martes, 9 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 19 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 9:1-7, 10:18-22
Zab: 113:1-2, 3-4, 5-6
Injili: Mt 18:15-20
Nukuu
Waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu. Basi, wakaanza kwa wazee waliokuwa mbele ya nyumba,” Eze 9:6

 “Nao makerubi wakainua mabawa yao, wakapaa juu kutoka katika dunia machoni pangu, hapo walipotoka nje, nayo magurudumu yakawa kando yao; wakasimama mahali pa kuingilia pa mlango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Bwana; na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao,” Eze 9:19 

Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo,” Mt 18.15 

 “Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:19

TAFAKARI:Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo.”

Wapendwa wana wa Mungu, tulitazamapo Agano la kale na Agano jipya, tunaona umbali na ukaribu wa Mungu. Pamoja na mambo mengi, Agano la Kale linaonyesha Mungu aliye mbali, na mwenye kutoa adhabu za papo kwa papo licha ya kwamba upendo na huruma yake huzidi uovu na dhambi za mwanadamu. Na hivi ndivyo ghadhabu ya Mungu inavyojionyesha katika mazingira na hali ya waja wake wanapokwenda ndivyo sivyo. Naye anamwambia Nabii Ezekieli,Waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu. Basi, wakaanza kwa wazee waliokuwa mbele ya nyumba,” Eze 9:6.

 Ghadabu hizi za Mungu za dhihirisha umbali wa utukufu wake. Kisha huo utukufu wa Bwana ukatoka pale juu ya kizingiti cha nyumba, ukasimama juu ya makerubi,” Eze 9:18. Agano hili la Kale laonyesha umbali wa utendaji wa Mungu, ingawa Mungu hakuachana wala kujitenga daima na watu wake katika nyakati zote. Hili linajidhihirisha utendaji wa Mungu kupitia manabii wake mbalimbali, na hata waamuzi. Nao makerubi wakainua mabawa yao, wakapaa juu kutoka katika dunia machoni pangu, hapo walipotoka nje, nayo magurudumu yakawa kando yao; wakasimama mahali pa kuingilia pa mlango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Bwana; na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao,” Eze 9:19. Na kwa njia hii Mungu aliweza kupatana na watu wake kupitia watumishi wake waaminifu, kama manabii.

Hata hivyo Agano Jipya linaonyesha ukaribu wa Mungu. Na huyu ndiye Imanueli, Neno aliyefanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli,” Isa 7:14. Na huu ndiyo unabii uliotabiriwa na kutimia katika Agano Jipya.  “Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi,” Mt 1:22-23. Huyu ndiye mpatanishi wetu na Mungu. Kristo ndiye upatanisho wetu na Mungu Baba, naye ndiye kielelezo cha upatanisho sisi kwa sisi pale tunapokoseana.

Je, tufanye nini tunapokoseana kama ndugu? Yesu anatufundisha namna ya kufanya. Naye anasema hivi: Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo,” Mt 18:15. Ni vyema kama umekosana na ndugu yako mkayazungumza mkiwa naye na kupatana naye. Ni vyema mkayamaliza kama ndugu. Hamuitaji kuyakuza na kuwafaidia wengine kwa upungufu wenu. Kama hatakusikia na hayupo tayari kukusikiliza, Yesu anatupa nafasi ya pili. Naye anasema hivi: Na asipowasikiliza wao, liambie Kanisa; na asipolisikiliza Kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru,” Mt 18:17. Kanisa likiwa ndio mwili wa Yesu nasi tukiwa viungo vyake, ndiyo sehemu muhafaka wa kuyazungumza yale yote yaliyokwenda kinyuma na upendo wa Mungu. Je, tunatumia nafasi hii vyema kuyamaliza yale yanayotusibu? Kwa nini basi tunakimbilia mahakamani kwa mambo yetu ya familia? Je, tuupatapo ushindi huo wa kimahakama utatusaidia kuujenga tena ule undugu wenu ulioingia dosari? Ndugu yangu, tusipokuwa tayari kulisikiliza Kanisa tunahesabiwa kama watu wa mataifa.

Wapendwa wana wa Mungu, yatupasa kuyamaliza mambo yote sisi wenyewe, na pale tunaposhindwa kufanya hivyo, basi tuliachie Kanisa litusaidie kufikia muhafaka wa matatizo yetu. Hapa ndipo penye furaha ya Mungu wetu aliye hai.Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:19. Je, unataka ushindi wa kidunia au upendo wa Mungu wako aliye hai? Patana na ndugu yako kindugu, naye Mungu atakuneemesha katika haki na kweli. Na walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao,” Mt 18:20. Utulivu na amani ni uwepo wa Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:19


Tusali:-Ee Yesu uliye mpatanishi wetu na Mungu Baba, tujalie moyo wa msamaha tunapokosewa na kuwakosea wengine. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario