domingo, 28 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 22 YA MWAKA-C

JUMATATU WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 2:1-5
Zab/Kit: 119:97, 98, 99, 101, 102
Injili: Lk 4:16-30
Nukuu
Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1 

Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5 

Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19 

Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21 

TAFAKARI:Lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake.”

Wapendwa wana wa Mungu, Yesu Kristo ndiye mfano hai na halisi kwetu wa kuiga na kufuata hata kama kwa hali yetu na ubinadamu wetu si rahisi. Leo Yesu katika Sinagogi huko Nazareti, wanapomjua vizuri anawaacha midomo wazi. Ni kweli walimfahamu Yesu katika maana ya historia yake. Mara zote tunajisikia vizuri na nyumbani pale tunapofikiri sawa, na kuwa na maisha yaliyowiyana. Kwa hali hii tunahitaji nguvu ya pekee kuwa tofauti. Yesu anatufundisha kuwa tofauti na kutokufanya mambo kimazoea. Yesu kama ilivyokuwa kawaida ya siku ya sabato, anaingia kwenye sinagogi na kulisoma neno la Mungu, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Hii ndiyo tofauti ya Yesu na kauli mbiu yake. Hiki ndicho kinachomtofautisha Yesu na wengine ingawa neno hili lilishasomwa na wengi waliomtangulia. Kwa kukazia Yesu anasema, “Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21. Maneno haya ndiyo msukumo wa mabadiliko yote na mtazamo mpya juu ya Yesu.

Mwana sayansi Isaac Newton wa Uingereza (1643-1727) alipolichukua jiwa na kulirusha juu na likarudi ardhini na kugundua nadharia “theory” ya mvutano “gravitation,”  hakuwa mwanadamu wa kwanza kurusha jiwe juu na likarudi ardhini. Ila kwa kwenda zaidi ya mazoea ya urushwaji wa jiwe na kurudi ardhini ndiko kunakomfanya leo tofauti na wengine waliomtangulia. Yesu anatualika kutokuishi kwa mazoea, bali tuende zaidi ya kile kilichozoeleka. Ukweli huu ni kwa hali zote za maisha na kwa namna ya pekee mahusiano yetu na wenzetu ambayo msingi wake ni Upendo, Kweli na Haki. Kwenda tofauti na yaliyozoeleka ni mshangao kwa wale wasiopenda kuwa tofauti katika kile kilichojificha. Hivyo, wakamshuhudia (Yesu) wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake, wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu?” Lk 4:22. Historia ya Mtu siyo kikwanzo cha yeye kuwa vizuri, mzuri, au kufanya vizuri zaidi hata kama historia ya kule alikotoka kuonekana kuwa mbaya.

Kwa msisitizo Yesu anatutaka tuione tofauti kati yake na wote waliomtangulia. Naye anasema, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni,” Lk 4:25-26. Leo pamoja na sintofahamu kama hizi tunalo tumaini ndani na katika Kristo. Yesu hatuponji tu majeraha yetu ya ndani na nje, bali hututakasa pia. Naye anasema, Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu,” Lk 4:27. Kristo kwa sasa ndiye utakaso wetu.

Kwa hali ya kawaida hasa kwa yale tuyoyazoea kuishi na kuyasikia, ujumbe huu wa Yesu hukuwapendeza Mafarisayo na waandishi walio kuwa vinara wa kudumisha desturi hizo. Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo,” Lk 4:28. Kwa vile saa yake ilikuwa bado kufika, ghadhabu ile haikumdhuru. Na mambo yalikuwa hivi; Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake,” Lk 4:29-30. Chuki na hila za mwanadamu haziwezi kufanikiwa palipo na mpango wa Mungu. 

Unyenyekevu wa Yesu uliobeba historia yake fupi hapa duniani unakuwa sababu ya hukumu yake. Mara nyingi tunawahukumu watu ndivyo sivyo kutokana na kujua historia zao, maeneo ya kijeografia walikotoka, historia za wazazi wao, mazingira ya makuzi yao, marafiki walioishi nao, na hata mtazamo wao kimaisha. Hili ni kosa kubwa sana kufanya. Hakuna aliyeko hapa duniani kwa bahati mbaya, au kuzaliwa kwa bahati mbaya. Sisi tu malengo na makusudi ya Mungu. Mungu anampango na kila mmoja wetu.

Baada ya Yesu kuwaambia ukweli Waandishi na Mafarisayo kwa kutokuamini kwao, hawapokei ujumbe ule wa ukweli na kubadilika, bali wanatafuta njia ya kumwangamiza. Katika hili Yesu anatujaza ujari kwa kusema, “Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Maana yake ni nini? Ukweli ni kwamba, tunaposimama katika kweli, na kuishi kweli hiyo, twatangaza vita kwa wale wasioipenda kweli hiyo. Kwa upande wa Imani ni vita, si tu ya nafsi, bali roho pia. Roho ambazo hazimwelekei Muumba wake zitakuwa kinyume na yote tusemayo na kuyaishi. Kuishi Ukristo na kumkiri Kristo leo ni vita kubwa ya kiroho. Tulizoea kusikia hadithi za Mashahidi wa Imani karne na nyakati za nyuma, lakini leo ni nafasi na wakati wetu kuwa mashahidi wa Kristo. Kuna kila dalili na sababu za kuutoa ushuhuda huo.

Tunachopaswa kuishi si maisha ya ushindani wa hoja katika majukwaa, bali zaidi ni kuishi na kutoa ushuhuda wa ukimya wa maisha ya kweli ya Ukristo wetu. Jambo hili ni muhimu sana, kwani katika utulivu Mungu yupo na kuonekana. “Na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu,” 1Fal 19:12. Huu ni wakati wa mitetemo ya Imani. Nasi tusienende kadiri ya mitetemo hiyo. Tuitafsiri hiyo mitetemo nako tutakutana na Mungu katika utulivu.

Ni wazi katika kutenda lililo la Mungu, yaani lenye kuongozwa na upendo wa kweli, tujiandae kupata upinzani. Yule mwovu shetani hafurahii yaliyo mazuri na mema yenye kuufunua Utukufu wa Mungu. Yesu Kristo mwenyewe alipata upinzani nyumbani mwake mwenyewe. Katika hili Yesu anasema, Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe,” Lk 4:24. Je, kama hatukubaliki nyumbani kwetu na watu wanaotufahamu iwe sababu ya kutokutenda mema? Jibu ni HAPANA! Tuendelee kutenda wema na upendo kwa wote, kwa sababu asili ya upendo ni Mungu, uwepo wa upendo ni Mungu, na Upendo ni Mungu. Kuyaona haya ya Mungu ndani yetu kwahitaji unyenyekevu na kuepuka kujiinua kusiko na sifa wala siha. Hali hiyo ndani yetu itatuwezesha kusema toka moyoni maneno haya ya Mtume Paulo; Basi, ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” 1Kor 2:1. Mungu ndiye anaye wezesha yote ndani yetu. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu,” 1Kor 2:4-5. Sifa na Utukufu ni kwa Mungu wetu. Amina

Tumsifu Yesu Kristo

“Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu,” Lk 4:21


Tusali:-Ee Yesu tujalie ujasiri. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario