JUMAPILI YA 19 YA MWAKA-C
Somo
I: Hek 18:6-9
Zab: 33:1, 12, 18-19, 20-22 (K) 12
Somo
II: Ebr 11:1-2, 8-19
Injili:
Lk 12:32-48
Nukuu:
“kwa hiyo watu wako
waliutazamia wokovu wa wenye haki na uharibifu wa adui. Madhali uliwalipia
kisasi watesi wale, na kwa njia ileile ulitutukuza ukituita ili tukujie,” Hek
18:7-8
“watoto watakatifu wa
watu wema walitoa dhabihu kwa siri, na kwa moyo mmoja walijitwalia agano la
torati ya dini, ya kwamba watashirikiana katika mambo mema na vilevile katika
hatari,” Hek 18:9abc
"Basi
imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo
yasiyoonekana,” Ebr 11:1
“Hawa wote wakafa
katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na
kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi,” Ebr
11:13
“Msiogope, enyi
kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme,” Lk 12:32
“Lakini fahamuni
neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha,
wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa,” Lk 12:39
TAFAKARI:
“Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo
yasiyoonekana. Na kwa njia ileile ulitutukuza ukituita ili tukujie. Hivyo, viuno
vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 19 ya mwaka “C,” wa Kanisa. Leo Mama Kanisa
kwa njia ya pekee anatualika kutafakari mambo makuu matatu; kwanza, ‘imani
katika maisha na sintofahamu zake tukilenga lile tumaini la kweli, yaani, uwepo
wa Mungu.’ Jambo la pili, ‘upi mwelekeo sahihi wa kukua katika imani kulielekea
lile tumaina la kweli.’ Na tatu, ‘ni mastahili yapi yatuwezeshayo kudumu katika
imani ya kweli tukilielekea tumaini lile la kweli, yaani, maisha baada ya kifo-maisha ya umilele.’ Haya
mawazo makuu matatu ambayo ndiyo kiini na mapaswa yetu kama Wakristo na wafuasi
wa Kristo, ndiyo yaliyobeba masomo yetu ya leo tuliyokwisha yasikia.
Wazo kuu la kwanza,
yaani, ‘imani katika maisha na sintofahamu zake tukilenga lile tumaini la
kweli, yaani, uwepo wa Mungu, tunalipata kutoka somo letu la pili la leo,
yaani, waraka ule kwa Waebrania kama tulivyosikia. Maisha kama zawadi ya Mungu
kwetu na mali yake, yana changamoto zake. Maisha ni changamoto kwa sababu
yanatuwajibisha kuishi kadiri ya kile tulichoitiwa na ndani ya hicho kitu,
yaani, wito huo, ndipo penya ule utakatifu ambalo ndilo tumaini lako mara baada
ya maisha ya hapa duniani. Maisha ni changamoto katika maana ya kwamba, tupo
hapa duniani kwa muda mfupi tu. Hivyo, maisha yamaanisha ‘kuzaliwa, kustawi, na
mwisho wa siku kunyauka.’
Hivyo kama nataka
kulifikia tumaini lile, yaani, uzima wa milele, yanipasa kuishi kadiri ya
mapenzi ya Mungu, na wakati huo huo kujiandaa vyema kwa sababu siijui siku wala
saa ya kutwaliwa kwangu katika ulimwengu huu. Na Yesu katika hili anasema, “Lakini fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba
angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake
kuvunjwa,” Lk 12:39. Kumbe huu ndio wito wa kuishi kadiri ya mapenzi ya Mungu,
na ndiyo maana halisi ya kukesha. Kukesha tu haitoshi kama sintojiandaa vyema
kwa sababu siri ile ya siku ya mwisho imefichwa kwangu. Hivyo Yesu anasema, “Nanyi
jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu,” Lk 12:40
Hata hivyo kuzikabili sintofahamu za
maisha kadiri ya wito wangu, na wakati huo huo kukabiliana nazo, yanipasa kuwa
na uelewa sahihi wa imani ya kweli. Somo hili la pili la tuelezea
"imani ni kuwa na hakika ya mambo
yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1. Kuwa na hakika ya
mambo yatarajiwayo ni ‘kutokuwa na shaka yoyote ilhali ukiwa umeyakabidhi yote
mikono mwa Mungu katika maana ya ufahamu wa kweli wa kile ukiaminicho, na
wakati huo huo umaana wake (rationality and significativity).’ Imani tu bila
kubeba ufahamu wake na umaana wake ni kishawishi kikubwa cha kuanguka kwenye
ujinga na upumbavu. Ni kwa mantiki hii ‘imani siyo ushuhuda tu uliobebwa katika
miujiza na alama nyingine kama hizo.’ Imani ni zaidi ya hayo licha kwamba kama
yapo katika kweli uimarisha imani changa. Imani ni zaidi ya ishara tuzionazo
kwa sababu, Imani “ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” Ebr 11:1b.
Maisha huwa na maana
kwa kila changamoto tunayokutana nayo kwa sababu maisha hayo yamepewa maana kwa
imani ile ya kweli ibebayo maisha yako kama nilivyokwisha sema kuhusu imani.
Muono huu wa imani ndiyo utupao tumaini hata pale tunapozungukwa na changamoto
katika maisha na sintofahamu zake. Ni ndani ya maisha haya yenye maana “Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke
aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako,” Ebr 11:8.
Ibrahimu hakushikamana na mali na mazingira yake aliyoyazoea kwa sababu aliona
maisha mengine kwa imani na tumaini la kweli hata kama hayakuwa yamefunuliwa
wazi kwake kwa wakati ule. Ni mara ngapi kwa kukosa maana ya maisha na imani ya
kweli twafa kwa shinikizo la damu tunapoamuriwa kuhama vituo vyetu vya kazi
tulivyovizoea? Ibrahimu ni tofauti kabisa kwa sababu, “Kwa
imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake,
akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile
ile,” Ebr 11:9. Kumbe kitu cha maana katika maisha yetu si pale tulipo, bali
maisha ya pale tulipo. Mtu wa kuyaboresha yawe mazuri zaidi na sehemu nzuri
zaidi ya kuishi ni wewe mwenyewe kwa sababu hu kiumbe shirikishwa cha Mungu
katika uumbaji wa pili. Maisha yasiyo na maana hata kama utakuwa huru, ni sawa
na kuishi gereza lisilokuwa na kikomo.
Ni katika ufahamu huu
na umaana wake katika maisha yabebwayo na imani ya kweli na tumaini la kweli, “Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba;
alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa
mwaminifu,” Ebr 11:11. Tukumbuke kuwa Sara alibeba mimba akiwa na umri wa miaka
90, na Ibrahimu akiwa na miaka 100, Mwa 17:17, kitu ambacho kwa hali ya kawaida
ni vigumu kutokea, ila kwa Mungu vyote vyawezekana tunapojisalimisha kwake. Hata
pale Mungu alipoyafanya yale yasiyowezekana, yaani, kuipatia familia hii
mtoto-Isaka, Ibrahimu hakukosa utii mbele ya Mungu kwa sababu imani yake
ilimfanya ayaweke matumaini yake yote kwa Mungu. Hivyo, “Kwa
imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea
hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee,” Ebr 11:17. Kwa uhakika
Ibrahimu anatambua kwamba, “Nchi
na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, Dunia na wote wakaao ndani yake,” Zab
24:1. Ibrahimu hapati maana ya maisha yake kwa utajiri aliokuwa nao, bali
tumaini lile alilokuwa nalo kwa Mungu mwenye milki zote na kila kitu kwake.
Kujisalimisha kwa Mungu
katika ufahamu na umaana wake ndiyo maisha yenyewe kuelekea lile tumaini la
kweli, yaani, maisha ya umilele. Ni katika kujisalimisha huku na katika maana
hiyo, “Hawa wote (Ibrahimu na Sara) wakafa
katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na
kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi,” Ebr
11:13. Ndugu yangu, “Mungu ndiye aliyeiumba
dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili
ikaliwe na watu,” Isa 45:18, na mwisho wa siku wale wote walio yasalimisha
maisha yao kwake pasipo shaka, kwa ufahamu na umaana wake, “waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni.
Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji,” Ebr
11:16. Ugoto wa maisha yetu hapa duniani ni mwanzo wa maisha ya milele mbinguni
kwa sababu tumeumbwa ili tuishi milele.
Wapendwa wana wa Mungu,
wazo kuu la pili, yaani, ‘upi mwelekeo sahihi wa kukua katika imani kulielekea
lile tumaina la kweli.’ Ndugu yangu, mwelekeo sahihi katika maisha ya kiroho ni
kuitafuta sura ya Mungu. Kama uhai unaye Mungu, ni wazi Mungu ndiye sababu ya
kila kitu katika maisha yetu. Huyu ndiye yatupasa kumtafuta kila siku ya maisha
yetu kwa sababu anajua jana yetu, leo yetu, na kesho yetu. “kwa hiyo watu wako
waliutazamia wokovu wa wenye haki na uharibifu wa adui. Madhali uliwalipia
kisasi watesi wale, na kwa njia ileile ulitutukuza ukituita ili tukujie,” Hek
18:7-8. Ndugu yangu hakuna maana yoyote ya kufahamu haya ya leo na kesho bila
ya kufahamu yule ayaratibishaye hayo ya leo na kesho. Huyu ndiye Mungu,
Mtakatifu, na mwenye Utakatifu na katika yeye sote tu watoto watakatifu kwa
mastahili yake na siyo yetu. Na ndani na katika Yeye ndiye mwenye kustahili
yote yatuhusuyo leo na kesho tusiyoijua. Na ndivyo ilivyo kwamba, “watoto
watakatifu wa watu wema walitoa dhabihu kwa siri, na kwa moyo mmoja walijitwalia
agano la torati ya dini, ya kwamba watashirikiana katika mambo mema na vilevile
katika hatari,” Hek 18:9abc. Mungu aliye alfa na omega, ndiye sababu ya kila
kitu katika maisha yetu.
Wapendwa wana wa Mungu,
jambo la tatu leo katika tafakari yetu ni juu ya ‘ni mastahili yapi
yatuwezeshayo kudumu katika imani ya kweli tukilielekea tumaini lile la kweli, yaani,
maisha baada ya kifo-maisha ya umilele.’ Stahili la jambo lolote lile huakisi uhasili
wa kitu hicho. Ni swala la vitendo zaidi kuliko nadharia. Na moja ya kuwa huru
ili kutumika vizuri kadiri ya matakwa ya Mungu ni kuipokea kweli hii kwamba, “Viuzeni mlivyo navyo, mtoe sadaka. Jifanyieni
mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia
mwivi, wala nondo haharibu,” Lk 12:33. Sababu na maana ya maisha yetu haipo kwa
yale tuyamilikiyo, bali katika tumaini la kweli la kile tukitegemeacho kwa
sababu yapo maisha baada ya haya. Angalizo ni hili; “Kwa
kuwa hazina yenu ilipo, ndipo itakapokuwapo na mioyo yenu,” Lk 12:34. Je,
furaha yangu ipo katika utajiri nilio nao wa leo na kesho, au kwa tumaini lile
la milele?
Ni vyema wewe na mimi
kuelewa vyema chanzo cha uhai wetu. Kumbe ni jambo la busara kabla ya yote
kujua uwezo wako binafsi dhidi ya vita
vile uvipiganavyo, na kusimama kwa yale yote yakutiayo nguvu. Ni katika kweli
na mazingira haya Yesu anakwambia wewe na mimi leo kwamba, “Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe
zinawaka,” Lk 12:35. Ufahamu wa kitu ujengwa katika kujua asili ya kile kitu
utakacho kukijua. Hivyo viuno vyetu vyapaswa kuwa vimefungwa kwa maanisha
kutumia vyema milango yetu ya ufahamu, yaani, kusikia, kunusa, kuonja, kugusa,
na kuona. ‘Na taa yetu iwe inawaka,’ kwa maanisha uhai wa dhamira ile iliyoko
ndani yako yenye kuona kweli kama ilivyo na sivyo kama ulivyo. Ni katika
mantika hiyo twaweza kuelewa maana ya maneno haya, kwamba, “nanyi
iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili
atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara,” Lk 12:36. Bila dhamiri hii njema
ndani yangu, hakuna sababu ya kukesha kwa kile nisichokijua. Hapa ndipo penye
ile heri ya mtumwa na kwenye uhai wa
dhamiri hii ndani yake. Hakika, “Heri
watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha. Amin, nawaambieni,
atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia,” Lk 12:37. Kuna
maana kubwa kukesha kwa kile ujuacho na chenye kubeba maana ya maisha yako.
Bila dhamiri hai na
njema ni vigumu kuijua siri ya Mungu ndani ya maisha yako na moyo wako. Na
kukesha hakuna maana yoyote bila kujua sababu ya kufanya hivyo na maana yake
hasa tukilitazama tumaini lile, yaani, uzima ule wa milele. Kuififisha dhamiri
hii, na hasa kwa dhambi ni kuua uzima ndani yako. “Lakini
fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi,
angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa,” Lk 12:39. Usalama wako na
wangu wa kuishi katika kweli hii na sintofahamu hii katika maisha ni kuwa
tayari kwa kila kitu katika maana ya kuishi mapenzi ya Mungu. “Nanyi
jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu,” Lk 12:40.
Ni katika kuwa tayari kwa kweli hii, Yesu anatuhoji na kututaka kufikiri zaidi
ya yale tuyaonayo kwa macho yetu, kwamba, “Ni nani, basi, aliye wakili mwaminifu, mwenye
busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya utumishi wake wote, awape watu posho
kwa wakati wake?” Lk 12:42. Kuwa wakili wa kitu chochote kile, na ili
kukabiliana na changamoto zake lazima kuwa na ufahamu wa kile ulicho kama
wakili.
Hata hivyo Yesu anatupa
angalizo, hasa pale tunapochukulia mambo kutokana na mazoea. Naye anasema, “Lakini,
mtumwa yule akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia kuja, akaanza kuwapiga
wajoli wake, wanaume kwa wanawake, akila na kunywa na kulewa; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku
asiyodhani na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake
pamoja na wasioamini,” Lk 12:45-46. Hapa ndipo pale penye kulia na kusaga meno,
na kama hauna meno, ndugu yangu hakika jiandae kusaga fizi. Usicheke! Kuna
kulia na kusaga meno kwa sababu Mungu aliye kweli, haki, huruma, msamaha, na
upendo, siye Mungu mwenye kuificha kweli yake, na hasa pale tunapokuwa tayari
kujifunua kwake. Ni kwa mantiki hiyo kwamba, “Na mtumwa yule aliyejua mapenzi ya bwana wake,
asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana,” Lk 12:47. Hiki ni kipigo cha kujichagulia kwa sababu kwa
hiari yako hukupenda kuenenda njia ile ya haki na kweli. Kinyume chake ni
kwamba, “yule asiyejua, naye
amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake
huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka
na zaidi,” Lk 12:48. Ndugu yangu, uwapo mwaminifu kwa yale ya kawaida na madogo
madogo, ni mizania hiyo hiyo itakayo kusogeza kwa yale makubwa na wakati
mwingine hubaki kama fumbo katika maisha yako. Mungu asemapo “ndiyo,” hakuna
mamlaka yoyote chini ya jua yenye uwezo wa kusema “hapana.”
Andrea cha Usiku, mkazi
wa mwenda pole, na mtoa habari wa Tarafa ya Jumuikeni, alikuwa na ujumbe wa
dharura katika kijiji cha Mwenge Mshindo. Hivyo ilimpasa kufikisha ujumbe huo jioni
ile ingawa ilimlazimu kusafiri usiku ambao kwa mazingira yale haikuwa salama
kutokana na mazingira hatarishi ya wanyama pori.
Andrea cha Usiku
alianza safari ile kuelekea kijiji kile cha Mwenge Mshindo majira ya saa kumi
na mbili ya jioni. Baada ya kusafiri kwa takribani masaa mawili, kwa mbali
alisikia sauti ya Simba. Kadiri ya uzoefu, wataalamu wanasema unaposikia sauti
ya simba kwa mbali ujue kwamba simba huyo yupo karibu, na kinyume chake ni kwamba
simba huyo yupo mbali. Hivyo kwa ufahamu huu, Andrea cha usiku ilimpasa
kutafuta mti mrefu wa karibu na ulio mwepesi kukwea ili kujiepusha na simba
yule aliye kuwa karibu.
Baada ya kuukweya mti
ule, alisikia mtikisiko wa nyasi, na mara simba yule aliyeonekana kushiba
alijilaza chini ya mti ule. Hadi jua linachomoza kesho yake, simba yule hakuonekana
kutoka chini ya mti ule, zaidi ya kupiga miayo na kutanua kucha zake kwa
kujinyoosha na kuonyesha umahiri wake. Hapa ndipo Andrea alipoanza kusali na
kuomba Mungu amwondoe simba yule mahali pale.
Ndani ya moyo wake aliisikia
sauti ikisema, “achia tawi hilo uliloshika nawe utakuwa salama.” Baada ya sauti
hii kujirudia zaidi ya mara tatu, Andrea alianza kupingana na sauti ile na kusema,
“hivi wewe wanifanya mimi ni mjinga wa mchana kweupeee kukubali kujiachi na
kutua kwenye meno haya ya simba huyu na kucha hizi na kuwa kifungua kinywa
chake?” Na baada ya robo saa, alisikia tena sauti ile ndani ya moyo wake
ikisema, “usalama wako upo pale tu utakapo jiachia.” Kwa vile hakuweza kulala
usiku kucha kwa hofu ya simba yule, aliingiwa na usingizi wa hapa na pale. Hali
hii ilimpelekea kushtuka shtuka. Na ndipo bila kujijua alijiachia na kutua
tumboni mwa simba yule kwa ghafla!
Kwa hofu ile, simba
alikurupuka na kukimbia alipokujua kusalimisha maisha yake, naye Andrea cha
usiku alitimka vikwake bila tone la usingizi. Na hivi ndivyo ilivyokuwa salama
na pona yake Andrea. Je, wamwamini Mungu?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kwa
kuwa hazina yenu ilipo, ndipo itakapokuwapo na mioyo yenu,” Lk 12:34
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie imani ya kweli. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario