viernes, 23 de diciembre de 2016

TAFAKARI: KIPINDI CHA KUZALIWA BWANA, NOELI: MISA YA USIKU


KIPINDI CHA KUZALIWA BWANA

NOELI: MISA YA USIKU

Somo I: Isa 9:2-7

Zab: 96: 1-2, 2-3,  11-12, 13

Somo II: Tit 2:11-14

Injili: Lk 2:1-14

Nukuu:

“Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza,” Isa 9:2 

Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani,” Isa 9:6 

Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo,” Isa 9:7

“Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa,” Tit 2:11-12

“tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu,” Tit 2:13

“ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema,” Tit 2:14

Yusufu naye aliondoka Galilaya, toka mji wa Nazareti, akapanda kwenda Uyahudi mpaka mji wa Daudi, uitwao Bethlehemu, kwa kuwa yeye ni wa mbari na jamaa ya Daudi; ili aandikwe pamoja na Mariamu mkewe, ambaye amemposa, naye ana mimba,” Lk 2:4-5 

Ikawa, katika kukaa huko, siku zake za kuzaa zikatimia, 7 akamzaa mwanawe, kifungua mimba, akamvika nguo za kitoto, akamlaza katika hori ya kulia ng'ombe, kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba ya wageni,” Lk 2:6-7

“Na katika nchi ile ile walikuwako wachungaji wakikaa makondeni na kulinda kundi lao kwa zamu usiku, Lk 2:8 

Malaika akawaambia, Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana,” Lk 2:10-11 

Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hori ya kulia ng'ombe,” Lk 2:12 

Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia,” Lk 2:14 

TAFAKARI: “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.”

Wapendwa wana wa Mungu, usiku huu Mama Kanisa amejawa furaha isiyokifani kwa tukio hili la upendo na ukarimu uliotukuka wa Mungu kuchukua hali yate ya kibinadamu na kuwa sawa na sisi isipokuwa dhambi, ili kutukomboa na kututoa katika hali yetu ya dhambi na kufa. Hili ndilo fumbo tunalosheherekea leo, yaani, kumwilishwa, “neno kufanywa mwili na kukaa kwetu,” Yoh 1:14. Kipindi hiki cha kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo, yapo mambo makuu matatu tunayo yatafakari kwa kina katika umoja wake. Mambo haya matatu hatuwezi kuyatenganisha ingawa katika kuyaelezea ili kujua kilichojificha katika fumbo hili hatuna budi kufanya hivyo.

Kwanza kabisa kipindi hiki tuna tafakari kwa undani tendo zima la Mungu kuchukuwa hali yetu ya ubinadamu, yaani, ‘neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, “Verbum caro factum est.” Huu ni upendo mkubwa sana wa Mungu kwetu, na unyenyekevu wa hali ya juu alioufanya. Mtume Paulo analinena tendo hili kama NEEMA ya ajabu sana kwetu, ambayo Mungu anakubali kuwa masikini ili mimi na wewe tuwe matajiri. “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9. Hili ndilo kusudio kubwa la Mungu kwetu la kuchukua hali yetu ya ubinadamu. Mungu anaridhia tendo hili pasipo shuruti yoyote. Ni upendo tu. Hakuna shaka yoyote kwamba kwa tendo hili Mungu yupo tayari kuanza upya nasi. Na huyu ndiye Mtoto tuliyepewa leo. “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani,” Isa 9:6.  Huu ni ushindi mkubwa sana kwetu, tunapotolewa katika giza na kuwekwa kwenye mwanga. “Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza,” Isa 9:2. Hakika ingawa tunajua siku moja tutakufa, ila kuanzia sasa kifo hakina nguvu na mamlaka tena kwetu. Mtoto huyu atalikamilisha hilo pale msalabani. Jambo hili ndilo litakalo kamilisha safari yake hapa duniani. Ubinadamu huu wa Yesu, ambao ni tokea zima la fumbo hili la kumwilishwa ndio tunalolitafakari usiku huu.

Pili, katika kipindi hiki cha kuzaliwa Bwana na mwokozi wetu, tuna tafakari kwa undani hali yetu ya ubinadamu ya kuinuliwa na kufikia hali ya Umungu ndani na katika Kristo Yesu, “Et habitabit in nobis.” Ni kwa kupitia Mtoto huyu aliyezaliwa leo kwamba, “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo,” Isa 9:7. Hapa kila mmoja wetu anarudishiwa hali yake ile ya kutokufa iliyosababishwa na anguko la wazazi wetu wa mwanzo, Adamu na Hawa. Kumbe ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, zawadi yako kubwa unayoweza kumpa Mungu katika kipindi hiki ni kuongoka kwako. Mungu anakutaka wewe na mimi katika ujumla wake na siyo nusunusu, au asilimia kadhaa tu.

Tatu, katika kipindi hiki cha Noeli, tuna tafakari kwa undani tendo la kufanywa vyote vipya katika uumbaji wa Mungu, “Ecce nova facio omnia.” Ni kwa kupitia Kristo ambaye ni Adamu Mpya nasi twafanywa wapya na kuwa warithi wa ufalme wa Mungu. Tendo hili la kufanywa vyote upya ndani na katika Kristo linaenda sambamba na kufanya kwetu toba na majuto ya kweli. Hivyo katika hali hii ya furaha kwa kuzaliwa kwetu mwokozi na mkombozi, ni mwito pia wa kufanya toba na majuto ya kweli ili tufanywe upya ndani na katika Kristo. “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani; ambaye ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu,” Mdo 3:19-21. Nyakati za kuburudishwa ndio sasa.

Hayo mambo makuu matatu ni NEEMA kubwa sana kwetu katika kipindi hiki cha Noeli. Neema hii kwa tendo la ‘neno kufanyika mwili na kukaa kwetu,’ imemiminwa na Mungu kwa watu wote. “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa,” Tit 2:11-12. Msingi wa haya yote ni uwepo wa Kristo duniani kama Neema ya Baba. Kwa lugha nyingine, Kristo Yesu ambaye ndiyo UPENDO wa Dhati wa Mungu kwetu, katika tendo hili la kumwilishwa anakuwa “CHRISTOGENESIS” katika ulimwengu huu kama Nguvu-Upendo ya mabadiliko yote. Na hii ndiyo maana ya maneno haya, kwamba, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Kwa maisha ya Kristo na neno lake, yanatupa mafundisha halisi, na njia ya kufuata. Yesu “ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema,” Tit 2:14. Hili ndilo tumaini la kweli na lenye uhakika katika maisha haya mapya tunayosheherekea leo, na “tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu,” Tit 2:13. Hivyo ndugu zangu leo kwa namna ya pekee tunautazama ubinadamu ya Kristo, na Kesho kadiri ya liturjia tutatafakari Umungu wa Kristo.

Hivyo, Injili yetu ya leo inatufikirisha zaidi katika ubinadamu wa Kristo. Hivyo kuzaliwa kwake Mwokozi na Mkombozi wetu Yesu Kristo, kumechukua taratibu zote za kila siku na mahangaiko ya kila siku ya mwanadamu. Nyakati hizo karibia na kuzaliwa kwake Mtoto Yesu, linatoka tangazo la kujiandikisha kwa lengo la kujua idadi ya watu. Huu ni utaratibu wa kawaida wadola yoyote ile yenye mpango wa maendeleo kwa watu wake. Takwimu hizi za sensa husaidia kujua ni wapi kuna uhitaji zaidi na ni nini cha kufanya. Kuitikia wito huu, “Yusufu naye aliondoka Galilaya, toka mji wa Nazareti, akapanda kwenda Uyahudi mpaka mji wa Daudi, uitwao Bethlehemu, kwa kuwa yeye ni wa mbari na jamaa ya Daudi; ili aandikwe pamoja na Mariamu mkewe, ambaye amemposa, naye ana mimba,” Lk 2:4-5. Kwa tendo hili, Mungu anashiriki misukosuko na mahangaiko yetu licha ya Ukuu aliyo nao. 

 Ubinadamu huu wa Kristo tunaoutafakari usiku  huu unatukumbusha kwamba historia ya mwanadamu ipo mikononi mwa Mungu. Ni kwa namna hiyo kwamba ukubwa wa himaya ya dola ya Kirumi unaishia horini ambapo kuna katoto kachanga kalichofungwa nguo za kitoto, naye ndiye Yesu. Yesu hapa ni alama halisi ya Upendo na Huruma ya milele ya Mungu, naye ndiye Mungu, Yoh 1:1. Waliofika kushuhudia upendo na huruma hii ya milele ya Mungu ni wale walio masikini na waliodharauliwa sana katika jamii. Hawa ndio wale wachungaji ambao mchana na usiku waliishi na mifugo huko makondeni. “Na katika nchi ile ile walikuwako wachungaji wakikaa makondeni na kulinda kundi lao kwa zamu usiku, Lk 2:8.  Pamoja na udogo wao na hofu waliyokuwa nayo kwa kile kilichotokea kisicho cha kawaida, kikiambatana na ishara nyingi, wanapata fursa ya kwanza kuyashuhudia mambo makuu ya Mungu. Wakiwa katika sintofahamu hii, “Malaika akawaambia, Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote; maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana,” Lk 2:10-11. Huyu ndiye Mungu anayemsema Bikira Maria katika utenzi wake ule wa ‘Magnificat,’-Wamtukuza,  kwamba, “Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Hakika Mungu ni wa ajabu sana!

Wapendwa katika Kristo, ni katika Yesu Kristo tunaona muunganiko wa umasikini wa watu na Mungu. “Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hori ya kulia ng'ombe,” Lk 2:12. Hivyo alama za Mfalme wetu aliyezaliwa leo ni kama zifuatazo; vipande vya vitambaa, nguo za kitoto, mtoto, na hori,  “umasikini.” Katika hali hii, Yesu ni sifa kwa Mungu na Wokovu kwa watu. “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.”  Pamoja na Ufalme aliokuwa nao Yesu kupita falme zote za dunia hii alikoswa mambo muhimu sana kupita hata kwa maisha ya mtu wa kawaida. Kama Mfalme basi ingetazamiwa azaliwe kama siyo kwenye hospitali nzuri na zenye huduma bora, basi ingekuwa kwenye moja ya majumba mazuri ya kifalme. Lakini badala yake kazaliwa kwenye hori la ng’ombe.

Kama Mfalme, tulitegemea kungekuwa na nderemo kila kona na viungo vyote vya miji ya Israeli na dunia nzima huku shangwe hizi zikisindikizwa na kwaya mashuhuri kuutubuiza usiku huu wa ajabu kwa kuwa Mungu yule aliyekuwa mbali sasa yu nasi, naye ni Emanueli, yaani, Mungu pamoja nasi. Badala yake bila shaka kulikuwa na kwaya ya nzi wengi wakisaidiana na mbu, kwani mahali pale alipozaliwa palikuwa holini mwa ng’ombe. Huyu ndiye Mungu aliyekubali kuchukua na kushuka chini kabisa katika hali na ubinadamu wetu.

Tukio hili na mazingira haya ya kuzaliwa Mwokozi wetu linanikumbusha tukio la kujifungua kwa Yosephina mke wa Barnaba. Yosephina na Barnaba ni wakulima wa kawaida sana. Mapato yao yalikuwa ni kutoka mkononi kwenye kinywani. Hivyo hawakuwa na akiba yoyote. Waliishi kwa kudra ya Mwenyezi Mungu. Kazi nzito kipato kidogo. Haya ni maisha ya familia nyingi tunazoishi leo. Hata usiku huu kati yetu tupo katika ukweli huu wa Yosephina na Barnaba. Maisha yao ya umasikini, yaani Yosephina na Baranaba, uliweza kuyatabiri haraka kwa namna ya vaa yao. Mama huyu hupenda kujifunga kanga nyingi sana kiunoni na wakati mwingine hufanana na mwanasesere.

Siyo ukweli kwamba Yosephina alipenda kufanya hivyo ili kuwachekesha na kuwafurahisha watu, ila ukweli ni kwamba kila kanga aliyojifunga ilikuwa na matobo. Hivyo kujifunga zaidi ya kanga moja alikuwa na lengo la kuyafunika matobo. Ni kwa namna hiyo kila kanga ilikuwa na kazi yake. Binafsi niliyapenda maisha yao na ushiriki wao katika Jumuiya, ingawa nilihuzunishwa sana na hali ya umasikini wao. Ndoa yao ni kati ya ndoa zile zilizofungwa kwa kundi la wanandoa wengi. Hata hivyo ilikuwa ni familia yenye furaha sana.

Yosephina na Mumewe Barnaba hupenda sana kuudhuria misa za asubuhi na baada ya tendo hilo la ibada huelekea pamoja mashabani mwao. Hakika maisha yalikuwa “HAPA KAZI TU,” licha ya ukweli wa mazingira magumu ya kazi na kipata kidogo. Akiwa mjamzito na kukaribia kujifungua, alifika Misa ya asubuhi kama kawaida na baada ya Misa walielekea mashambani. Mara walipofika shambani hali ilibadilika na ilimlazimu Mumewe amsaidie kujifungua. Mungu mwema, zoezi hili lilikwenda salama. Baada ya saa moja tu ya mapumziko, walikiweka kichanga chao chini ya kivuli cha mti kikiwa kimeviringishwa kanga mbili zenye mipasuko juu ya godoro zuri la nyasi kavu na kuendelea na kazi. Jioni ilipowadia, walirudi nyumbani na kachanga chao. Maisha yaliendelea kama kawaida.

Wapendwa hata katika hali hizi za kutisha, Mungu hutulinda kwa namna ya ajabu sana. Huyu ndiye Mungu aliyekuja kutafuta kile kilichopotea. Leo tunaposheherekea siku hii ya kuzaliwa Mwokozi na Mkombozi wetu, ni mwito vile vile wa kuwafikiria wengine hasa majirani zetu ambao hakika leo hawajui watakula nini. Noeli ni sikukuu pia ya Familia. Tusipoutazama utajiri wa Mungu na utayari wake wa kuwa masikini ili sote tuwe matajiri, tukio hili la kuzaliwa Mwokozi na Mkombozi katika maisha yetu halina maana kabisa. Ni vyema kujiuliza maswali haya;

Je, tukio hili la kuzaliwa Kristo lina tafsiri gani katika maisha yangu? Je, ni mfululizo tu wa moja ya siku za kihistoria ninazozijua na kuzisheherekea kama nilivyozikuta katika jamii ninayoishi, au kuna kitu kikubwa zaidi ya hicho?

Je, kuzaliwa Kristo kwangu ni kipindi cha kuzama zaidi katika fumbo hili la kumwilishwa, na kuona mahitaji ya wengine kama Mungu alivyoona hitaji letu na kutukomboa, au ndiyo fursa mpya ya kula, kunywa, kuvaa, na kufurahia biashara yangu kama mfanyabiasha kwa kuuza zaidi, kufurahia mateso ya wengine hasa pale tunapojisikia huru kwa vile tumeshawanyamazisha?

Wapendwa wana wa Mungu, lazima tuelewe jambo hili; Kristo amemwilishwa ili kutufanya nasi kuzaliwa wapya ndani na katika historia ya wanadamu. Hivyo mimi binafsi bila kutambua na kutaabika kwa ajili ya wahitaji na hasa wanaonizunguka, ni kupungukiwa utoshelevu katika Kristo na fumbo zima la kuzaliwa kwake  kwangu na kwetu.

Kama binadamu halisi, Kristo kazaliwa ili kutupeleka katika hali ya juu ya Umungu wa Mungu. Hii ni heshima kubwa sana kwetu. Je, kwa nafasi niliyonayo na uwezo niliojaliwa na  Mungu, ni wangapi walioduni kabisa nimeweza kuwafikisha katika hali ya maisha ninayoishi? Kuzaliwa kwa Kristo ndio mwanzo wa safari ya sisi kuzaliwa wapya ndani na katika Yeye.

Tumsifu Yesu Kristo!

Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia,” Lk 2:14

Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wangu, nifanye chombo chako cha haki, amani, upendo, wema, kweli, msamaha, na huruma. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario