martes, 20 de diciembre de 2016

TAFAKARI: DECEMBA 22, WIKI YA 4 YA MAJILIO


DECEMBA 22, WIKI YA 4 YA MAJILIO

Somo: 1Sam 1:24-28

Zab: 1Sam 2:1, 4-5, 6-7, 8abcd

Injili: Lk 1: 46-56

Nukuu:

Naliomba nipewe mtoto huyu; Bwana akanipa dua yangu niliyomwomba; kwa sababu hiyo mimi nami nimempa Bwana mtoto huyu; wakati wote atakaokuwa hai amepewa Bwana. Naye akamwabudu Bwana huko,” 1Sam 1:27-28

“Mariamu akasema, Moyo wangu wamwadhimisha Bwana,” Lk 1:46

“Na roho yangu imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu,” Lk 1:47

“Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48

“Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52

TAFAKARI: “Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa.”

Wapendwa wana wa Mungu, masomo ya leo yanatualika kuyatafakari Makuu ya Mungu kwa wanyenyekevu wake wa Moyo. Taswira hii na fadhila hii ya unyenyekevu inajionyesha katika wimbo ule wa Ana na Bikira Maria. Ana ana kila sababu ya kumshukuru Mungu kwa kumrudishia heshima yake kama Mama kwa kumpatia Mtoto, Samweli. Kwa kutokuwa na mtoto alidharaulika sana na kuonekana hafai.

Hivyo inamlazimu kumrudishia Mungu sifa na shukrani kama alivyokwisha kuhaidi mbele ya Eli, Kuhani huko Shilo. “Naliomba nipewe mtoto huyu; Bwana akanipa dua yangu niliyomwomba; kwa sababu hiyo mimi nami nimempa Bwana mtoto huyu; wakati wote atakaokuwa hai amepewa Bwana. Naye akamwabudu Bwana huko,” 1Sam 1:27-28. Ndugu yangu, nawe hauna kitu cha kumshukuru Mungu kama Mama huyu Ana? Ukweli ni kwamba, ‘moyo usio na shukrani ukausha mema yote.’

Tenzi hizi zote mbili, yaani wmbo wa Ana na Bikira Maria zinatuonyesha utendaji wa Mungu katika historia ya wokovu. Kwa kuikamilisha safari hii ya wokovu, Mungu aliwachagua baadhi ya watu, na wakati mwingine wale waliodharauliwa na hata kutokujaliwa katika jamii. Watu hawa ni kama Ana mama yake Samweli aliyekuwa tasa, Elizabeti mama yake Yohane Mbatizaji, Mama Bikira, na wengine wengi tu katika historia hii ya wokovu.

Utenzi wa Bikira Maria, “Magnificat,” wenye maana ya “Wamtukuza,” unaonyesha kutukuza na kuinuliwa kwa hali ya juu roho na nafsi ya binti wa Sioni. “Moyo wangu wamwadhimisha Bwana,” Lk 1:46. Utenzi huu unaonyesha matumaini mapya na furaha mpya kwa kujibiwa kwa sala ambayo ilifanywa muda mrefu na wana wa Mungu waliokuwa wakisubiri kujibiwa kwao. “Amemsaidia Israeli, mtumishi wake; Ili kukumbuka rehema zake; Kama alivyowaambia baba zetu, Ibrahimu na uzao wake hata milele,” Lk 54-55. Machozi, furaha na matumaini ya watu yamefungwa katika  mioyo yao. Hivyo Mungu ndiye mwenye kutukuzwa kwa sababu kamjibu mjakazi wake. Huruma ya Mungu imefanywa milele ndani ya mjakazi wake. “Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48.

Kwa maana hiyo, Neno kufanyika mwili ni neno la kinabii ambalo huharibu na kutengeneza, hung’oa na kupanda, Yer 1. Yesu Kristo ndiyo hitimisho la historia, nguvu inayokamilisha ahadi za kale. “Agano langu nitalifanya imara kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako,” Mwa 17:7. Binti Sioni alitoa jina letu kwa  “Ndiyo” yake kwa Mungu, na Neno akafanyika mwili, 1Sam 2:1-10.

Wapendwa katika Kristo, unyenyekevu na kule kujishusha ni silaha kubwa sana katika maisha, kuzijua njia za Mungu, na mwisho kutumika naye kwa mambo makubwa na hata kupita uwezo wetu kama wanadamu. Unyenyekevu ni mama wa fadhila zote. Anza sasa kwa kutambua mipaka yako ikiwa ni pamoja na madhaifu yako.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu,” Mit 11:2

Tusali:- Ee Yesu Mwema, tuondelee ukuta wa kiburi na majivuno, ili tufikie makuzi yale yalio kusudi ya kuumbwa kwetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario