JUMATANO
WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 3:1-9
Zab/Kit: 33:12-13, 14-15, 20-21
Injili: Lk 4:38-44
Nukuu
“Lakini,
ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali
kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo,”
1Kor 3:1
“Mimi nilipanda,
Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu,” 1Kor 3:6
“Hivyo,
apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye,” 1Kor 3:7
“Akasimama karibu
naye, akaikemea ile homa, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia,” Lk
4:39
“Pepo nao waliwatoka
watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea,
asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo,” Lk 4:41
“Akawaambia,
Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana
kwa sababu hiyo nalitumwa,” Lk 4:43
TAFAKARI: “Hivyo,
apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye,” 1Kor 3:7
Wapendwa wana wa Mungu, uwepo wa
Kristo katika maisha yetu ni habari njema ya ufalme wa Mungu. Habari hii njema
ni wokovu na uzima wetu. Ujio wa Yesu kwetu, yaani, Neno kufanyika mwili na
kukaa kwetu, Yoh 1:14, siyo ujio wa mwivi mwenye kupora na kuondoka. Naye Yesu
anasema, “Mwivi
haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha
wawe nao tele,” Yoh 10:10. Ujio wa Kristo ni
uzima kwetu, na tena atutaka tuwe nao wa kutosha. Ukweli huu unajidihirisha
katika uponyaji wa Mama mkwe wa Petro Mtume, Lk 4:38. Yesu “akasimama karibu naye, akaikemea ile homa,
ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia,” Lk 4:39. Kama tendo la shukrani
kwa uponyaji ule, kilichofuata ni kuwajibika kama sehemu ya kuyafanya mapenzi
ya Mungu.
Kristo anatutaka pamoja na mambo yote
tuyafanyayo kila siku tusiache kamwe kuutafuta ufalme wa Mungu. Ufalme huo
umeshajidhihirisha hapa hapa duniani kwa matendo ya wokovu ya Kristo mwenyewe. “Na jua lilipokuwa
likichwa, wote waliokuwa na wagonjwa wenye maradhi mbali mbali waliwaleta
kwake, akaweka mikono yake juu ya kila mmoja akawaponya,” Lk 4:40. Alama na
ishara hizi zinaufunua Utukufu wa Mungu na Ufalme wake. “Pepo
nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelele na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu.
Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo,” Lk 4:41. Uwepo
wa Kristo unatikisa mfumo mzima wa shetani, na hiki ndicho kiama cha uovu na
kushamiri kwa wema ndani na katika Kristo. Ni kwa
sababu hiyo Kristo kaja kwetu. Tuushinde uovu kwa wema mara zote katika maisha
yetu.
Mambo
yote tuyapataya duniani hapa kwayo yenyewe siyo ukamilifu wa yale
aliyotuandalia Mungu katika ufalme wake. Ni kwa mantiki hiyo, ishara au miujiza
licha ya kuufunua Utukufu wa Mungu, kwayo kama ilivyo siyo mwisho wa kila kitu,
bali utusaidia kukua katika Imani. “Hata
kulipokucha alitoka akaenda mahali pasipokuwa na watu; makutano wakawa
wakimtafuta-tafuta, wakafika kwake, wakataka kumzuia asiondoke kwao,” Lk 4:42.
Kutaka kumzuia Yesu abaki nao ni kupenda kugaagaa katika miujiza ambayo kwayo
kama ilivyo siyo kusudi hasa la ujio wa Kristo kwetu.
Kupenda ishara na
kubaki katika ishara ni alama ya kutokukua au kukomaa katika Imani. Yesu
anawaambia wale waliokuwa wanataka kukaa naye tu, “Imenipasa kuihubiri habari
njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo
nalitumwa,” Lk 4:43. Na kauli mbiu ya Yesu
kwako na kwangu ni hii; “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia;
tubuni, na kuiamini Injili,” Mk 1:15. Wapendwa, yatupasa kuinjilishana ili kila mmoja ajue
kusudi la Yesu hapa duniani.
Kielelezo cha kazi hii ya
kuinjilishana ni Kristo mwenyewe na siyo kujiinua kwetu kuliko kwa kibinadamu.
Nafasi yako katika uinjilishaji ni kama chombo cha udongo katika kutimiza
wajibu wake kwa yale ipasayo kufanya. Hakika sote tu vyombo vya udongo kama
asemavyo Mtume Paulo, “Lakini
tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu,
wala si kutoka kwetu,” 2Kor 4:7. Hatuna cha kujisifia zaidi ya kumshukuru Mungu
kwa kututumia vyema hata katika udhaifu wetu.
“Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza
kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia
ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo,” 1Kor 3:1. Leo na hasa
tunapozungumzia uinjilishaji mpya, ni wito kwa kila mbatizwa kuifanya kazi hiyo
kuanzia pale alipo.
Leo wengi wetu hatuweki
tena mkazo katika mafundisha ya Kanisa na badala yake tumekuwa ‘vidakizi’ wa
mambo na mwisho wa siku kukosa mwelekeo thabiti wa imani. Ndugu yangu, mkate
usioiva vizuri ni hatari sana kwa tumbo. Wengi wetu leo twatambulika kama
Wakrito kwa majina yetu tu. Hili ni jangwa la Imani katika familia. Ukweli ni
kwamba, familia ndiyo shule ya kwanza kabisa tunapoweza kujifunza na kuishi
imani yetu.
Baba na Mama ndiyo
walimu wetu wa Imani. Mtume Paulo anatambua wajibu wake katika kweli hii, na
kusema, “Naliwanywesha maziwa sikuwalisha
chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa
tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa
tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?” 1Kor 3:2-3. Kumjua na kumuishi Kristo ni kuwa upande wa
mabadiliko, yaani, kutoka kwenye giza na kuingia katika mwanga.
Mabadiliko hayo na katika ngazi tofauti
tofauti yasiwe sababu ya mimi au wewe kujisifia na kujikweza. Udakuzi hapa si
nani kafanya nini au kamzidi nini mwenzake, bali sote kwa pamoja tumelifikia
lengo la kuihubiri habari njema? “Maana
hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je!
Ninyi si wanadamu?” 1Kor 3:4. Je, hayo yote tuyaonayo pamoja na tofauti zetu
katika utendaji yapo kama yalivyo kwa nguvu zetu binafsi? “Basi
Apolo ni nani? Na Paulo ni nani?” IKor 3:5a. Tofauti zetu katika utendaji ndiyo
uzuri wa Mungu. Hatukuumbwa tuwe ‘maroboti,’ bali tuwe wamoja katika tofauti
zetu. Hivyo Apolo na Paulo “ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama
Bwana alivyompa,” 1Kor 3:5b. Na ndivyo ilivyo mpendeza Mungu.
Uzuri wa umoja katika
utofauti ukuza ubunifu na utofauti wa yale ya kawaida tuyafanyayo. Katika hili
Mtume Paulo anasema, “Mimi nilipanda, Apolo
akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu,” 1Kor 3:6. Tunapozitanguliza nafsi
zetu kwa kila jambo, tunazikwamisha neema za Mungu ndani yetu. Ni sawa na kubaki
katika furaha ya kujichora kwako kusikobeba uhasili wako. Ukweli ni kwamba, “apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu
akuzaye,” 1Kor 3:7. Je, natambua nguvu hiyo ya Mungu ndani yangu na kwa
mwenzangu? Kama natambua kweli hiyo, Je, namshukuru Mungu kwa uwepo wa
mwenzangu na mafanikio yake? Ndugu yangu, “yeye
apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake
mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe,” 1Kor 3:8. Kufurahia mafanikio ya
mwenzako na kumshukuru Mungu ni ukomavu wa imani.
Wapendwa wana wa Mungu,
kamwe tusisahau ukweli huu kwamba, “sisi tu
wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu,”
1Kor 3:9. Umoja katika utofauti wetu ndiyo
uzuri wa Mungu na wenye kuufunua Utukufu wake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Imenipasa kuihubiri habari njema
ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa,”
Lk 4:43
Tusali:-Ee
Yesu, tutumie vyema kama vyombo vyako vya udongo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario