ALHAMISI
WIKI YA 21 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 1:1-9
Zab/Kit: 145:2-3, 4-5, 6-7
Injili: Mt 24:42-51
Nukuu
“Neema na iwe kwenu na
amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo,” 1Kor 1:3
“Namshukuru
Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika
Kristo Yesu,” 1Kor 1:4
“Mungu ni mwaminifu
ambaye mliitwa na yeye mwingie katika ushirika wa Mwanawe, Yesu Kristo Bwana
wetu,” 1Kor 1:9
“Kesheni
basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42
“Lakini
fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja,
angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa,” Mt 24:34
TAFAKARI: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi
atakayokuja Bwana wenu.”
Wapendwa wana wa Mungu, leo tutafakari kuhusu
maisha ni jukumu la muda mfupi. Na ndiyo dhima ya Injili ya leo kwa maneno haya
ya Yesu, “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni
siku ipi atakayokuja Bwana wenu,” Mt 24:42. Ndugu unayesafiri nami katika
tafakari hii, ni ukweli usiofichika kwamba maisha duniani ni jukumu la muda
mfupi. Je, unabisha? Maandiko Matakatifu hufundisha na kutukumbusha maisha yetu
duniani yalivyo mafupi na yasiyodumu. Maisha yanaelezwa kama ukungu, mkimbiaji,
pumzi, na mvuke. "Kwani sisi tu wa
jana tu, wala hatujui neno, kwa kuwa siku zetu duniani ni kivuli tu." Ayu
8:9
Ndugu, ili kutimiza
vizuri maisha yako hupaswi kusahau ukweli wa aina mbili: Kwanza,
yakilinganishwa na umilele, maisha ni mafupi sana. Pili, dunia ni makazi ya
muda tu. Hatuwezi kukaa hapa kwa muda mrefu, hivyo usijishikamanishe sana nayo. “Fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba
angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba
yake kuvunjwa,” Mt 24:34. Tumwombe
Mungu atusaidie kuyaona maisha ya duniani kama anavyoyaona yeye mwenyewe.
Mfalme Daudi aliomba, "Bwana, nijulishe mwisho wangu, na kiasi cha siku
zangu ni kiasi gani; nijue jinsi nilivyo dhaifu," Zab 39:4
Ndugu yangu hapana shaka wa mfahamu
vizuri "inzi!" Mdudu huyu kadiri ya utafiki wa kisayansi huishi siku
saba tu. Ni wiki moja kati ya wiki 52 katika mwaka mmoja. Tazama fujo na papara
za inzi. Hutua kila mahali kwa siku hizo saba; kwenye vyakula (vilivyo chacha
na visivyo chacha), kwenye vinjwaji, kwenye vidonda, kwenye vinyesi, nk. Tazama
anavyoongea kwa ishara akiwa amenyanyua miguu yake ya nyuma na kusema,
"yaliyopita yeshapita." Na anapoinua miguu ya mbele husema hivi,
"yajayo na yaje, ponda mali, furahia yote, haya ndiyo maisha."
Ndugu yangu, tulio
wengi leo maisha yetu hayana tofauti na haya ya inzi. Hutaka kufanya yote na
kujaribu yote katika maisha. Hakuna muda wa maandalizi wala tafakari kuhusu
umilele wetu kama zawadi ya pekee tuliyopewa sisi wanadamu. Katika kweli hii
Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Kwa
sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana
wa Adamu yuaja,” Mt 24:44
Ona! tunavyoishi na
jirani zetu! Unaweka wigo "fence" kiasi kwamba unamzuiya hata jirani
yako kufungua mlango. Ona! tusivyo wajali wengine afya zao! Tunaelekeza maji
taka kwenye makazi yao bila huruma. Eti kwa vile unapesa, na unajulikana hadi
usalama wa Taifa. Eti kwa vile wewe ni kiongozi wa ngazi za juu kwenye utawala
dhalimu. Eti kwa vile wewe ni mfanya biashara maarufu nchini. Je, hili ndilo
kusudio la Mungu kwa maisha yako hapa duniani? Yesu anatutaka kila mmoja wetu
tutafakari swali hili; “Ni nani basi yule
mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake,
awape watu chakula kwa wakati wake?” Mt 24:45. “Ambaye Bwana wake alimweka juu
ya nyumba yake,” kwa maanisha utumiaji mzuri wa mali, karama na vipaji
ulivyojaliwa na Mungu. Huku ni sawa na kuwa ‘mtumwa mwaminifu.’ Naye Yesu anasadifu utumwa huu na kusema, “Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo
atamkuta akifanya hivyo,” Mt 24:46. Mwenye kuwekeza vizuri katika haya atawekwa
juu kabisa machoni mwa Mungu. “Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake
vyote,” Mt 24:47
Ndugu yangu, usisahau kuwa maisha ya
hapa duniani ni sawa na kuwa ugenini. Haya si makazi yako ya kudumu, au hatma
yako ya mwisho. Unapita tu! Unatembea tu duniani. Mfalme Daudi anatukumbusha,
"Mimi ni mgeni katika nchi, usinifiche maagizo yako," Zab 119:19, na
Mtume Petro anasema, "na ikiwa
mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi
yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni."
1Pet 1:17. Waamini wa kweli wanafahamu wazi kwamba kuna mambo mengi ya maisha
kuliko hii miaka michache tunayoishi hapa duniani.
Ndugu yangu, kitambulisho chako kiko
katika umilele, na nchi yako ni mbinguni. Unapofahamu ukweli huu, utaacha kuwa
na wasiwasi wa "kupata kila kitu" hapa duniani. Mungu yupo wazi kabisa
kuhusu habari za kuishi kwa ajili ya "hapa" na "sasa" tu
huku ukijifananisha na watu wa dunia hii katika kipaumbele na mtindo wa maisha.
Tunapochezacheza na
majaribu ya dunia hii, Mungu anaita hali hiyo uzinzi wa kiroho. "Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa
rafiki ya dunia ni kuwa adui wa Mungu?" Yak 4:4. Karipio hili kwa maana
nyingine la tuambia kwamba 'twajidanganya mbele za Mungu iwapo tunachotaka ni
mambo yetu, kuchezacheza na ulimwengu kwa kila nafasi tunayopata mwisho wetu ni
kuwa maadui wa Mungu na njia yake.' Rejea mfano wa inzi hapo juu. Tukichukua
mfano wa mtumwa wa Injili ya leo, Yesu anamfananisha na Mtumwa mbaya, yaani
asiye tumia vyema mali, karama na vitaji vyake. Ni mtumwa yule asemaye moyoni
mwake ‘kula maisha kifa chaja.’ Ni “mtumwa
yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula
na kunywa pamoja na walevi; bwana
wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani, na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea
fungu lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno,” Mt
24:48-51
Mimi na wewe "tu
wajumbe kwa ajili ya Kristo..." 2Kor 5:20. Cha kusikitisha, wakristo wengi
tumemsaliti mfalme wetu na ufalme wake. Katika hali ya upumbavu tumeamua kwamba
kwa sababu tunaisha hapa duniani, basi hapa ndiko nyumbani kwetu.
"Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili
zipinganazo na roho." 1Pet 2:11. Tunasahau ukweli huu kwamba, hata tukiwa
katika kila jambo tulitajirika katika Yeye Yesu Kristo, 1Kor 1:5. Kristo ndiye
anayethibitika kwetu tunapomwamini, 1Kor 1:6. Na katika Kristo Yesu
hatupungukiwi kitu na hatutapungukiwa kitu,1Kor 1:7. Mungu hubaki kuwa
mwaminifu ambaye tumeitwa na Yeye tuingie katika ushirika na Mwanaye, Yesu
Kristo Bwana wetu na Mwokozi wetu, 1Kor 1:9.
Mungu pia anatuonya tusijishikamanishe
sana na vitu vinavyotuzunguka kwa kuwa si vya kudumu. "Na wale wautumiao
ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu
yanapita." 1Kor 7:31. Ni wazi yatupasa kufanya kazi na kujipatia mahitaji
yetu ya kila siku. Ila yote hayo tuyapatayo hatupaswa hata mara moja
kujilinganisha nayo. Utu wetu na watu wengine ni zaidi ya mali hizo. “Nanyi
mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu;
mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa
damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya
Kristo,” 1Pet 1:18-19. Ndugu yangu, ni ukweli usiotia shaka kwamba kwa mivuto
ya hali ya juu, na vyombo vya mawasiliano vyenye kutia upofu, na mambo mengi ya
anasa yaliyopo siku hizi, ni rahisi kusahau kwamba maisha si kufanya raha tu.
Ndugu sikuonei gere bali nakukumbusha tu!
Ni pale tu tunapokumbuka kuwa maisha ni
jukumu la muda mfupi ndipo mvuto wa mambo ya anasa utakapokosa nguvu maishani
mwetu. Hili likifikiwa twaweza kujiandaa kwa jambo jingine ambalo ni bora
zaidi. "Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni
vya milele. "2Kor 4:18b. Ukweli kwamba dunia si makazi yetu ya kudumu
huelezea kwa nini, kama wafuasi wa Kristo, tunapatwa na magumu, huzuni, na
kukataliwa (Yoh 15: 18-19; 16:20; 16:33). Ukweli huu pia hueleza kwa nini
baadhi ya ahadi za Mungu huonekana kutotimizwa, baadhi ya sala hazijajibiwa, na
baadhi ya mazingira kuonekana kutokuwa na haki. Huu si mwisho wa mambo.
Ili kutufanya tusijifungamanishe na
ulimwengu sana, Mungu huruhusu tusikie hali fulani ya kutokuridhisha na
kutosheka katika maisha-hitaji ambalo "haliwezi" kutoshelezwa kamwe
hapa duniani. Hatuna furaha kabisa hapa kwa sababu hatutakiwi! Dunia si makazi
yetu ya milele, tumeumbwa kwa ajili ya kitu bora zaidi. Ndugu yangu, samaki
hawezi kuwa na furaha kuishi nchi kavu, kwa sababu ameumbwa kwa ajili ya kuishi
majini. Tai kadhalika asingefurahi kama asingeruhusiwa kupaa angani. Hatuwezi
kamwe kujisikia kutosheka kabisa hapa duniani, kwa sababu tumeumbwa kwa mambo
mengine zaidi. Utakuwa na vipindi vya furaha hapa, lakini hakuna cha kufanana
na kile Mungu amepanga kwa ajili yako.
Kwa kutambua kwamba maisha ni jukumu la
muda mfupi tu ni lazima kubadili kabisa mambo unayoyaona ya muhimu maishani
mwako. Mambo ya milele, yasiyo ya muda mfupi, yapasa yawe vigezo vya maamuzi
yako. Kama C. S. Lewis anavyosema, "Kila kisicho cha milele hakifai
milele."Tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana
vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele," 2Kor
4:18.
Ndugu, ni kosa kubwa
kudhani kuwa mpango wa Mungu kwa ajili ya maisha yako ni mafanikio ya mali au
mafanikio ya siku hizi, katika ulimwengu unavyoyaona. Maisha tele hayana uhusiano
na mali tele, na uaminifu kwa Mungu hautuhakikishii kuwa na mafanikio ya kazi
au huduma, usitazamie taji zisizodumu (1Pet 2:11). Pia, "usiogope mtu
atakapopata utajiri, na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa
hatachukua chochote; utukufu wake hautashuka ukimfuata," Zab 49:16-17.
Paulo “aliyeitwa
kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu,” 1Kor 1:1, baada ya kuongoka
kwake alikuwa mwaminifu lakini alijikuta gerezani. Yohane Mbatizaji alikuwa
mwaminifu lakini alikatwa kichwa. Mamilioni ya watu waaminifu wameuawa,
wamepoteza kila walichokuwa nacho, au maisha yao yamekoma wakiwa hawana kitu.
Lakini mwisho wa maisha haya si mwisho, bali mwanzo wa maisha mapya ya umilele.
Ndugu niliyesafiri nawe
katika tafakari hii, naomba nisikuchoshe.
Katika macho ya Mungu, mashujaa wa imani sio wale waliopata mali, wenye
mafanikio na nguvu katika maisha haya, bali ni wale wanaoyaona maisha kama
jukumu la muda mfupi na kutumia uaminifu, wakitumaini kupokea thawabu yao
katika umilele. "Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi,
bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni,
na wasafiri juu ya nchi. Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya
mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao, maana amewatengenezea
mji," Ebr 11:13, 16. Asante kwa kusafiri nami. Tafakari na chukua hatua.
Na mara zote tujitazamapo katika hali zote kama yalivyo majira ya mwaka na
tusema kama Mtume Paulo, “Namshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu,
kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika Kristo Yesu,” 1Kor 1:4.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mungu
ni mwaminifu ambaye mliitwa na yeye mwingie katika ushirika wa Mwanawe, Yesu
Kristo Bwana wetu,” 1Kor 1:9
Tusali:
Neema na iwe kwetu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu
Kristo. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario