kuwa na sauti katika jamii. Hivyo Yesu alikuwa sauti
ya wasio na sauti, yaani, wakoma, wadhambi, viwete, vipofu, wazinzi, wanawake,
watoto, na watoza ushuru. Hawa ndio waliokuwa jamaa na rafiki wa karibu wa
Yesu. Kuwa kwake karibu hakukumaanisha alifurahia hali yao na hivyo ni utukufu
kuwa hivyo, bali alikuwa karibu yao ili awatoe katika mateso na masikitiko yao.
Na hili ndilo dhihirisho lililo wazi la Mkombozi wetu. Na kwa maana hiyo,
“Kristo amefanyika mhudumu wa agano la kutahiriwa kwa ajili ya kweli ya Mungu,
kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze
Mungu kwa ajili ya rehema zake; kama ilivyoandikwa, Kwa hiyo nitakushukuru kati
ya Mataifa, Nami nitaliimbia jina lako,” Rum 15:8-9
Hakina Kristo anatupenda upeo, Yoh 13:1, na
kwa tendo hili la kumwilishwa, Yesu anaukubali umasikini ili wewe na mimi tuwe
matajiri mwili na roho. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi
alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi
mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Ndugu yangu, utajiri wa kweli
ni kumpata Kristo Yesu na kuishi ndani na katika Yeye tu. Na kwake tu, yaani,
Kristo Yesu, kuna furaha ya kweli kwa sababu kwake tu tunapata sababu ya
furaha, mateso, na mahangaiko yetu.
Daudi Jamali, mzaliwa
wa Kigoma, katika kuyatafuta maisha mazuri na yenye hadhi, rafiki yake
alimwamba nchini Kongo kuna dhahabu nyingi sana, na kuipata ni rahisi sana
kwani watu wa huko Kongo uchimba umbali wa mita mbili tu.
Hivyo Daudi alianza
safari yake ingawa hakujua ni sehemu gani huko Kongo kuna hiyo dhahabu.
“Nitakwenda tu, na nitawauliza watu wa huko nami nitafika,” Daudi alijipa moyo.
Safari kutoka Kigoma
hadi Kongo kwa miguu ilimchukua wiki mbili hivi. Akiwa katikati ya msitu mnene,
hakujua mwelekeo wa kufuata. Na hapa aliona ulazima wa kuuliza. Mbele yake
kulikuwa na Mzee mmoja, na baada ya kumuuliza Mzee huyo alimjibu, “Ukitaka
kufika huko kwenye hiyo dhahabu yakupasa kurudi hadi pale ulipoanza safari
yako. Hapa ulipo hutoweza kufika huko,” yule Mzee aliondoka taratibu.
Daudi alijishauri sana,
akifikiria safari yake tena ya wiki mbili kurudi hadi Kigoma. Mwisho kwa unyonge
alifanya maamuzi magumu na kurudi.
Ndugu yangu, hata wewe
waweza kuwa kama Daudi Jamali. Ikiwa ushapotea na hicho ukiangaikiacho
hujakipata, ni vyema kurudi pale ulipoanza safari yako, kwani kwa kufanya hivyo
kuna uhakika wa kukipata hicho ulichokuwa unakitafuta kwa sababu hapa utapata
ramani ya kufika kwenye nia yako. Na hii ndiyo toba ya kweli. Usitazame muda
uliokwishapoteza, bali tumaini lile la kweli.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Tubuni; kwa maana ufalme wa
mbinguni umekaribia,” Mt 3:2.
Tusali:-Ee
Yesu na Mwokozi wetu, tunakutumainia. Usituache. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario