JUMATATU
WIKI YA 21 YA MWAKA-C
Somo: 2The 1:1-5, 11-12
Zab/Kit: 96:1-2a,
2b-3, 4-5
Injili: Mt 23:13-22
Nukuu
“Ndugu,
imetupasa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa
kuwa imani yenu inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa
mwingi,” 2The 1:3
“jina
la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu
wetu na ya Bwana Yesu Kristo,” 2The 1:12
“Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa
mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia
hamwaachi waingie,” Mt 23:13
“Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa
mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na
akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili zaidi kuliko
ninyi wenyewe,” Mt 23:15
“Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa
kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga,” Mt
23:16
TAFAKARI: “Imetupasa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu.”
Wapendwa wana wa
Mungu, ‘Moyo usio na shukrani ukausha mema yote.’ Tendo la shukrani licha ya
kusadifu kile kilichotendwa kiwe kidogo au kikubwa, tendo hilo kama lilivyo
ujeuka na kuwa sala au ombi lingine. Unaposema neno ‘asante,’ ni kwa namna hiyo hiyo unafungua ‘uwezekano’
wa kuomba tena. Ni mara ngapi tunasema asante kwa mafanikio tuliyoyafikia au
kuyapata hata kama ni kidogo? Lakini badala yake tunapofaulu katika mambo yetu
utanguliza nafsi na juhudi zetu binafsi. Na tunaposhindwa kuyafikia malengo
yetu ujiweka pembeni na kuwatupia wengine lawama.
Mtume Paulo na wenzake
wanatambua kwamba mafanikio yao katika shughuli za kitume si tokeo la nguvu na
juhudi zao wenyewe, bali ni tunda, mchango, na kazi ya kila mmoja katika
jumuiya ile ya kwanza ya Kikristo. Naye
anasema, “ndugu, imetupasa
kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa kuwa imani yenu
inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa mwingi,” 2The
1:3. Hii ndiyo picha halisi ya kutumika kama kiongozi na siyo kutumikiwa. Na
mazingira haya humjengea kiongozi hali ya kufikika na siyo kuogopwa au
kukimbiwa. Hapa tunaona jumuiya inayoongozwa na malengo dhabiti bila kumtenga
yoyote. Kristo Yesu ndiye dira halisi ya maisha ya jumuiya hii ya kwanza ya
Wakristo, na katika Kristo na ndani ya Kristo wote wanafanywa ndugu. Ikiwa hiki
ndicho kiungo na dhamiri halisi ya maisha, Mtume Paulo akosi kusisitiza ukweli
huu kwa Wakristo wenzake, na kusema, “jina la Bwana wetu Yesu
litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana
Yesu Kristo,” 2The 1:12. Nisipotambua kwamba kuna “zaidi” ya kile nilicho na
ambacho kipo nje ya uwezo wangu kama mwanadamu pamoja na hali na nafasi
niliyokuwa nayo katika jamii, ni rahisi kukoswa unyenyekevu kama msingi wa
fadhila zote.
Pasipo unyenyekevu ni
vigumu kuzama kwa yale yaliyo dhaifu ndani yangu kwa lengo la kuyaponya au kuyarekebisha.
Pasipo unyenyekevu ni vigumu kujirekebisha, kujikosoa, au kukosolewa. Pasipo
unyenyekevu mtu utumia muda mwingi kujitetea na kujilinda hata pale pasipokuwa
na sababu ya kufanya hivyo. Na pasipo na unyenyekevu na hasa pale nitumiapo
muda mwingi kujitetea na kujilinda, basi kila kisemwacho hata kwa nia njema
nitakitafsiri kama ‘sengenyo’ kwangu.
Wapendwa katika Kristo,
pamoja na ufahamu wa Maandiko Matakatifu waliokuwa nao waandishi na Mafasisayo,
walikoswa unyenyekevu na mwisho wa siku waliyatafakari Maandiko hayo Matakatifu
kukidhi hitaji lao na kujikuza kwao. Kwa mtazamo na tabia yao hii, waliinyambua
torati kwa kujifaidisha wao ilhali sehemu kubwa ya jamii ilikuwa na mateso
makubwa kutoka na tafsiri ile ya Torati. Hivyo tafsiri hii ya Torati (TALMUD),
badala ya kuwaweka karibu na Mungu ilizidi kuwaweka mbali na Mungu. Na huu ndio
uliokuwa ugomvi kati ya Yesu na hawa Mafarisayo na waandishi. Naye Yesu
anawakaripia na kusema, “Ole wenu waandishi
na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi
wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie,” Mt 23:13
Waandishi na Mafarisayo
hawa walitumia upenyo huo wa iliyo tafsiri ya Torati-Talmud na kuiweka pembeni
Torati ili kujifaidia kutoka kwa wajane na wasiojiweza. Hakika waliwatiisha
mizingo mikubwa na mizito kundi hili la wanyonge ilhali wao wakijiweke pembeni
na kujihurumia. Na Yesu anawapasha ukweli na kuwaambia, “Ole
wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na
kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi,” Mt
23:14. Ni sawa na kusema wewe ni rafiki ya masikini, lakini wakikupiga kisogo
tu unawaponda migongo yao kwa marungu.
Unafiki huu hauna
tofauti na siasa zetu na hasa inchi za bara letu la Afrika. Twawatumia wanyonge
kama ngazi, na tukishafika huko juu kwenye magorofa yetu (vyeo tulivyokuwa
tunavitaka) tunasahu ngazi zile (wanyonge) bila kujua ipo siku tutawajibika
shuka chini (kufikia ukomo wa uongozi). Na ndivyo Yesu alivyo waambia waandishi
na mafarisayo, na leo anakuambia wewe na mimi tuliopewa dhamana kwamba, “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa
kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa
mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa jehanum mara mbili
zaidi kuliko ninyi wenyewe,” Mt 23:15. Pasipo na utaratibu hapana akili, na
kinyume chake ni sawa, yaani, palipo na akili pana utaratibu. Yesu kwa hakika
aliona wazi wazi kujikanyaga kwao, yaani, waandishi na Mafarisayo juu ya
Torati.
Hali hii, yaani, kujikanyaga
kwa iliyo wazi na kweli Yesu anailinganisha sawa na UPOFU hasa ule wa kujitakia
kwa viongozi wanafiki. Naye Yesu anasema, “Ole
wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali
mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga,” Mt 23:16. Ni mara ngapi
tunawaona na kuwasikia viongozi na watawala wetu kukinzana na Katiba ikiwa
ndiyo sheria Mama? Tunatofauti gani kati yetu na waandishi na mafarisayo juu ya
kukinzana na torati? Kwa nini basi twapindisha iliyo kweli kwa manufaa na
maslahi yetu binafsi au ya vikundi vyetu (vyama vya siasa)? Isipofika mahali
tukaona kijiko kama kilivyo kijiko, na badala yake tukaona na kulazimisha
wengine waone kijiko kama koleo, hatutaweza kuondokana na vurugu na hata
ukandamizaji wa haki za binadamu kwa kigezo cha kuilinda amani. Amani ni tunda
la haki. Hivyo siwezi kutumia njia ovu kwa kigezo cha kuilinda amani. Kwa
maneno mengine ni kwamba, ‘si vyema na siyo sahihi kulifikia lililo jema na
zuri kwa kutumia njia ovu.’ Hapana!
Ni heri kuwa mjinga
kwani upo utayari wa kujifunza na kuelewa, kuliko kuwa mpumbavu, yaani, asiye
na utayari wa kujifunza akijiaminisha kuelewa kila kitu kumbe hajui chochote.
Ndugu yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, hakuna binadamu yeyote
katika ulimwengu huu mwenye kujua moja ya kumi ya mambo yote katika ulimwengu
huu. Uwapo katika ulimwengu huu upo “shuleni” kujifunza kutoka kwa wenzako na
mazingira yanayokuzunguka hadi siku ya kiama yako. Na ndivyo Yesu anavyowaona
viongozi vipofu na kusema, “Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo
kubwa, ile dhahabu, au lile hekalu liitakasalo dhahabu?” Mt 23:17. Kwa maneno
mengine ‘yatupasa kuepuka majibu rahisi kwa maswali magumu’ kwa sababu
hatutakuwa tunatatua tatizo au kutafuta ufumbuzi wa tatizo, bali kuchochea tatizo
na migogoro isiyo na sababu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ole
wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali
mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga,” Mt 23:16
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tuongoze kwa iliyo kweli na haki. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario