miércoles, 21 de diciembre de 2016

TAFAKARI: DECEMBA 23, WIKI YA 4 YA MAJILIO


DECEMBA 23, WIKI YA 4 YA MAJILIO

Somo: Mal 3:1-4, 4:5-6

Zab: 25:4bc-5ab, 8-9, 10, 14

Injili: Lk 1: 57-66

Nukuu:

Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema Bwana wa majeshi,” Mal 3:1

 “Naye ataigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto wao, na mioyo ya watoto iwaelekee baba zao, ili nisije nikaipiga dunia kwa laana,” Mal 4:6

Mamaye akajibu akasema La, sivyo; bali, ataitwa Yohana,” Lk 1:60

Akataka kibao, akaandika ya kwamba, Jina lake ni Yohana. Wakastaajabu wote,” Lk 1:63

“Na wote walioyasikia wakayaweka mioyoni mwao, wakisema, Mtoto huyu atakuwa wa namna gani? Kwa sababu mkono wa Bwana ulikuwa pamoja naye,” Lk 1:66

TAFAKARI: “Kwake vyote vitafanywa upya.”

Wapendwa wana wa Mungu, mazoea hujenga tabia. Na tabia ya mtu kama ni mbaya huchukua muda sana kurudi katika njia iliyo sahihi. Kinyume cha kuhani aliyekuwa siyo mwaminifu, Nabii Malaki anatangaza siku ya Mungu ambayo itakuwa ya kutisha sana. “Lakini ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? Au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo,” Mal 3:2 

 Tunaweza kusoma habari hii ya kutisha ya siku ya Bwana pia kutoka kwa Nabii Amosi, 5:18-20, na Namii Joeli, 1:15-20. Katika hatua hii, Bwana atarudi katika hekalu lake na kulitakatifuza kwa moto, Eze 22: 17.22, na kumweka Kuhani Mtakatifu na sadaka ya haki itakayokubalika. “Angalieni, nitawapelekea Eliya nabii, kabla haijaja siku ile ya Bwana, iliyo kuu na kuogofya,” Mal 4:5. Kama ilivyokuwa kwamba huwezi kumwona Mungu bila kufa, Kut 33:20, Mungu alionekana kwa watu mfano wa Malaika, Mwa 16:7, Kut 3:2. Malaika wa agano ni Bwana ambaye anawatafuta watu wake, na siyo mjumbe.

Hii inamaanisha Mungu mwenyewe, anayeonekana, atakuwa muhuri wa agano hili jipya, Yer 31:31ff, kwenye Hekalu lake. Maneno haya yanamaanisha Yesu mwenyewe, Mt 11:10, Ebr 3:5-6. Ujio wa Bwana unamaanisha upya wa mambo na mtazamo wa maisha wa watu kuelekea  umilele. “Naye ataigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto wao, na mioyo ya watoto iwaelekee baba zao, ili nisije nikaipiga dunia kwa laana,” Mal 4:6. Kinyume cha baraka ni laana. Hivyo pona ya watu wake ni kufuata maagizo yake yenye uhai ndani yake.

Kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji kunathibitishwa katika uhalisia wake kwa tangazo la Malaika wa Mungu. Tunda la kwanza katika kuzaliwa kwake ni furaha. Yohana tunda la muujiza, halina uhusiano na watu; hitimisho lake halipo mikoni mwa familia yake, limefanywa hivyo na Mungu mwenyewe. Mungu amempa jina ambalo linaelezea hatma yake, Mwa 17:3-8, Mt 16:17-19. Yohana anauvunja mwendelezo uliokuwepo. Hivyo hataitwa Zakaria, jina lake  litakuwa Yohane, Lk 1:60.

Elizabeti kama alivyokuwa Ana mama yake Samuel, anajua mwanaye si mali yake. Mtoto Samweli alitwaliwa, na kuchaguliwa hata kabla ya kuzaliwa kuwa ni mali yake Bwana, Yer 1:5. Zakaria Baba yake Yohane anakubali hatma ya mtoto wake, na mdomo wake unafunguka na kumsifu Mungu. Haya ndiyo maajabu ya Mungu kwa watu wake. “Na wote walioyasikia wakayaweka mioyoni mwao, wakisema, Mtoto huyu atakuwa wa namna gani? Kwa sababu mkono wa Bwana ulikuwa pamoja naye,” Lk 1:66. Kwake Mungu vyote vitafanywa upya. Hakuna aliyekutana na Mungu katika hali yoyote ile akabaki kama alivyo kuwa mwanzo.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu,” Tit 3:5

Tusali:-Ee Yesu Mwema, yaanze yote upya katika maisha yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario