lunes, 1 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 18 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI  YA 18 YA MWAKA-C
Somo: Yer 30:1-2, 12-15, 18-22
Zab: 102:16-18, 19-21, 29, 22-23
Injili: Mt 14:22-36
Nukuu:
Maana Bwana asema hivi, Maumivu yako hayaponyekani, na jeraha yako ni kubwa. Hapana mtu wa kukutetea; kwa jeraha yako huna dawa ziponyazo,” Yer 30:12-13 

Wote wakupendao wamekusahau; hawakutafuti; maana nimekujeruhi kwa jeraha ya adui, kwa adhabu ya mtu mkatili; kwa sababu ya ukubwa wa uovu wako, kwa sababu dhambi zako zilikuwa zimeongezeka,” Yer 30:14 

 “Nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu,” Yer 30:22 

 “Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho,” Mt 14:24 

 “Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli; wakapiga yowe kwa hofu,” Mt 14:26 

Mara Yesu alinena, akawaambia, Jipeni moyo ni mimi; msiogope,” Mt 14:27 

 “Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka?” Mt 14:31 

TAFAKARI:Nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu wetu aliye hai anatuambia, ‘ninyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu.’ Maneno haya ya Mungu pamoja na ukuu wake, yanafafanua Mungu wetu ni wa aina gani, na zaidi yanaonyesha uhusiano wa Mungu huyu na viumbe vyake. Uhusiano wa Mungu wetu si ule wa mtumwa na mtwana, bali ni uhusiano wa Baba mwenye kujali na kuwajibika ipasavyo. Ni Mungu mwenye kujali na asiyesahau ahadi zake hata pale tunapokumbana na sintofahamu nyingi katika maisha ya kila siku. Kamwe Mungu hawezi kuisahau sura na mfano wake katika tendo zima la uumbaji wetu sisi wanadamu, Mwa 1:27.

Kwa mwonekano huu wa Mungu wetu, ni wazi Mungu wetu “ni mpole wa hasira, mwingi wa rehema, mwenye kusamehe uovu na makosa, naye hatamfanya mwenye hatia kuwa hana makosa kwa njia yo yote; mwenye kuwapatiliza wana kwa uovu wa baba zao, katika kizazi cha tatu na cha nne,” Hes 14:18. Hata hivyo, upole na wingi huu wa rehema za Mungu siyo halalisho la sisi kufanya kama tutakavyo, bali ni mwaliko wa sisi kufanana naye katika ukamilifu wake, Mt 5:48. Tunaposhindwa kuzifuata njia za Mungu, ni dhahiri tutakayo kutana  nayo mbele ya safari  yatakuwa tokeo matakwa yetu, na siyo ya Mungu. Huu ndio uovu tutesekao kama tokeo la ufahamu na utashi wetu. “Maana Bwana asema hivi, Maumivu yako hayaponyekani, na jeraha yako ni kubwa. Hapana mtu wa kukutetea; kwa jeraha yako huna dawa ziponyazo,” Yer 30:12-13. Mateso na mahangaiko ya Taifa lile teule la wana wa Israeli kwa kiasi kikubwa yalitokana na uasi wao kwa kumsahau Mungu na kuenenda kadiri ya ubinafsi na matakwa yao yasiyo na hofu ya Mungu ndani yake.

Mungu hubaki kama Mungu, na katika nafasi yake kama Mungu. Jambo la ajabu na kusikitisha ni pale mwanadamu anapojifananisha na Mungu, na kutoa maneno mazito ambayo huzidi upole na wingi wa rehema za Mungu. Mwanadamu huyu ambaye hata sekunde moja ya uhai wake haiijui, hujijengea himaya ya juu kuliko hata makerubi. Hujikuza na hata kujiona kuwa zaidi ya Mungu unapoyatazama matendo yake. Vita yoyote ile dhidi ya Mungu na watu wake mwanadamu mwenye mifupa na nyama hawezi kuishinda hata kidogo. Kuendelea kushindana na Mungu kwa mtindo huu ni dhihirisho la ufinyi wetu wa kufikiri uliojaa mbwembwe za hapa na pale kama mvua za vuli.

Na hii ndiyo maana ya kutegemea nguvu zetu na urafiki wa kibinadamu wenye kupotoshana kama asemavyo Mungu kupitia kinywa cha Nabii Yeremia,  Wote wakupendao wamekusahau; hawakutafuti; maana nimekujeruhi kwa jeraha ya adui, kwa adhabu ya mtu mkatili; kwa sababu ya ukubwa wa uovu wako, kwa sababu dhambi zako zilikuwa zimeongezeka,” Yer 30:14. Katika majivuno na hali hii ya kujihesabia haki, Mungu hubaki kama alivyo na ukuu wake si kwa ubaya, bali kwa vile umejitenga naye. Hivyo kulia kwako na lawama zako juu yake hukurudia mwenyewe hadi pale utakapoifuata njia yake na kukutana naye. Naye Mungu anakuambia, Mbona unalilia maumivu yako? Hayaponyeki maumivu yako; kwa sababu ya ukubwa wa uovu wako, kwa sababu dhambi zako zimeongezeka, nimekutenda haya,” Yer 30:15. Ponya yako katika hali na mazingira haya ni kumrudia Mungu kwa toba ya kweli na majuto.

Unapomrudia Mungu katika toba ya kweli na majuto, Mungu hurudisha ahadi zake zote, neema na baraka. Na hivi ndivyo atakavyofanya kwa wana wa Israeli. Bwana asema hivi, Tazama, nitarudisha tena hema za Yakobo zilizohamishwa, na kuyahurumia makao yake; nao mji huo utajengwa juu ya magofu yake wenyewe, nalo jumba litakaliwa, kama ilivyokuwa desturi yake,” Yer 30:18. Huyu ndiye Mungu aliye hai na mwenye kututakia mema muda wote. Naye anasema,  Tena kwao itasikiwa shukrani, na sauti yao wachangamkao; nami nitawazidisha, wala hawatakuwa wachache; tena nitawatukuza, wala hawatakuwa wanyonge,” Yer 30:19. Tukiwa na Mungu aliye hai hatuna cha kuogopa wala kufishwa. Licha ya kutupa yale tunayohitaji, Mungu utulinda dhidi ya  adui na watesi wetu.

Na katika hili Mungu anasema, Watoto wao nao watakuwa kama zamani, na kusanyiko lao litathibitika mbele zangu, nami nitawaadhibu wote wawaoneao,” Yer 30:20. Katika usalama huu na amani, Mungu humwinua mmoja katika kundi kuliongoza kundi hilo katika kweli na haki. Na mkuu wao atakuwa mtu wa kwao wenyewe, naye mwenye kuwatawala atakuwa mtu wa jamaa yao; nami nitamkaribisha, naye atanikaribia; maana ni nani aliye na moyo wa kuthubutu kunikaribia? Asema Bwana,” Yer 30:21. Ndugu yangu, ukizitazama siasa za Bara letu la Afrika na sehemu nyingine kusipokoma vita na mateso ya watu, karibia wote waliohodhi mamlaka hawakuwa na siyo matakwa ya Mungu kupitia watu wake kwa sanduku la kura. Kinachofanyika ni mchezo wa kuigiza.

Wengi hujitokeza kuchagua wampendaye na mwenye mastahili hayo kadiri ya hitaji la wakati, ila watu wachache na tena wasiozidi kumi huamua nani awe kiongozi. Hii ni dhambi kubwa sana, na ndiyo chanzo cha mateso ya watu. Ni vyema kuheshimu sauti ya Mungu kupitia watu wake walio huru na wenye utashi katika maamuzi. Naye Mungu anasema, Nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu,” Yer 30:22. Tunapokosa hofu ya Mungu katika matendo yetu, Mungu hujitenga nasi hadi pale tutakapo mtafuta. Leo badala ya kuwa na hofu ya Mungu, wengi tumekuwa na hofu isababishwayo na ubinadamu wetu, na hofu ya wachache wanaojitwalia umungu watu. 

Ndugu yangu, hofu ni kitu kibaya sana katika maisha. Ikiwa maisha ya kawaida ya mtu hujengwa katika msingi wa Imani, hofu kwa upande mwingine hubomoa msingi huu. Ukiwa na hofu huwezi kufikiri sawasawa, huwezi kupanga mipango yako sawasawa, huwezi kukua kimwili na kiroho, huwezi kuabudu vizuri. Hofu hutujengea shaka kwa kila kitu tufanyacho. Hatuwezi kumwendea Mungu katika hali ya hofu. Tukiwa na hofu ni vigumu kuelewa fumbo la Kristo katika maneno yake yale matatu: “mimi ndiye njia, kweli na uzima,” Yoh 14:6. Hivyo Yesu anapowaacha wafuasi wake wenyewe katika boti, wanaingiwa na hofu wanapomwona akitembea juu ya baharí. Wote wanadhani kuwa yeye ni kivuli. Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli; wakapiga yowe kwa hofu,” Mt 14:26. Wanafunzi wa Yesu wanashindwa kufahamu ukuu wa Kristo na mamlaka aliyokuwa nayo.  Nao walipomwona, walimsujudia; lakini baadhi yao waliona shaka. Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani,” Mt 28:17-18. Tukiwa ndani na katika Kristo hatuna sababu yoyote kuwa na mashaka juu ya utendaji wake.

Hata katika hali hii ya hofu na sintofahamu katika maisha, Kristo anatuambia kama alivyowaambia wanafunzi wake, Jipeni moyo ni mimi; msiogope,” Mt 14:27. Ila ukweli ni kwamba kwa Mkristo yule anayejitamba kuwa ni mfuasi wa Kristo, na akawa na mashaka juu ya utendaji wa Kristo katika maisha yake, huwa sikitiko kubwa kwa Yesu Kristo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wanafunzi wa Yesu. Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka?” Mt 14:31. Je, wamwamini Kristo wakati mambo yako yakikunyookea tu? Ni kweli kwamba Yesu hawezi kuongea nawe katika shida? Je, Yesu anamaanisha nini anaposema yeye ndiye NJIA? Ndugu yangu labda nikukumbushe kidogo. Njia ya kweli aliyoichagua Yesu kukukomboa kutoka utumwa wa dhambi, ni njia ile aliyoichukua, yaani, njia ya mateso. Hivyo Yesu anatuambia hata katika mateso tunawekwa huru katika kweli. Ni kwa namna hiyo hiyo kwamba hakuna Utukufu pasipo Msalaba.

Wapendwa katika Kristo, ni katika Imani ya kweli Kristo anaendelea kutuponya majeraha yetu ya mwili na roho. nao wakamsihi waguse hata pindo la vazi lake tu; na wote waliogusa wakaponywa kabisa,” Mt 14:36. Hili ni tendo la Imani. Uwe na Imani, Usiogope.

Tusifu Yesu Kristo!

“Jipeni moyo ni mimi; msiogope,” Mt 14:27


Tusali:-Ee Yesu, uliye tumaini letu, kwako kuna amani ya kweli. Litazame taifa letu katika mapito yake. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario