miércoles, 28 de diciembre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA FAMILIA TAKATIFU; YESU, MARIA, NA YOSEFU


SIKUKUU YA FAMILIA TAKATIFU MWAKA-A

Yesu, Maria, na Yosefu

Somo I: YbS 3:3-7; 12-14

Zab: 128: 1-2, 3, 4-5

Somo II: Kol 3:12-21

Injili: Mt 2:13-15, 19-23

Nukuu:

“Amheshimuye baba yake atafanya upatanisho wa dhambi, naye amtukuzaye mama yake huweka akiba iliyo azizi,” YbS 3:3-4

“Amheshimuye babaye atawafurahia watoto wake mwenyewe, na siku ya kuomba dua atasikiwa,” YbS 3:3:5

“Amtukuzaye baba yake ataongezewa siku zake; akimsikiliza Bwana, atamstarehesha mamaye, na kuwatumikia wazazi wake kama mabwana. Mwanangu,” YbS 3:6-7

“Mwanangu, umsaidie baba yako katika  uzee wake, wala usipate kumhuzunisha siku zote za maisha yake,” YbS 3:12

 “Akiwa amepungukiwa na ufahamu umwie kwa upole, wala usimdharau iwapo wewe u mzima sana,” YbS 3:13

Mwenye kumdharau baba yake ni mfidhuli, naye mwenye kumlaani mama yake amekwisha kulaaniwa na Bwana,” YbS 3:16

Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi,” Kol 3:12-13

Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu,” Kol 3:14

 Ninyi wake, watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana. Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao,” Kol 3:18-19

Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana,” Kol 3:20

Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa,” Kol 3:21

Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize,” Mt 2:13

“Ndipo Herode, alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi,” Mt 2:16

TAFAKARI: Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu,” Kol 3:14

Wapendwa wana wa Mungu, leo tukiwa bado katika kipindi cha kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo, Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Kwa namna ya pekee leo, masomo yote matatu yanamulika swala zima la Familia, muundo wake, wajibu wake kwa ujumla na kila mmoja katika familia kadiri ya nafasi yake, Mahangaiko ya familia, na kutengemaa kwa familia yenye kujali na kuwajibika. Bila shaka msingi wa familia ni ule moyo ya upendo wenye kuzaa hali ya kuvumiliana na kutabikiana. Hiki ndicho kifungu cha ukamilifu. Kama asemavyo Mtume Paulo, “Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu,” Kol 3:14. Tukiachia mbali hii Familia Takatifu ya Yesu, Marian na Yosefu, familia zetu si kamili katika maana ya Utakatifu. Familia yetu zina madhaifu mengi sana. Lakini familia hizi ambazo ni dhaifu husimama imara pale wanapotazama, jifunza, na kuishi Utakatifu wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu kama mfano ulio hai wa kuiga.

Ni wazi kwamba familia iliyosimama katika kweli, haki, upendo, huruma, na kusamehana si kazi rahisi na si kazi ya siku moja. Leo tunaposheherekea Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, haikuwa kazi rahisi kwa Maria na wala Yosefu kumlea mtoto Yesu. Tuelewa kwamba Yesu ni Mungu na Mwanadamu. Asili hizi mbili zilileta sintofahamu nyingi kwa Maria na Yosefu katika malezi ya Mtoto Yesu.

Uwepo wa Yesu ulikuwa tishio kubwa sana wa utawala ule wa Herode ambaye mamlaka yalikuwa kila kitu kwake. Hivyo kwa kusikia yaliyosemwa juu ya Mtoto Yesu, Herede anaingiwa na hofu na kuruhusu umwagikaji wa damu zisizo na hatia. Njia aliyochukua Herode haina tofauti na watawala wetu wa leo wanapopatwa na hofu juu tawala zao za mabavu. Wapo wengi wanaouwawa kila dakika ulimwenguni na hasa nchi zetu za kiafrika kwa sababu ya hofu ya madaraka yaliyobebwa na utawala dhalimu.

Hivyo kuhakikisha anamwangamiza Mtoto Yesu, tangazo linatolewa mara moja baada ya kujua wale Mamajusi wamemdanganya kadiri ya maagizo aliyokwisha wapa, yaani, “Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie,” Mt 2:8. Wakijua nia yake mbaya juu ya mtoto Yesu, Mamajusi walishika njia nyingine baada ya kumsujudu mtoto Yesu na kutoa zawadi zao.

Hapa ndipo lilipotolea tangazo la kuwaangamiza watoto wasio na hatia. “Ndipo Herode, alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi,” Mt 2:16. Nguvu ya Mungu na mpango wake kwa wale aliorithia nao ni tofauti na mipango yetu ambayo kwayo haina uzima ndani yake.

Kama Mungu ndiye mweza wa vyote hakuna chochote kitakachozuia mpango huo, kwani nasi kama tulivyo na mamlaka tuliyonayo humtegemea Mungu huyu huyu. “Na hao walipokwisha kwenda zao, (Mamajusi) tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize,” Mt 2:13. Ni nani kama Mungu wetu? Leo tunajionea wenyewe baadhi ya tawala ambazo hazipo tayari kuachia dola kwa AMANI, na hivyo kuleta maafa makubwa ya mauaji ya watu wasio na hatia. Pamoja na ukatili huu, uovu hauwezi kudumu katika umilele wake, kwa sababu uovu hauna umilele. Wale wote wauteteao na kuulinda uovu ujichosha kure. Hivyo, “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure,” Zab 127:1

Hali na mazingira haya yanaleta hofu kubwa sana katika familia hii Takatifu. Hivyo kama mazingira na hali ya ukimbizi tuionayo leo, hata Yesu ameipitia. Na yanapotokea maafa kama haya wanaotesema ni akina mama na watoto. Mama Marian a Yosefu wanayanusuri maisha ya Mtoto Yesu kwa kukimbilia Misri. Familia hii Takatifu inaishi maisha ya ukimbizi. 

Pamoja na sintofahau hizi, na malezi ya Mtoto Yesu, Bikira Maria alikuwa na muda mwingi wa kutafakari haya asiyoyafahamu. “Lakini Mariamu akayaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake,” Lk 2:19. Kuyaweka moyoni ni kuyapa nafasi ya tafakari kwa yale tusiyoyajua. Je, wewe kama mzazi mwanao anapofanya ndivyo sivyo, wajiuliza kwa nini amefanya kama alivyo fanya? Kujua chanzo cha tatizo ni bora kuliko kukimbilia kulitatua tatizo. Hivyo tafakari ya Bikira Maria ilimsaidia kufahamu uwezo na kile alicho mwanaye Yesu Kristo.

Muujiza wa kwanza ya Yesu kule Kana unathibitisha ufahamu wa Maria juu ya mtoto wake. Kulipotokea upungufu wa divai, Bikira Maria alienda moja kwa moja na kumwambia Yesu, Mwanaye, kwamba hakuna divai. Bikira Maria hakubaki na jibu la mwanaye, ila alienda moja kwa moja kwa wale wahudumu na kuwaambia,  “Lo lote atakalowaambia, fanyeni,” Yoh 2:5. Kwa tendo hili hakuna shaka kwamba Mama Bikira Maria anaufahamu uwezo wa mtoto wake. Je, leo wazazi wangu muna muda wa kutosha kuwafahamu watoto wenu ikiwa ni pamoja na tabia zao? Basi tujifunze kwa Mama Bikira Maria. Leo tunapoongelea familia na hasa zenye malengo na mwelekeo, tunaongelea familia ndani ya ndoa Takatifu yenye kujali na kuwajibika. Hivyo ni vyema kujua fumbo zima la ndoa na chimbuko la famila kama tunda na matokeo ya ndoa hiyo.

1. Fumbo zima la ndoa na chimbuko la familia

Wapendwa wana wa Mungu, upendo huu wa Mungu kwa watu wake yatupasa kuuona katika mambo yote yenye kutupeleka katika umoja wake, upendo wake, ushirikiano wake na hata katika maagano yetu katika maisha. Ni kwa kupitia umoja huo, upendo huo, na ushirikiano huo wa Mungu na mwanaye mpenzi, Yesu Kristo Mungu hujidhihirisha kwetu kila siku ya maisha yetu hapa duniani. Upendo wa Mungu na mshikamano na mwanaye tunauona katika masakramenti yake, na hasa leo tunavyotafakari kwa ukaribu sakramenti hii ya ndoa. Naye Mtume  Paulo anasema, “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili,” Efe 5:22-23. Hapa upendo wa Mungu kupitia Kristo mwenyewe unaonekana kwa utii huu wanaoishi wana ndoa, na hasa kwa mke kumtiii mumewe. Je, ndoa zetu leo ni salama? Akina mama mnaishi ukweli huu katika agano lenu la ndoa? Leo baadhi ya wanawake wamefikia kuwaita waume zao vyuma chakavu. Je, hayo ndiyo makusudio ya Mungu na muungano wenu huo?

Kwa upande wa wanaume yawapasa kuwapenda wake zao katika kweli na haki. Upendo huu unafananishwa na upendo wa Kristo na Kanisa lake. “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa,” Efe 5:25-27. Wanaume zieshimuni ndoa zetu kwani ndio utakatifu wenu mnapoziishi katika kweli na haki. Wake zenu hawahitaji mambo ya pekee sana zaidi ya kuyasadifu yale wayatendayo kila siku katika familia. Tabia ya kuwaita wake zetu magoli kipa ni chukizo mbele ya Mungu. Muunganiko wenu ni makusudio ya Mungu, na ndivyo alivyoona inafaa.

Utii wa kweli si utumwa kwenu, bali ni ukamilifu wa makusudio ya Mungu katika maisha ya umilele. Wito wenu wa ndoa ni kuufikia umelele wa maisha yenu mlioandaliwa kupitia sakramenti hiyo. Hivyo, “kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo,” Efe 5:24. Ni kuwa na utii katika Kristo kwa sababu yeye anayo maneno la uzima wa milele. Ni kwa kupitia NENO huyu vyote vilifanyika, na kwa kupitia NENO huyu vyote huwa na uzima wa milele, Yoh 1:3. “Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja,” Efe 5:31. Tendo hili la ajabu katika sakramenti hii ya ndoa halimwesabii haki mmoja wa wanandoa kuwa na mambo yake ya pekee na binafsi tena. Hakuna msamiati huu tena wa kusema hiki changu na hiki chako. Kwa kufanya hivyo ni kuujeruhi mwili huu mmoja. Je, jambo hili lina ukweli katika ndoa yako? Je, ni mambo mangapi ya siri unayoyafanya bila kumuhusisha mwenzi wako wa ndoa? Je, hujui kwa kufanya hayo unaijeruhi ndoa yako? Ndugu yangu kama unaishi ukweli huu na kinyume cha sakramenti hiyo ya ndoa, elewa kwamba ndoa hiyo ishakufua katika uhalisia wa mambo na ukweli wa Kimungu. Kilicho baki ni maagizo kuu, na wote mmekuwa wasanii katika sakramenti hii Takatifu.

2. Changamoto kwa watoto na wajibu wao katika familia:

Ni ukweli usiotia shaka kwamba ni wajibu wetu kuwaheshimu wazazi wetu ikiwa ndiyo amri ya nne ya Mungu. Tokeo hilo linatupa heri na miaka mingi katika maisha ya umilele. “Amtukuzaye baba yake ataongezewa siku zake; akimsikiliza Bwana, atamstarehesha mamaye, na kuwatumikia wazazi wake kama mabwana. Mwanangu,” YbS 3:6-7. Tendo la kuwapenda wazazi ni haki na linapendeza machoni mwa Mungu. Ni haki kama asemavyo Mtume Paulo, "enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki," Efe 6:1. Pia tendo hilo lapendeza machoni mwa Mungu, "ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hii lapendeza katka Bwana," Kol 3:20.

Kwa mantiki hiyo, mtume Paulo anaenda mbali na kutupa angalisho kuhusu kuwatii wazazi wetu, na kusema, "maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi," 2 Tim 3:2. Kwa hiyo ndugu yangu jambo hilo ni wajibu, ni shukrani na ni safi kufanya hivyo. “Mwenye kumdharau baba yake ni mfidhuli, naye mwenye kumlaani mama yake amekwisha kulaaniwa na Bwana,” YbS 3:16.  Kwa upande mwingine wazazi ndiyo vielelezo vya Mungu wakiwa kama washiriki wa Mungu katika uumbaji. Kazi hii hata Malaika hakupewa. Ndugu yangu huna Baba zaidi ya Baba uliye naye. Hata kama ni mwendawazimu huyu ndiye Baba yako na unapomweshimu na kutimiza wajibu wako hapo ndipo penye chemchemu ya neema zote. “Amheshimuye baba yake atafanya upatanisho wa dhambi, naye amtukuzaye mama yake huweka akiba iliyo azizi. Amheshimuye babaye atawafurahia watoto wake mwenyewe, na siku ya kuomba dua atasikiwa,” YbS 3:3-5.

Hivyo ni wajibu wa kila mtoto katika familia kuwaheshimu, kuwajali na kuwatunza wazazi katika uzee wao. Tendo hili linakukumbusha kutoa shukrani kwa majitoleo yao katika maisha yako. “Mwanangu, umsaidie baba yako katika  uzee wake, wala usipate kumhuzunisha siku zote za maisha yake. Akiwa amepungukiwa na ufahamu umwie kwa upole, wala usimdharau iwapo wewe u mzima sana,” YbS 3:12-13. Ndugu yangu, namna unavyomjali na kumweshimu mzazi wako ni kwa namna hiyo hiyo utakavyo heshimiwa na kujaliwa na wanao ufikiapo uzee wako. Ni vyema ukawekeza kuanzia sasa katika jambo hili la muhimu katika maisha.

3. Changamoto za wazazi kwa watoto wao, na hasa malezi:

Pamoja na hayo niliyokwisha kuyasema, wazazi yawapasa kuheshi matakwa ya watoto wao ikiwa ni pamoja ya  ndoa za watoto wao wakijua wajibu wao wa kimalezi na kuwaacha watoto wao kuwa huru kuchagua mwenzi wake wa maisha. Pia wapo wazazi wengi wanaowageuza watoto wao kama miradi yao. Kikomo cha famili na kugawanyika ni pale watoto ndani ya familia wanapofikia kuwa na familia. Hili mzazi lazima ulijue na ujiandae vizuri hasa kisaikolojia. Hata kama unampenda vipi mtoto wako huwezi kuzuia asiumwe, asipate matatizo, na wala asife. Cha kushangaza, unakuta binti kaolewa na mara kwa mara mama mzazi yupo beneti naye kwenye shughuli zake, biashara zake, bila taarifa ya Mume wa binti yake. Ndoa ni ya watu wawili. Muwaache. Wewe mama kila mnada unapenda kwenda na binti yako kwa nini?

Jambo lingine la wazazi ni manyanyaso kwa mwali wao. Manyanyaso yakimfumo yasiyokwisha. Mnamfanya mwali wenu kama remote/kiongozea mbali. Anakuwa kama dekio lenu. Mwajiona ndoa yenu ni bora kuliko ya mwali huyu. Mbona yenu hatuyasemi. Yawezekana wewe ulimpenda huyo mume wako kwa kipande tu cha muwa. Usicheke! Kinachowaunganisha wawili na kuwa familia ni fumbo kubwa sana. Hivyo, “Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa,” Kol 3:21. Waacheni waishi maisha yao. Ni kweli yawezekana kabla ya mtoto wenu kuoa au kuolewa vimiminika (tumafuta, tusukari, tunyama, tunguo twa mtimba, na hata tupesa) vilikuwa vingi nyumbani. Baada ya ndoa, hayo yamepungua au kutoweka kabisa. Je hamjui ya kwamba, "kwa sababu hayo ndiyo mlioitiwa ili mrithi baraka?" 1Pt 3:9c. Kuyakosa hayo isiwe kero na shiiida kwa ndoa yao.

Ndoa inakuwa na uhai haya yakizingatiwa kadiri ya mtazamo wa Mtume Petro. "Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka," 1Pt 3:8-9.

4. Changamoto za leo kwenye familia, na wajibu wake:

Ndugu yangu, maneno hayo ni mazito sana kwa wanandoa. Kwa upande wa kina mama, wapo wanaoishi kwenye ndoa bado hawana utambuzi au tofauti na usichana wao. Mama kwenye ndoa tambua kwamba kila siku yakupasa "kupungua" kwa ajili ya familia yako "iongezeke." Familia yaani Baba na watoto wenu waongezeke; upendo, furaha,  afya, akili na mambo mengine mengi tu. Je, utapunguaje? Mtume Petro anatuambia, "kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi; bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyo haribika; yaani roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu," 1Pt 3:3-4. Mtume Petro hapa hapingi mama usiende saloon au kutokuvaa vizuri; bali muelewe kwamba hayo siyo vipauwa mbele katika familia.

Wengi tumetumia muda mwigi nje badala ya ndani. Vikao kila siku visivyoisha. Sema za kiroho januari hadi decemba, mikutano ya injili hadi manane ya usiku, nk. Je, saa ngapi utaijenga nyumba yako? Huku ni kukosa busara kama tunavyoaswa, "Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe, kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili," Mit 11:22. Kwa maana hiyo, "kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe," Mit 14:1. Wakati mwingine tunamtafuta mchawi wakati mchawi mwenyewe ndiwe wewe. “Ninyi wake, watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana. Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao,” Kol 3:18-19. Huu ni wajibu msingi katika maisha ya ndoa na ufahamu wake.

Wanawake wengi ni wawivu kupindukia. Jua likichomoza tu utakuta mkeka upo nje. Nikujigalagaza kwenye mkeka kama dagaa wa kigoma. Masikini wa Mungu labda mumewe alivutiwa na umbo lake la kushikika, baada ya nusu mwaka afadhali ya mkuyu wa handeni. Licha ndoa ni zaidi ya haya ya nje, ila nayo huleta matamanio ya kutazama kwingine kama tulipo kuna pazia na kiza. Elewa mumeo kama ameajiriwa au kujiajiri mwenyewe, awapo huko naye ameolewa na hiyo kazi yake. Awapo nyumbani anaitaji amani na utulivu. Wanawake wengi hawana muda wa kuyasoma mapigo ya mioyo ya waume zao. Mmewe akifika nyumbani tu anadakiwa mlangoni na risala ya mahitaji; utasikia, unajua hakuna sukari, chumvi, unga, nk. Mpe kwanza nafasi ya kupumzika. Muulize habari za huko alikotoka. Muulize angependa kupata nini kabla ya ulichoandaa. Wakati mwingine kuandaa meza anafanya mfanyakazi wa ndani. Au akifanya yeye utashangaa. Ugali kaupika saa sita mchana  wakati mumewe kafika nyumbani saa kumi jioni. Ugali unatoka jasho tu. Kwa nin usiandae mboga tu na wakati mumeo anapata chai ukawa unasonga ukali?

Angalia! Huko alikotoka kila mahali kuna ‘bar’ na nyama choma. Na nyumba nyingi pembezoni mwa barabara kuna kibao kimeandikwa "vyumba bado vipo." Ni kwa namna hii sebule ujeuka kuwa kwenye Bar. Pale anahudumiwa vizuri na kwa ujuzi. Huuliwa, "uncle tukusaidie nini? Anajibu, "bia, kilimanjaro." "Ya baridi "au ya moto? Mhudumu anasisitiza. Kwa vile nyumbani weshagombana na mkewe, anajibu, "ya baridi." Tazama binti huyu hakai mbali na mteja wake. Wewe ulipomwandalia chakula ulirudi kwenye mkeka wako. Binti huyu hukaa nyuzi 45 hivi. Baba huyu akimeza fundo moja la bia ananyanyua macho anakutana na tabasam. Kama Baba huyu alikuwa na mpango wa kunywa bia moja huongeza zadi 5. Hapa kwishakuwa sebuleni pake. Nani wa kulaumiwa?

Wanawake wengi huwasema vibaya sana waume zao. Wengine ufikia hata kuwaita waume zao "vyuma chakavu," kama nilivyokwisha kusema hapo mwanzo. Onyaneni kindugu tena mkiwa chumbani.

Baadhi ya wanaume nao ni balaa! Kumtukana hata kumpiga mkewe mbele za watu au marafiki zake na watoto ni fursa. Ona matusi hayo anavyoyafyatua kama bomu la skadi. "Mwanamke gani wewe nimekuokota bar? Bado sijaoa!" Unayasema maneno haya mbele ya watoto wako. Hata kama ni kweli hubakia maumivu makubwa kwa watoto.  Mtume Petro anasema, "ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu, na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe." 1Pt 3:7. Mke wako haitaji ununulie ndege ili awe na furaha. Ni wewe tu kusadifu kila kitu kidogo anachokifanya nyumbani. Mmefikia hatua ya kuwaita wake zenu "magoli kipa." Mkimaanisha wao ni kudaka tu! Jambo hili halipendezi mbele ya Mungu. Nyote wawili yawapasa kusomana tabia na kupongezana kwa kila kitu mfanyacho kizuri. Mmeo akikununulia kitu kabla ya kukikosoa mpongeze na kumwambia siku nyingine ukitaka ninunulia kitu itapendeza tukienda sote wawili. Kiukweli Wanaume hatuna uhalisi wa kuchambua uzuri kama uzuri, tupo zaidi katika idadi ya kitu au vitu.

Wapendwa wana wa Mungu, wazazi wetu wana nafasi yao muhimu sana katika maisha yetu kama viumbe shirikishi katika uumbaji na Mungu, mahusiano yetu kimaagano yana nafasi yake katika umilele wetu, na hivyo isiwe sababu ya kudharau au kukengeuka na kuwakana wazazi wetu. Mwisho yatupasa kujua wajibu wetu kwa wazazi, maisha yetu ya kimaagano kila mmoja kadiri ya wito wake, na kusudi la kuumbwa wetu na uwepo wetu hapa duniani. Yote haya ni maandalizi ya maisha ya umilele, kama ilivyo amri ya nne wa Mungu, Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana, Mungu wako,” Kut 20:12

Kijana Felix aliyemaliza masomo yake ya udaktari alibahatika kumwoa mwanamke mwenye elimu kama yake. Mwanamke huyu alijipenda sana kupita kiasi kutokana na mazingira ya makuzi yake. Ni kweli alitoka familia yenye pesa na tajiri sana.

Felix alitoka familia masikini sana, na soma yake ilikuwa ya shida sana. Felix alifika hapa alipo kwa kutegemea biashara ndogo ndogo za mama yake mzazi. Baba yake Felix alifariki muda mrefu, Felix angali darasa la pili.

Akiwa ameajiriwa na kuwa na mji wake, mama yake mzazi alipenda kumtembelea mtoto wake. Kwa bahati mbaya au nzuri Mama yake Felix alifika na kumkuta mke wa mtoto wake. Kwa namna alivyokuwa mama yake Felix, mke wa Felix alikuwa na mashaka naye kwani alionekana kama ombaomba fulani hivi. Hata kwa kujitambulisha kote kule mke wa felix hakuweza kumpokea vizuri na kulazimika kumwifadhi moja ya vyumba vya stoo.

Alipofika Felix kutoka kazini mkewe alimwambia ujio wa mwanamke mmoja mchafu na waajabu kutokea, na kusema, “eti mama huyo hapa stoo anasema kuwa wewe ni mwanaye.” Felix kwa aibu naye hakumpokea vizuri mama yake, na ndipo ugomvi ulipoanzia. “Kama unasema kuwa wewe ni mama yangu piga mahesabu ya gharama zote ulizonitunza na kunilea nami nitakulipa,” Felix alimwambia mama yake kwa hasiri.

“Naombeni munionyeshe uhani nami nikirudi nitakupa hesabu yangu,” mama yake Felix mjibu Felix. Baada ya muda kidogo mama yake Felix alirudi akiwa amejipaka kinyesi chake mwili mzima na kumwambia Felix, “haya naomba uniogeshe na hii ndiyo gharama yangu kwa siku moja tu katika utoto wako. Kutokana na harufu ile, Felix hakuweza hata kumsogelea Mama yake. Je, Yesu angemlipa nini Mama yake kwa mahangaiko aliyoyapata hadi chini ya msalaba alipokata roho? Yesu anamkabidhi mama yake Kanisa na kusema, “Mama tazama mwanao.” Je, watambua nafasi yako katika familia?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mwanangu, wakati wa kufanikiwa uendelee katika unyenyekevu; hivyo utapewa kuliko mwenye ukarimu,” YbS 3:17

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie amani ya kweli, upendo na tulizo kwenye familia zetu ambazo leo hazipo tayari kutaabikiana. Amina

Familia Takatifu ya Yesu, Maria, na Yosefu, Mtuombee.

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario