KIPINDI CHA KUZALIWA BWANA
NOELI:
MISA YA MCHANA
Somo
I: Isa 52:7-10
Zab:
98: 1, 2-3, 3-4, 5-6
Somo
II: Ebr 1:1-6
Injili:
Yoh 1:1-18
Nukuu:
“Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, Enyi mahali pa
Yerusalemu palipokuwa ukiwa; Kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, Ameukomboa
Yerusalemu,” Isa 52:9
“Bwana
ameweka wazi mkono wake mtakatifu Machoni pa mataifa yote; Na ncha zote za
dunia Zitauona wokovu wa Mungu wetu,” Isa 52.10
“Mungu,
ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia
nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa
mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu,” Ebr 1:1-2
“Yeye kwa kuwa ni
mng'ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya
uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu
huko juu; amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina
alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao,” Ebr 1:3-4
“Hata tena, amletapo
mzaliwa wa kwanza ulimwenguni, asema, Na wamsujudu malaika wote wa Mungu,” Ebr
1:6
“Hapo mwanzo kulikuwako
Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo
mwanzo alikuwako kwa Mungu.Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye
hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:1-3
“Bali wote waliompokea
aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa,
si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa
Mungu,” Yoh 1:12-13
“Naye Neno alifanyika
mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee
atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli,” Yoh 1:14
TAFAKARI:
“Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
“Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, Enyi
mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa; Kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake,
Ameukomboa Yerusalemu,” Isa 52:9. Leo katika adhimisho hili la Misa
Takatifu, siku hii ya kuzaliwa Mwokozi na Mkombozi wetu Yesu Kristo, Misa hii
ya Mchana, Mama Kanisa kwa furaha kubwa,
anatuzamisha ndani kabisa tutafakakari juu ya Umungu wa Bwana wetu Yesu Kristo,
ikiwa ni asili yake ya pili. Jana usiku kwenye Misa ile ya Kesha la Noeli, Mama
Kanisa alifanya tafakari ya kina kuhusu ubinadamu wa Yesu Kristo. Hivyo asili
hizi mbili ndizo alizokuwa nazo Yesu hapa duniani kwa ajili ya kile
alichokijia, yaani, kutukomboa kutoka katika utumwa wa dhambi, na kuturudishia
hadhi yetu tena ya kuwa wana na warithi wa ufalme wa mbinguni, na kuviratibisha
vyote katika kweli na haki, kuelekea ukamilifu na upendo wa Mungu Baba.
Hivyo kadiri ya Injili
ya leo, Mwinjili Yohane anatutafakarisha kwa undani kabisa asili hii ya Umungu
wa Mwokozi na Mkombozi wetu Yesu Kristo. Ni kwenye sehemu hii ya Injili pia
tunaona nani ni Yesu, na nafasi yake
ilikuwa wapi kabla ya kuumbwa kwa ulimwengu na vyote vinavyoonekana na
visivyoonekana. Siku hii ya leo Tukufu ya Mungu, kuzaliwa kwake Yesu Kristo,
imeufunua ukweli ambao haukuwahi kujulikana tangu kuumbwa kwa ulimwengu. Ukweli
huo ni huu kwamba, “Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote; Mungu Mwana
pekee aliye katika kifua cha Baba, huyu ndiye aliyemfunua,” Yoh 1:18. Huu ndio
msingi na ufupisho wa hayo yote aliyoyasema Mwinjili Yohane.
Ufupisho huu unagusa
subira yote katika historia nzima ya wokovu wetu, kama asemavyo Nabii Isaya, “Bwana ameweka wazi mkono wake mtakatifu Machoni pa
mataifa yote; Na ncha zote za dunia Zitauona wokovu wa Mungu wetu,” Isa 52.10.
Kwa hiyo, “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye
Neno alikuwa Mungu. Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi
tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa
neema na kweli,” Yoh 1:1, 14. Ni kwa sababu hiyo katika Mwili ni Mungu kama
Baba.
Kwa uwezo wake wa
Kimungu, hakuna chochote kilichokuwa pasipo Yeye, yaani, neno huyu aliyefanyika mwili. “Hapo mwanzo
kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo
mwanzo alikuwako kwa Mungu.Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye
hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:1-3. Ni kwa maana hii na ukweli
huu kwamba, ye yote amwonaye Kristo, amemwona Baba. Yesu kauthibitisha ukweli
huu, kuiondoa shaka aliyokuwa nayo Filipo pale alipomtaka amwonyeshe Baba.
Naye, “Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja
nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba;
basi wewe wasemaje, Utuonyeshe Baba?” Yoh
14:9. Lakini “kuona” huku kunawezeshwa tu kwa yule anayelisikia neno, yule
ambaye kwa imani anaona zaidi ya “mwili,” yaani, utukufu wa Baba alioupokea.
Kwa hiyo kuja kwake Mwokozi wetu ulimwenguni huku ni “utengano”: kuwatenga watu
katika mwanga na giza, kama mwanga ambao ni wa ulimwengu. “Huyo
hakuwa ile nuru, bali alikuja ili aishuhudie ile nuru. Kulikuwako
Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu, akija katika ulimwengu,” Yoh 1:8-9.
Mwilinjili Yohana hapa anamnukuu Yohana Mbatizaji kama mtengeneza njia.
Hivyo wapendwa katika
Kristo, wote watakaoupokea mwanga huo wanaupokea kwa Imani ikiwa ndiyo zawadi
kubwa aliyetuletea Mwokozi na Mkombozi wetu. “Bali wote waliompokea aliwapa
uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa,
si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa
Mungu,” Yoh 1:12-13. Mwokozi na Mkombozi wetu leo hii anahitaji nafasi ndani ya
Moyo wako. Bila shaka wengi wetu hii siyo Noeli ya kwanza kusherehekea. Basi
nikuombe ufanye mabadiliko mwaka huu kama tendo la shukrani kwa Mungu. Yakupasa
kufanya mkataba na Mungu kuhusu maisha yako, na iwe tendo lako la kudumu muda
wote uwapo hapa duniani. Fanya hivyo na Mungu atakutumia vizuri kadiri ya
mpango na hitaji lake.
Huna wakati mwingine
tena katika maisha yako wa kufanya jambo hili ninalokuwambia. Kama Mungu
ilifika mahali akasema basi na inatosha, kwa nini wewe usiseme pia basi
inatosha kwa kuanza upya na Mungu? Ni Mungu huyu, “ambaye alisema zamani na
baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa
siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena
kwa yeye aliufanya ulimwengu,” Ebr 1:1-2. Leo tunapewa nafasi ya kuongea naye
moja kwa moja na bila chenga.
Wapendwa katika Kristo,
katika Ukuu na Umungu wake Mwokozi na Mkombozi wetu, “Yeye… ni mng'ao wa
utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake,
akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu;
amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo
tukufu kuliko lao,” Ebr 1:3-4. Hivyo mwisho wa maisha yetu hapa duniani utakuwa
na maana na uhakika wa umilele ndani na katika Kristo Yesu. Jamani Mungu yupo
na huyu ndiye tunayemshangilia na kumsheherekea leo. Hatuna uzima pasipo Yeye.
Mwana falsafa, mwana
mashairi, mwanamziki na mtaalamu wa lugha,
aliyejulikana sana, Friedrich Wilhelm Nietzche (1844-1900), hakuamini
kuwa Mungu yupo. Nietzche alikuwa mzaliwa wa Urusi ya Zamani, ila maisha yake
karibia yote aliishi Ujerumani. Falsafa yake ilijulikana kama “Nihilism and
death of God,” kwa maana ya kwamba, “Vyote ni ubatili na kifo cha Mungu.”
Katika moja ya maandishi
yake yaliyobeba falsafa hii alithubutu kusema “Mungu amekufa kwa hiyo hakuna
Mungu.” Watu wengi wasioamini uwepo wa Mungu walishabikia sana falsafa yake na
hasa eneo la Ulaya. Ila jambo la ajabu, tarehe 25 mwezi wa Agosti, 1900, Mungu
alitangaza kuwa “Mwafalsa mashuhuri Friedrich Wilhelm Nietzche amefariki,” kwa
ugonjwa wa Neumonia katika umri wa miaka 55.
Ndugu yangu uliyesafiri
nami katika tafakari hii, kati ya Nietzche na Mungu, ni nani aliye mkweli?
Tusisahau jambo hili: “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu,
tena huleta juu. Bwana
hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bwana
ameweka wazi mkono wake mtakatifu Machoni pa mataifa yote; Na ncha zote za
dunia Zitauona wokovu wa Mungu wetu,” Isa 52.10
Tusali:-Ee Yesu na
Mkombozi wetu, tuondolee upofu wetu wa Imana na kuacha kuona Umungu na
Ubinadamu wako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario