lunes, 26 de diciembre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA MT. YOHANE MTUME , NA MWINJILI


Sikukuu ya Mt. YOHANA MTUME na mwinjili

DECEMBA 27

Somo: 1Yoh 1:1-4

Zab: 97:1-2, 5-6, 11-12

Injili: Yoh 20:1, 2-8

Nukuu:

“Lile lililokuwako tangu mwanzo, tulilolisikia, tuliloliona kwa macho yetu, tulilolitazama, na mikono yetu ikalipapasa, kwa habari ya Neno la uzima,” 1Yoh 1:1

 “hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana nasi: na ushirika wetu ni pamoja na Baba, na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo,” 1Yoh 1:3

 “Basi akaenda mbio, akafika kwa Simoni Petro na kwa yule mwanafunzi mwingine ambaye Yesu alimpenda, akawaambia, Wamemwondoa Bwana kaburini, wala hatujui walikomweka,” Yoh 20:2

“Basi Petro akatoka, na yule mwanafunzi mwingine, wakashika njia kwenda kaburini,” Yoh 20:3

 “Basi akaja na Simoni Petro, akaingia ndani ya kaburi,” Yoh 20:6

“Basi ndipo alipoingia naye yule mwanafunzi mwingine aliyekuwa wa kwanza wa kufika kaburini, akaona na kuamini,” Yoh 20:8

TAFAKARI: “Na haya twayaandika, ili furaha yetu itimizwe.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Mtume Yohane na Mwinjili. Yohane mwana wa Zebedayo alikuwa mmojawapo kati ya Mitume wa Yesu, ambaye alipendwa na mwalimu wao kuliko wenzake wote. Mapokeo ya Kanisa yanamuona kuwa mwandishi wa Injili ya Yohane, wa barua tatu (Waraka wa kwanza wa Yohane, Waraka wa pili wa Yohane, Waraka wa tatu wa Yohane) na wa Kitabu cha Ufunuo.

Mtume Yohane alizaliwa na Salome baada ya  Yakobo Mkubwa mwanzoni mwa karne ya 1 B.K. akafa mkongwe mwishoni mwa karne hiyo huko Efeso (katika Uturuki wa leo). Kabla ya kumfuata Yesu Kristo alikuwa mvuvi na mfuasi wa Yohane Mbatizaji Ndiye shahidi mkuu wa miaka mitatu hivi ya utume wa Yesu, akiwa wa kwanza kumfuata (pamoja na Mtume Andrea), mshiriki wa matukio ya pekee ya mwalimu wake (kama alipogeuka sura mlimani), mtume pekee aliyesimama chini ya msalaba, wa kwanza kusadiki ufufuko wa Yesu hata kabla hajamuona.

Kutokana na udhati wa teolojia yake alifananishwa na Tai (Ndege) mwenye kuruka juu zaidi angani, na kuyaona yaliyo yote vizuri chini. Yohane Mtume anaheshimiwa na madhehebu karibu yote ya Kikristo kama Mtakatifu, hasa tarehe 27 Decemba.

Mpendwa katika Kristo, pamoja na Injili ya leo kuelezea tukio la ufufuko wa Bwana Yetu Yesu Kristu, Yoh 20:1,  imekazia mambo makuu mawili. Kwanza, nafasi ya Kanisa, na pili, nafasi ya Mtume Petro, ikiwa ni pamoja na kujitambua kwake Mtume Yohana ambaye leo kwa namna ya pekee tunaadhimisha sikukuu yake. Kwa namna ya pekee leo naomba tuyatafakari mambo haya.

Tuelewe kwamba Yesu Kristo alikwisha weka mfumo fulani wa uongozi kabla ya mateso, kifo na ufufuko wake. Ni katika mfumo huyo wafuasi wake wapaswa kuufuata. “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba wako huu nitalijenga Kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18. Jambo hili na nafasi hii ya Petro inajitokeza na kujionyesha wazi wakati wa Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. “Basi akaja na Simoni Petro, akaingia ndani ya kaburi,” Yoh 20:6.

Licha ya kwamba Mtume Yohani ambaye Yesu alimpenda sana kuliko Mitume wote, ikiwa ni moja ya sifa yake na uhusiano wake na Yesu Kristo, pia alikuwa ni kijani kuliko wote; hakuwa wa kwanza kuingia katika kaburi licha ya kwamba alikimbia kuliko Mtume Petro na kufika wa kwanza Kaburini baada ya kupata taarifa ya Kristo Mfufuka.

Yohane Mtume anatambua nafasi ya Petro kama kiongozi halali aliyepewa mamlaka na Kristo mwenyewe. Hapa ndipo tunapoona nafasi ya Baba Mtakatifu kama HALIFA wa Kristo. Huyu ndiye Petro, yaani mwamba ambapo Kanisa lake limeoteshwa na kukua. Na hapa ndipo tunapoona umoja wa Baraza la Maaskofu na Mwenyekiti wao kama msemaji Mkuu wa Kanisa mahalia.

Kwa sababu hiyo, Mtume Petro anakuwa wa kwanza kuingia Kaburini. Na baada ya Petro, Mtume Yohane anaingia na kuona na kuamini. “Basi ndipo alipoingia naye yule mwanafunzi mwingine aliyekuwa wa kwanza wa kufika kaburini, akaona na kuamini,” Yoh 20:8. Kuona na kuamini kwa Mtume Yohane, kunachukuliwa kwa namna mbili;

 Moja, Mtume Yohane mwenyewe kwa upendo aliokuwa nao Kristo juu yake, na upendo wa Mtume Yohane juu ya Kristo. Kwa kuonyesha furaha na upendo wake kwa Kristo, Yohana Mtume anaongea kwa niamba ya Kanisa, na kusema, “Na haya twayaandika, ili furaha yetu itimizwe,” 1Yoh 1:4

Pili, Yohane Mtume katika jambo hili la kuona na kuamini, anasimama badala ya Kanisa kama mshuhudia na mshuhuda wa kweli wa ufufuko wake Yesu Kristo. “Lile lililokuwako tangu mwanzo, tulilolisikia, tuliloliona kwa macho yetu, tulilolitazama, na mikono yetu ikalipapasa, kwa habari ya Neno la uzima,” 1Yoh 1:1. Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, huwezi kutoa ushuhuda wa Neno kama huna uwezo wa kulishirikisha Neno. Huwezi lishirikisha Neno kama ukuweza kulitafakari Neno hilo. Huwezi litafakari Neno kama ukuweza kulipokea Neno hilo. Na hutoweza kulipokea Neno kama ukulisikia Neno. Na “hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana nasi: na ushirika wetu ni pamoja na Baba, na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo,” 1Yoh 1:3

 Kumbe kuwa shuhuda wa Neno kutanipasa haya yafuatayo; kulisikia Neno, kulipokea Neno, kulitafakari (ikiwa ni pamoja na kulitafiti) Neno, na kulishirikisha Neno. Hatua hizi ndizo ziletazo uzima kwa Neno lile tuishilo. “(Na uzima huo ulidhihirika, nasi tumeona, tena twashuhudia, na kuwahubiri ninyi ule uzima wa milele, uliokuwa kwa Baba, ukadhihirika kwetu),” 1Yoh 1:1

Kanisa tuishilo leo na sasa linaishi katika ushuhuda huu wa Ufufuko. Kanisa halipo kama hakuna Imani hii ya Ufufuko. Je, jambo hili linasema nini kuhusu vipaumbele vyako katika Imani?

Ndugu yangu, yale ambayo yanachukua muda wako mwingi katika maisha yako, ndiyo hayo yanayo akisi maisha yako baada ya kifo. Yawezekana hadi sasa huna mpangilio wa maisha yako. Mambo ya muhimu kufanya katika maisha  yako mapya ya ufufuko ni haya;

Moja, Mshukuru Mungu kwa kukutumia vyema, endapo unaishi vyema utume wako kadiri ya wito wako. Katika jambo hili utafunuliwa siri ya umilele.

Pili, kila mmoja wetu yampasa kufanya mkataba na Kristo kama ishara ya kuanza maisha mapya ya ufufuko. Mkataba wako  ulenge kufanya jambo jema kwa ajili ya Kristo kila siku. Hapa haitegemei ukubwa wa jambo au udogo wake.

Tatu, lifanye jambo hilo kuwa kiu yako kila siku na usichoke kulifanya. Nakuhakikishia utaanza kuona mabadiliko makubwa katika maisha yako yakiambatana na Neema na Baraka za ajabu.

Nne, Sala kuu yako iwe kushukuru hata kwa yale ambayo bado kuyapata. Hapa ni kumwachia Kristo usukani wa maisha yako. Yesu Kristo ndiye dereva maarufu kuliko wote waliokwisha kutokea. Yeye ndiye “Njia, na Ukweli, na  Uzima,” Yoh 14:6

Na mwisho, omba kifo Chema kila siku na hasa mara uamkapo. Sala hii iambatane na Neema ya kutoa msamaha bila kujibakiza.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1

Ee Yesu, nijalie neema ya kutafuta yale yakuelekeayo katika maisha yangu kila siku. Amina.

Mtakatifu Yohana Mtume, na Mwinjili, Utuombee

No hay comentarios:

Publicar un comentario