martes, 23 de agosto de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA MTAKATIFU BARTOLOMEYO, MTUME

SIKUKUU YA MTAKATIFU BARTOLOMEYO, MTUME
Somo: Ufu 21:9-14
Zab/Kit: 145:10-11, 12-13, 17-18
Injili: Yoh 1:45-51
Nukuu
Upande wa mashariki milango mitatu; na upande wa kaskazini milango mitatu; na upande wa kusini milango mitatu; na upande wa magharibi milango mitatu,” Ufu 21:13

Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo,” Ufu 21:14 

 “Nathanaeli akamwambia, Laweza neno jema kutoka Nazareti? Filipo akamwambia, Njoo uone,” Yoh 1:46

 “Nathanaeli akamjibu, Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli,” Yoh 1:49

Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50

Akamwambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51

TAFAKARI:Laweza neno jema kutoka Nazareti? Filipo akamwambia, Njoo uone.”

Wapendwa wana wa Mungu, wale wote waliotukuzwa na Mungu na kuinuliwa juu kabisa hawakuwa watu wa pekee sana katika jamii. Tabia ya Mungu katika kuonyesha ukuu wake uviinua vilivyo dhauriwa katika jamii na kuvidondosha vinavyojikweza mbele za watu. Maandiko Matakatifu yanafunua ukweli huu kwa mifano mingi sana. Kwa ukaribu katika kweli hii tumtazame Mama yetu Bikira Maria. Kwa ushuhuda wa makuu ya Mungu, Mama Bikira Maria asema, “amefanya nguvu kwa mkono wake; Amewatawanya walio na kiburi katika mawazo ya mioyo yao; Amewaangusha wakuu katika viti vyoa vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:51-52. Huyu ndiye Mungu asiyewatupa wanyonge na wale wote wenye kumcha.

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anavyo sherehekea sikukuu ya Mtakatifu Bartolomeyo Mtume, nasi tunapewa nafasi ya kuutafakari upendo wa Mungu usio na upendeleo. Yesu hakuwachagua watu wa pekee sana ili wafanya yale aliyotaka wafanye, yaani, kuieneza kauli mbiu yake ‘ufalme wa Mungu umekaribia, tubuni na kuiamini Injili,’ Mk 1:15. Badala yake aliwachagua watu wa kawaida kabisa na wengine walikuwa na mwonekano mbaya katika jamii kama Mathayo karani, Mt 9:9. Mitume hawakuwa na elimu ya pekee sana. Wengi wao walikuwa wavuvu tu.

 Ndugu yangu, kitu cha kutazama siyo mtu kadiri ya mwonekano wake nan je na mbwembwe zake, bali neema ile ifanyayo kazi ndani yake. Ndiyo kwa maantiki hii utume kwa Mitume unafananishwa kama Bibi Harusi aliyeshuka kutoka mbinguni kama mji wa Yerusalema. Mji huu una milango mitatu pande zote nne, yaani, kaskazini na mashariki, na kusini na magharibi, Ufu 21:13.  “Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo,” Ufu 21:14. 

Katika Injili ya leo tunaona Mitume hawa kuchakuguliwa kwao hakukua swala la kubahatisha. Yesu Kristo alifanya hivyo na kumaanisha hivyo katika uchaguzi wake. Filipo akamwona Nathanaeli, akamwambia, Tumemwona yeye aliyeandikiwa na Musa katika torati, na manabii, Yesu, mwana wa Yusufu, mtu wa Nazareti,” Yoh 1:45. Nathanaeli hakusadiki kweli hiyo, na badala yake aliyashikilea mapokea ya agano la kale na kumwambia Filipo, Laweza neno jema kutoka Nazareti?” Yoh 1:46a. Filipo aliye jaa Imani na Matumaini kwa kile alichokishuhudia akamjibi, “Njoo uone,” Yoh 1:46b.

 Ndugu yangu, Yesu anapokutembelea huwezi kubaki kama ulivyokuwa mwanzo.Nathanaeli akamjibu, Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli,” Yoh 1:49. Hata kwa jibu hili la kina la Nathanaeli, Yesu anataka Nathanaeli ajue zaidi ukweli kuhusu Yesu Kristo. Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50. TUKIWA NDANI NA KATIKA YESU, tutayaona mengi. Naye Yesu anatuambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu wakikwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu,” Yoh 1:51. Huu ndio utukufu wa Yesu utakao dhihirishwa kwa wale wote wamchao.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Utaona mambo makubwa kuliko haya,” Yoh 1:50b

Tusali:-Ee Yesu tujalie imani dhabiti kama ya Mitume wako. Amina

Mtakatifu Bartolomeyo, Mtume, Utuombee

No hay comentarios:

Publicar un comentario