jueves, 4 de agosto de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 18 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI  YA 18 YA MWAKA-C
Somo: Nah 1:15; 2:2; 3:1-3, 6-7
Zab/Kit: Kumb 32:35cd-36ab, 39abcd, 41
Injili: Mt 16:24-28
Nukuu:
“Zishike sikukuu zako, Ee Yuda, uziondoe nadhiri zako; kwa maana yule asiyefaa kitu hatapita kati yako tena kamwe; amekwisha kukatiliwa mbali,” Nah 1:15

 Ole wake mji wa damu! Umejaa mambo ya uongo na unyang'anyi; mateka hayaondoki,” Nah 3:1 

 “Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate,” Mt 16:24 

Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona,” Mt 16:25 

Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” Mt 16:26 

TAFAKARI:Salama yetu ipo katika unyofu wetu. Na mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate.”

Wapendwa wana wa Mungu, penye utaratibu wowote ule ipo akili. Na kinyume chake ni kweli. Maisha adilifu ni maisha yenye utaratibu na yenye kuona si leo na kesho tu, bali mbali zaidi, kule tukutamanipo ingawa hatupajui sawa sawa. Na maisha adilifu huongozwa na dhamiri unyofu. Na hizi ndizo nadhiri Mungu anazo wakumbusha wana wa Israeli. Na sasa “zishike sikukuu zako, Ee Yuda, uziondoe nadhiri zako; kwa maana yule asiyefaa kitu hatapita kati yako tena kamwe; amekwisha kukatiliwa mbali,” Nah 1:15. Maisha bila utaratibu hupoteza lengo lake, na mwisho wa siku dhana ya kuwajibika upotea. Huu ukiwa ndiyo mfumo wa maisha, fahari ya maisha hupotea pia. Kuona fahari ya maisha ni kuishi kwa utaratibu na unyofu. Kwa maana Bwana anairudisha fahari ya Yakobo, kama fahari ya Israeli; maana watekao nyara wamewateka, na kuyaharibu matawi ya mizabibu yao,” Nah 2:2. Utulivu wa maisha utegemea sana kweli na haki katika jamii husika.

Kweli na haki inapokosekana au kutolewa kwa ubaguzi, jamii husika kamwe haiwezi kubaki salama. Na hili ndilo onyo la Mungu kwetu: Ole wake mji wa damu! Umejaa mambo ya uongo na unyang'anyi; mateka hayaondoki,” Nah 3:1. Katika hali na mazingira haya, mateso na shida za watu huwa kilio kisicho koma. Manung’uniko na vitendo vya ukiukwaji wa haki za kibinadamu huonekana kuwa jambo la kawaida. Na hii ndiyo hali, kwamba,  Kelele za mjeledi, kelele za magurudumu yafanyayo kishindo; na farasi wenye kupara-para, na magari ya vita yenye kuruka-ruka; mpanda farasi akipanda, na upanga ukimeta-meta, na mkuki ukimemetuka; na wingi wa waliouawa, na chungu kubwa ya mizoga; mizoga haina mwisho; wanajikwaa juu ya mizoga yao,” Nah 3:2-3. Je, hili ndilo lengo la maisha?

Katika mazingira hayo Mungu anasema, Nami nitatupa uchafu uchukizao juu yako, kukufanya uwe mchafu, nami nitakufanya kuwa kitu cha kutazamwa kwa dharau,” Nah 3:6. Je, Mungu atakapotuchoka tutakimbilia wapi? Kwa nini unapenda kuwa sababu ya mateso kwa wengine? Kwa nini hutaki kukaa kwenye kiti, na badala yake wapenda kukaa vichwani mwa watu kwa mabaya tu? Kama haya yalitoke Ninawi itashindikanaje kutokea kwetu leo? Hata itakuwa, wote wakutazamao watakukimbia, wakisema, Ninawi umeharibika; ni nani atakayeuhurumia? Nikutafutie wapi wafariji?” Nah 3:7. Haya ni masikitiko makubwa sana kwa Mungu muumba wetu. Kupoteza dira ya maisha na malengo yake ni hasara kubwa sana kwa maendeleo ya mwili na roho. 

Katika agano jipya la Mungu na watu wake, chini ya mwanaye mpenzi Yesu Kristo, ili kuurithi uzima huu wa milele, kila mmoja wetu yampasa kuishi njia hii ya uzima wa kweli kama Mwanaye Yesu Kristo anavyotuwasa katika injili ya leo: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate,” Mt 16:24. Tunamfuata Yesu kwa sababu ‘Yeye ndiye njia, kweli na uzima,’ Yoh 14:6. Katika ufuasi wetu kwa Kristo, haya mambo matatu ni muhumu sana: KUJIKANA NAFSI, KUJITWIKA MSALABA, NA KUMFUATA YESU. Kujikana nafsi ni tendo la kujisalimisha na kuwa tayari kufanya kadiri ya mapenzi yake Mungu, na siyo tutakavyo sisi au tuonavyo. Ni tendo la kusalimisha utashi wako kwa Mungu, na kuwa tayari kutumika kadiri ya mpango wa Mungu. Unafanya tendo hili na kuwa sehemu ya maisha yako kwa kuyachuchumilia yale ya umilele ukilinganisha na haya ya leo na sasa tu. Ni kuishi ulimwenguni pasipo kubebwa na malimwengu. Ni kuishi maisha yanayoongozwa na malengo.

Kujitwika msalaba ni kukubali kuwa hapana utukufu pasipo msalaba. Maisha tunayoyaishi kila mmoja kadiri ya wito wake, si maisha rahisi. Kuna wakati katika maisha hayo itakupasa kutoa sadaka kubwa ili kuufia umilele ule aliotuandalia Mungu. Hivyo kujitwika msalaba ni kupokea mateso pasipo shaka yoyote na bila manung’uniko. Mambo hayo yanaweza kuwa magonjwa, ulemavu, mahangaiko katika maagano yetu, mfano: ndoa, maisha ya wakfu, aka. Ni kuona utukufu wa Mungu katika mateso na mahangaiko yetu ya kila siku tunapokabiliana nayo. Msalaba huo katika maisha utusukume kuubeba kila siku na kusafiri nao hadi golgota alipowambwa Bwana wetu Yesu Kristo. Ni kuyapokea mateso yote na kuyabeba mpaka mwisho bila kumwasi Mungu na mwanaye Yesu Kristo. Tukifanya hivi pasipo shaka yoyote ndipo tutakapo hesabiwa haki na kuushinda mateso hayo. Mateso hubadilika kuwa ushindi, na msalaba huwa kielelezo cha ushindi huo. Hapa ndipo tunapoweza kuiokoa nafsi yetu katika majaribu. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona,” Mt 16:25. Je, upo tayari kuipoteza nafsi yako katika umilele wote?

Kumfuata Yesu ni mwito na matokeo ya kujikana nafsi, na kujitwika msalaba pasipo shaka. Kumfuata Yesu ni kusafiri naye pasipo shaka tukijua na kuamini kabisa kuwa ni yeye tu njia ya umilele, ukweli wa umilele, na uzima wa umilele. Ni kufahamu pasipo shaka na kuamini maneno haya aliyosema Yesu: Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:28-30. Hivyo kitulizo cha mahangaiko na mateso yetu ni YESU TU. Tunapojikana nafsi na kujitwika msalaba wetu bila kufuatana na Yesu alioshinda mateso na maumivu ya msalaba ni bure na kupoteza muda. Katika mahangaiko yote tuyapitiayo kamwe tusimwache Yesu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake,” Mt 16:27


Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wetu, tuongoze katika kweli yako ili tuweze kuibeba misalaba yetu kila siku bila manung’uniko. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario