IJUMAA
WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 16:1-15, 60, 63
Zab: Isa 12:2-3, 4bcd, 5-6
Injili: Mt 19:3-12
Nukuu
“Nami
nilipopita karibu nawe, nikakuona ukigaagaa katika damu yako, nalikuambia,
Ujapokuwa katika damu yako, uwe hai; naam, nalikuambia, Ujapokuwa katika damu
yako, uwe hai,” Eze 16:6
“Nalikufanya
kuwa maelfu-elfu, kama mimea ya mashamba, ukaongezeka, na kuzidi kuwa mkubwa,
ukapata kuwa na uzuri mno; matiti yako yakaumbwa, nywele zako zikawa zimeota;
lakini ulikuwa uchi, huna nguo,” Eze 16:7
“Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba
mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema,
Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao
wawili watakuwa mwili mmoja?” Mt 19:4-5
“Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu,
aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi,” Mt 19:8
“Nami
nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya
uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini,” Mt 19:9
TAFAKARI: “Kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu.”
Wapendwa wana wa Mungu, tendo la uumbaji wa Mungu siyo kama mtengeneza
saa ambaye akisha maliza kazi yake huiacha saa ikajiendea yenyewe tu. Mungu
baada ya kutuumba uendelea kutuumba tukiwa na ushirika naye huku tukiuelekea
ule ukamilifu alionao Yeye. Ni katika maana hii, Yesu anatuwasa na kutukumbusha
kwamba, “ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa
mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Huu ni uumbaji endelevu wa nafsi na roho.
Ni katika mwendelezo huu wa uumbaji endelevu wa nafsi na
roho, Nabii Ezekieli anatumia lugha ya picha kuelezea ukengeufu na uasi wa wana
wa Israeli hasa pale walipo mpiga Mungu kisogo. Na kwa upande mwingine, somo
hili la kwanza linaonyesha wazi kwamba Mungu hakuacha kuwa karibu nao kwa
kuonyesha huruma na upendo wake kwao. “Nami
nilipopita karibu nawe, nikakuona ukigaagaa katika damu yako, nalikuambia,
Ujapokuwa katika damu yako, uwe hai; naam, nalikuambia, Ujapokuwa katika damu
yako, uwe hai,” Eze 16:6. Tatizo walilikuwa nalo wana wa Israeli ni ile hali ya kuupoteza uhasili wao mara walipokutana
na mila na desturi za mataifa mengine. Mchanganyiko huu uliwafanya kuwa uchi
kiimani licha ya kwamba Mungu aliwapigania na kuwafanya kuwa Taifa kubwa. Naye
anasema, “nalikufanya kuwa maelfu-elfu,
kama mimea ya mashamba, ukaongezeka, na kuzidi kuwa mkubwa, ukapata kuwa na
uzuri mno; matiti yako yakaumbwa, nywele zako zikawa zimeota; lakini ulikuwa
uchi, huna nguo,” Eze 16:7. Taifa lolote lile linapovunja misingi yake upoteza
uhasili wake na kukosa dira. Hiki ndicho kilio cha waasisi wa mataifa yetu.
Pasipo msingi imara kuta za nyumba haziwezi kulibeba paa la nyumba vizuri.
Lazima nyufa zitakuwepo tu.
Hata
katika hali hiyo ya kuupoteza uhalisi wao na kutokuwa na dira kiimani, Mungu
hakuwaacha. Mungu alizidi kuwa karibu nao na kuonyesha upendo na huruma yake. “Basi,
nilipopita karibu nawe, nikakutazama; tazama, wakati wako ulikuwa wakati wa
upendo; nikatandika upindo wa vazi langu juu yako, nikakufunika uchi wako;
naam, nalikuapia, nikafanya agano nawe, asema Bwana MUNGU, ukawa wangu,” Eze
16:8. Hizi ni zile nyakati za neema na baraka walipokuwa na mshikamano na
Mungu. Mungu hakuchoka kuanza upya na wana wa Israeli hata katika udhaifu wao.
Naye Mungu anawakumbusha na kusema, “kisha
nikakuosha kwa maji; naam, nalikuosha kabisa damu yako, nikakupaka mafuta; nikakuvika nguo ya taraza, nikakupa
viatu vya ngozi ya pomboo, nikakufunga nguo ya kitani safi kiunoni mwako,
nikakufunika kwa Hariri,” Eze 16:9-10.
Ndugu
yangu, hali na mazingira haya kwa upande wako na wangu, ni nyakati zile
tubarikiwazo si kwamba tu watakatifu sana kuwazidi wengine, bali Mungu huruhusu
neema na baraka zake kwetu katika huruma na upendo wake. Na hivi ndivyo Mtume
Paulo anavyotueleza juu ya neema ya Mungu inavyofanya kazi ndani yetu; “Lakini kwa neema ya
Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali
nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya
Mungu pamoja nami,” 1Kor 15:10
Mungu hakuzuia neema na
baraka kwa wana wa Israeli licha ya udhaifu waliokuwa nao. Upendo wa Mungu kwa
taifa hili ulikuwa kama kuku na vifaranga vyake. Naye Yesu anawakumbusha na
kusema, “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye
manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka
kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga
vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka!” Mt 23:37. Na hivi ndivyo Mungu alivyowapenda upeo. “Nikakupamba kwa mapambo pia, nikatia vikuku mikononi mwako,
na mkufu shingoni mwako,” Eze 16:11.
Mungu
aliwapamba na kuwainua juu zaidi ya maitaifa mengine yote, Eze 16:12-13. Mungu aliufunua utukufu wake kwao na kuwatia
utukufu huo, Eze 16:14, lakini walijisahau katika fahari na uzuri huo na mwisho
kuzama katika ukahaba kwa sababu ya sifa, Eze 16:15. Ukahaba unaozungumziwa
hapa ni ile hali ya kila kitu ni ‘ruksa’ bila kujali uhalisi wao na misingi yao
kiimani. Hatuwezi kujichanganya kwa kila kitu na mwisho wa siku tukasema kila
kitu ni sawa. Katika swala la imani si vizuri kuwa na falsafa ya chura. Huwezi
kujua pozi alilokuwa nalo chura ni la kusimama au kuchuchumaa. Ni heri kuwa
baridi au moto kiimani, kuliko kuwa vuguvugu.
Mungu kwa kutambua
kwamba Israeli ni taifa lake teule, hachoki kufanya tena na tena agano na wana
hawa wa Israeli. “Walakini
nitalikumbuka agano langu nililolifanya pamoja nawe, katika siku za ujana wako,
nami nitaweka imara agano la milele pamoja nawe,” Eze 16:60. Upendo wa Mungu kwetu ni waajabu sana. Mungu
anakupenda kiasi hiki ili siku ya mwisho “upate
kukumbuka, na kufadhaika, usifumbue kinywa chako tena, kwa sababu ya aibu yako;
hapo nitakapokusamehe yote uliyoyatenda, asema Bwana MUNGU,” Eze 16:63. Je,
‘utakuwa na la kujiteteza zaidi ya kilio na kusaga meno?’ Lk 13:28. Haya yote
ni kwa sababu ya ugumu wa mioyo.
Na
katika Injili ya leo tunaona Mafarisayo wanamtega Yesu kuhusu swala la talaka.
Swali ni hili: Je! Ni halali mtu
kumwacha mkewe kwa kila sababu? Kwa kujibu swali hili, Yesu anawarudisha kwenye
lengo na makusudi ya Mungu la kumuumba mtu mke na mtu mume. Uumbaji huo
ulilenga ukweli huu kwamba, “mtu atamwacha
babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja?” Mt
19:4-5. Kuwa mwili mmoja siyo kitu cha
kujibandua tena, wala hakuna hoja ya ubinafsi, yaani, madai ya hiki ni changu.
Kuhusu fumbo hili la
kuwa mwili mmoja, Yesu anasisitiza kwa kusema, “Hata
wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu
asiwatenganishe,” Mt 19:6. Hapa hesabu ya Mungu ni 1+1=1, na siyo 2. Kwa
mantiki hiyo, hayo wayafanyayo ambayo wanataka uhalali kutoka kwa Yesu halikuwa
kusudi la Mungu wala Yeye Yesu hawezi kubadili mpango huo. Naye anawaambia
kwamba swala hilo mlifanyalo liliwezekana kwenu kwa kupitia Musa “kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa
ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi,” Mt 19:8. Kwa
maana nyingine, yalikuwa maamuzi ya kukubaliana kwa kutokubaliana. Na hapa
ndipo pale ilipo dhana ile ya Yesu kwamba, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua
torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka
mbingu na nchi zitakapoondoka,yodi moja wala nukta moja ya torati haitaoondoka
,hata yote yatimie,” Mt 5:17-18
Fundisho
la Yesu ni hili: “Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa
sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa
azini,” Mt 19:9. Ndugu yangu, mazoea hujenga tabia. Kwa fundisho hili,
wanafunzi wake Yesu walikwazika na kumwambia, “Mambo
ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa,” Mt 19:10. Je, kuna ugumu gani hapa
wa kutokuoa kama ni wito wako kufanya hivyo, zaidi ya kuwa na moyo mgumu na
wakutokubadukana na mila na desturi zetu zilizo mbaya? Kwa fundisho hili la Yesu,
ni wazi hakuna mbadala mwingine zaidi ya kuishi na huyu uliye naye. Maisha ya
ndoa kila siku ni kurekebishana na kuumbana. Hapa tuna uumbaji endelevu wa
nafsi na roho katika kusaidiana kuelekea utakatifu.
Hata
hivyo, Yesu anawatoa wasiwasi na dukuduku wanafunzi wake kuhusu fundisho
alilolitoa. Naye anasema, “Si wote wawezao
kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa,” Mt 19:11. Waliojaliwa hapa ni wale
waliopewa uwezo huo. Kwa maana nyingine kuoa au kuolewa siyo ‘kamtindo fulani
cha maisha,’ katika maana ya kuiga kwa vile
fulani kafanya hivyo na wewe ufanye hivyo katika hali ya kukurupuka na bila
maandalizi. Je, umejipima sawa sawa? Kwa kuelezea ukweli wa jambo hili kwa
undani, Yesu anasema, “wako
matowashi waliozaliwa hali hiyo toka matumboni mwa mama zao; tena wako
matowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi; tena wako matowashi waliojifanya
kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na
alipokee,” Mt 19:12.
Kwa
maneno mengine, wapo wasio na uwezo huo wa kuoa au kuolewa kwa sababu
wamezaliwa hivyo. Wapo walikuwa na uwezo huo wa kuoa na kuolewa lakini
walifanywa hivyo na mwisho wa siku kutokuwa na uwezo. Hawa ni wale ambao hasa
nyakati zile za wafalme, walifanywa hivyo ili kufanya kazi katika nyumba za
wafalme kwa kutokuleta madhara katika familia ya kifalme (hasa katika mahusiano
kimapenzi). Wengine walifanywa hivyo ili kutoa burudani nzuri kwa wafalme hasa
kwa kuimba na michezo mengine. Na kundi la mwisho ni wale walioamua kutokuoa au
kuolewa kwa kuyatoa maisha yao wakfu kwa ufalme wa mbinguni. Hawa ni Watawa wa kiume na kike,
Watawa (Makleri), Makleri (wasio watawa).
Tumsifu Yesu Kristo!
“Wanafunzi wake wakamwambia, Mambo
ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa,” Mt 19:10
Tusali:- Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu
Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. Amina
Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario