viernes, 12 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 19 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 18:1-10, 13b, 30-32
Zab: 51:12-13, 14-15, 18-19
Injili: Mt 19:13-15
Nukuu
“Neno la Bwana likanijia tena, kusema, Je! Maana yake ni nini hata mkatumia mithali hii katika Israeli, mkisema, Baba wamekula zabibu mbichi, nao watoto wakatiwa ganzi la meno?” Eze 18:1-2 

Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hamtakuwa na sababu ya kuitumia tena mithali hii katika Israeli,” Eze 18:3 

 “Basi, nitawahukumu ninyi, nyumba ya Israeli, kila mmoja kwa kadiri ya njia zake, asema Bwana MUNGU. Rudini, mkaghairi, na kuyaacha makosa yenu yote; basi hivyo uovu wenu hautakuwa uharibifu wenu,” Eze 18:30

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; jifanyieni moyo mpya na roho mpya,” Eze 18:31a 

Maana mimi sikufurahii kufa kwake afaye, asema Bwana MUNGU; basi ghairini, mkaishi,” Eze 18:32

 “Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao,” Mt 19:14 

TAFAKARI: “Maana mimi sikufurahii kufa kwake afaye, asema Bwana MUNGU; basi ghairini, mkaishi.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha ya kiroho na yenye furaha ni kuishi bila hatia. Mtu anayeisha katika hatia, hutumia muda wa maisha yake yote kupekua lawama na kuficha aibu. Hivyo watu wanaoongozwa na hatia wanaonewa sana na kumbukumbu. Wanaruhusu mambo yaliyopita kutawala mambo yao ya usoni. Wanajiadhibu bila kujua kwa kuharibu mafanikio yao. Kaini alipotenda dhambi, hatia yake ilimtenga na Mungu, na Mungu akasema, "utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani," Mwa 4:12. Hii inawaeleza jinsi watu wengi walivyo siku hizi-wanatangatanga katika maisha bila lengo. Mfano mzuri angalia katika vyama vyetu vya kitume. Wapo walio wengi huama chama kimoja cha kitume kwenda kingine na mwisho huishia katika nyumba za sala. Nyumba za sala hapa ninamaanishisha vijikanisa vinavyojiibua na kujiinua kwa wachungaji wao kuwa manabii.

Ndugu yangu, sisi ni matokeo ya muda wetu uliopita lakini hatupaswi kuwa wafungwa wa muda huo. Kusudi la Mungu halifungwi na muda wako uliopita. “Neno la Bwana likanijia tena, kusema, Je! Maana yake ni nini hata mkatumia mithali hii katika Israeli, mkisema, Baba wamekula zabibu mbichi, nao watoto wakatiwa ganzi la meno?” Eze 18:1-2. Ona! Alimbadilisha muuaji Musa na kuwa kiongozi mzuri; akambadilisha Gidioni aliyekuwa mwoga akawa shujaa na hodari; anaweza kufanya mambo ya ajabu na maisha yako yaliyobaki. Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, hamtakuwa na sababu ya kuitumia tena mithali hii katika Israeli,” Eze 18:3. Kila mtu lazima awajibika kwa kile alichokifanya na siyo kuuzunguka mbuyu. Tazama pia maisha ya Mt. Augustino wa Hippo kabla na baada ya kuongoka kwake. Alitumia muda mrefu kumtafuta Mungu nje kumba Mungu aliwa naye. Ni pale tu alipomwelekea naye akawa na amani ndani yake.

Mungu ni mtaalam wa kutupa mawazo mapya. "Heri aliyesamehewa dhambi, na kusitiriwa makosa yake," Zab 32:1. Kwa maana nyingine twaweza kusema, "wana furaha kubwa wale waliosamehewa hatia zao. Na wana amani wale waliotubu dhambi zao na Mungu amefuta mashtaka yao." Bali kama mtu ni mwenye haki, na kuyatenda yaliyo halali na haki; hakula juu ya milima, wala hakuviinulia macho vinyago vya nyumba ya Israeli, wala hakumtia unajisi mke wa jirani yake, wala hakumkaribia mwanamke wakati wa kutengwa kwake; wala hakumdhulumu mtu, bali amemrudishia mdeni wake rehani yake, wala hakumnyang'anya mtu mali yake kwa nguvu, naye amewapa wenye njaa chakula chake, na kuwavika nguo walio uchi,” Eze 18:5-7. Bila kubadilika na kuziacha njia mbaya, hatutaweza kuwa na amani ndani yetu. Naye Mungu anasema, Tazama, roho zote ni mali yangu; kama vile roho ya baba ni mali yangu, ndivyo ilivyo roho ya mwana mali yangu; roho ile itendayo dhambi itakufa,” Eze 18:4 

Kwa namna hii tunamwona Nabii Yoha anajihukumu na kuchagua kufa kwa sababu ya kuhisi Mungu amemtenga na kumwacha. Hata hivyo Nabii Yona anajua kwa uhakika Mungu anayemtumikia jinsi alivyo, na kusema, “nalijua ya kuwa wewe u Mungu mwenye neema, umejaa huruma, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema, nawe waghairi mabaya,” Yon 4:2c. Hata pamoja na kujua ukweli huu, bado Yona haoni uwepo wa Mungu katika shida zake. Hivyo kwa kukata tamaa anaamua afe. Basi, sasa, Ee Bwana, nakuomba, uniondolee uhai wangu; maana ni afadhali nife mimi kuliko kuishi,” Yon 4:3. Uhai huo ambao Yona anaotaka kuuondoa siyo mali yake. Uhai ni mali ya Mungu na zawadi ya Mungu. Kujiua kwa kukimbia matatizo siyo njia sahihi ya kufanya. Na kukata tamaa ni kumkufuru Roho Mtakatifu. Dhambi hii haisamehewi. “Kwa sababu hiyo nawaambia, Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasamehewa,” Mt 12:31

Kuishi katika kweli na haki ndiyo salama yako. Na mfano wa mtu huyu ni yuleambaye hakumkopesha mtu ili apate faida, wala hakupokea ziada ya namna yo yote; naye ameuepusha mkono wake na uovu, na kufanya hukumu ya haki kati ya mtu na mwenzake,” Eze 18:8. Na huyu ni yule, "azishikaye hukumu za Mungu; mtu huyu ni mwenye haki; hakika ataishi, asema Bwana MUNGU,” Eze 18:9. Kinyume na mpango huu wa Mungu, mtu huyo hatakuwa na maisha hata kama atafanikiwa sana katika njia zake mbaya. Kuhusiana na dhambi za kurithishana Mungu anasema, Walakini mtu akizaa mwana aliye mnyang'anyi, mmwaga damu, atendaye mambo hayo mojawapo. La, hataishi; amefanya machukizo hayo yote; hakika atakufa; damu yake itakuwa juu yake,” Eze 18:10. Hili huwezekana katika mtindo huu tu. Kwa maana hiyo, Mungu anasema, nitawahukumu ninyi, nyumba ya Israeli, kila mmoja kwa kadiri ya njia zake, asema Bwana MUNGU. Rudini, mkaghairi, na kuyaacha makosa yenu yote; basi hivyo uovu wenu hautakuwa uharibifu wenu,” Eze 18:30. Toba na majuto ya kweli ndiyo njia sahihi ya kuurudisha uhusiano ule ‘haribika’ kati yetu na muumba wetu. Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; jifanyieni moyo mpya na roho mpya; mbona mnataka kufa, enyi nyumba ya Israeli?” Eze 18:31

Ndugu yangu, Mungu wetu anasema, Mimi sikufurahii kufa kwake afaye, asema Bwana MUNGU; basi ghairini, mkaishi,” Eze 18:32. Wito wetu ikiwa ndio uhusiano wetu na Mungu ni kuwa na unyenyekevu kama watoto wadogo. Ni husiano usio na shaka, yaani, wa mtoto na mzazi wake. Mtoto huamini yote yawezekana kwa mzazi wake na hakuna cha kumshinda. Ni kwa mantiki hiyo Yesu anasema,Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao,” Mt 19:14. Ndugu yangu tujifunze kwa watoto wadogo.
Tumsifu Yesu Kristo!

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; jifanyieni moyo mpya na roho mpya,” Eze 18:31a


Tusali:-Ee Yesu uliye mwingi wa huruma na rehema, tujalie utulivu wa ndani. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario