JUMANNE
WIKI YA 22 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 2:10b-16
Zab/Kit: 145:8-9,
10-11, 12-13ab, 13cd-14
Injili: Lk 4:34-37
Nukuu
“akisema,
Acha! Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani,
Mtakatifu wa Mungu,” Lk 4:34
“Yesu
akamkemea, akisema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati,
akamtoka asimdhuru neno,” Lk 4:35
“Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya
Mungu,” 1Kor 2:10b
“Vivyo
hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu,” 1Kor 2:11b
“Maana, Ni nani
aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo,” 1Kor
2:16
TAFAKARI: “Nakujua u
nani, Mtakatifu wa Mungu.”
Wapendwa katika Kristo,
uwepo wa Kristo na Jina lake, ni tishio kwa roho zile zilizo kinyume na mpango
wa Mungu. Pepo wachafu huelewa na kuogopa uwepo wa Kristo. Hakuna roho chafu
zinazoweza kuushinda uwepo wa Kristo. Pepo wachafu hawana amani mara litamkwapo
jina la Yesu. Uwepo wa Kristo ni tishio
kwa wale wote wampingao Kristo. Mapepo yanasema, “Tuna
nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa
Mungu,” Lk 4:34. Utakatifu wa Yesu na Ukamilifu wake ni kielelezo cha maisha
yetu na yale yatupasayo kuishi ili kuurithi ufalme wa Mungu.
Ukamilifu na Utakatifu
wa Yesu ndio unaompa mamlaka ya kukemea roho chafu na kuwaweka huru wale
waliofungwa katika ulimwengu huo wa roho. Ukweli huo hata mapepo yenyewe
yanakiri na kusema, “Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu,” Lk 4:34c. Hata baada
ya ukiri huo wa hayo mapepo, Yesu anakemea roho hiyo chafu na kusema, “Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha
katikati, akamtoka asimdhuru neno,” Lk 4:35. Ndugu yangu, kimbilio lako lipo
wapi?
Ni wazi kati yetu mara
tupatwapo na changamoto za imani ukimbia hapa na pale, na kushika hiki na kile ili
kupata ulinzi. Kwa msukumo na woga huo, wengi ujikuta tumejiweka wenyewe wakfu
kwa shetani kwa kupenda au kutokupenda kwa njia mbalimbali. Mfano: wengi wetu
ni vinara wa ibada za mitambiko mara kwa mara na zisizo na kikomo. Wapo pia baadhi yetu huzindika nyumba zao
ikiwa ni pamoja na sehemu zao za kazi na biashara. Wengine na walio wengi, huziweka
mali na fedha zao wakfu kwa shetani kabla ya kuzitumia, nk. Haya yote ni tokeo la
hofu na ujinga.
Hofu na ujinga huu
kamwe hauwezi ukawa ndiyo salama yako. Hofu na ujinga huu mwisho wa siku
utakuingiza kwenye uovu mwingine na mkubwa zaidi. Ishinde hofu yako kwa
kumwamini Kristo Yesu pasipo shaka. Kwa kuwa “hakuna wokovu katika mwingine
awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu
litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:12. Je, ndumba, hirizi, na haya
mazindiko yako, yanasema chochote kuhusu wokovu wako? Tafakari na chukua hatua
mapema!
Wapendwa wana wa Mungu,
unavyo yakumbatia yaliyo ya shetani, yaani, ndumba, hirizi, mazindiko na hata
wewe mwenyewe kujiweka wakfu kwa shetani na mali zako, Roho yule wa Mungu
aliyeko ndani yako huondoka na kukuacha. Ukweli ni kwamba, miili yetu ni hekalu
la Roho Mtakatifu, 1Kor 6:19. Na kwa mantiki hiyo, tunapolinajisi hekalu hili
ndivyo hivyo hivyo tunavyomfukuza Roho huyo ndani yetu. Kazi ya Roho huyo ndani
yetu “huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu,” 1Kor 2:10b. Utawezaje kuyajua mafumbo ya Mungu kama walinajisi
hekalu la Roho huyo, yaani, mwili wako? Ndugu yangu tunayesafiri sote katika
tafakari hii, “mambo ya Mungu hakuna
ayafahamuye ila Roho wa Mungu,” 1Kor 2:11b. Bila Roho wa Mungu ndani yako ni
sawa na kapu tupu licha ya kwamba kapu hilo laweza kubeba chochote kile. Roho Mtakatifu ndani yako ni ulinzi tosha wa
Mungu. Ikiwa mwili bila Roho Mtakatifu ndani yake hakuna ulinzi, ni sawa na
kapu tupu licha ya uwezo wa kapu hilo kubeba chochote kile.
Pamoja na ulinzi huo wa Roho Mtakatifu
ndani yetu, tusifananishe roho hiyo na roho ya
dunia. Kwa maana nyingine “sisi hatukuipokea
roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua
tuliyokirimiwa na Mungu,” 1Kor 2:12. Utaithamini na kuitunza zawadi ukijua thamani yake. Uthaminishwaji wa Roho
ndani yetu ndio utupao uwezo wa kusema
zaidi ya hekima ya kibinadamu. “Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa
kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya
rohoni kwa maneno ya rohoni,” 1Kor 2:13. Na hili twalifanya siyo kwa nguvu zetu
na werevu wetu, bali yote twawezeshwa kwa neema za Mungu.
Kwa mantiki hiyo ni
wazi kwamba “mwanadamu
wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi,
wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni,” 1Kor 2:14.
Kwa maneno mengine ni kwamba, mtu yule awekaye matumaini yake yote kwenye nguvu
nyingine, mfano, kujiweka wakfu kwa shetani, hatoweza kufahamu nguvu ya Roho
Mtakatifu ndani yake. Badala yake, “mtu wa
rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu,” 1Kor 2:15. Mtu huyu ni
yule anayeongozwa na Roho wa Mungu ndani yake, na mwenye hofu hiyo ya Mungu. “Maana,
Ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya
Kristo,” 1Kor 2:16. Kristo ndiye kielelezo chetu kwa sababu ni katika Yeye tu
twaweza kuokolewa Naye.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini
sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate
kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu,” 1Kor 2:12
Tusali:- Ee Yesu Mwema, tujalie Nguvu
ya Roho wako Mtakatifu ili tuyawaze daima yaliyo Matakatifu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario