miércoles, 10 de agosto de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 19 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 12:1-12
Zab: 78:56-57, 58-59, 61-62
Injili: Mt 18:21-19:1
Nukuu
Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi,” Eze 12:2 

 “Sema, Mimi ni ishara kwenu; kama mimi nilivyotenda, wao nao watatendwa vile vile; watahamishwa, watakwenda kufungwa,” Eze 12:11 

 “Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba?” Mt 18:21

Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,” Mt 18:22 

TAFAKARI: Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake

Wapendwa wana wa Mungu, ni ukweli kwamba katika maisha yetu tumeumizwa na kuwaumiza wengine. Kwa mantiki hii kila mmoja wetu anayo maumivu yake ya ndani. Ili kuponya maumivu haya ya ndani yatupasa kusamehe tukitambua pia katika maisha tuliwaumiza watu wengine pia. Injili ya leo inatuwasa kusamehe. Tendo hili si ombi ila ni amri ya Mungu mwenyewe. Sala yetu ya Baba yetu, inaeleza tendo hili la kusamehe kama sharti ya yale tuyaombayo kwa Mungu, “utusamehe sisi kama tunavyo wasamehe wale walio tukosea.” Mfano alioutoa Yesu kwenye Injili ya leo unaonyesha ni kwa namna gani yatupasa kuwa na utu wa kweli na kusamehe pasipo sharti. Pili, yatupasa kuishi na watu vizuri. Kwa kufanya tendo hilo, tutajua kweli ni nani tunayemtumikia na kumfuata.

Je, kipimo cha kusamehe ni kipi? Mtakatifu Augustino anatuambia kipimo cha upendo ni kupenda bila kipimo. Hivyo basi, kipimo cha kusamehe ni kusamehe bila kipimo. Habari njema yetu ya leo, yaani, Injili,  inafafanua ulazima wa kutoa msamaha. Yesu akamwambia Petro, “Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.” Mt 18:22. Ndugu yangu, lazima tufahamu msingi wa swali la Petro. Petro anamwambia Yesu, “Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba?” Mt 18:21. La kujiuliza ni kwamba, kwa nini Petro ajikite kwenye mara saba? Wapendwa katika Kristo, kadiri ya Maandiko Matakatifu, namba saba inamaanisha UKAMILIFU, ILIYOKAMILIKA, YAKUTOSHA. Kwa Petro mara hizo saba za tosha na za pendeza machoni mwa Mungu.

Yesu katika hili hatengui ukamilifu na utoshelevu wa mtazamo huo, bali anaupa maana zaidi na kuutimiliza, kwani Yeye mwenyewe anasema, “Msidhani ya kuwa nilikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17. Tunapotoa msamaha yatupasa kuzama ndani katika tendo la kusamehe na kusamehewa. Ni kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi ndani kwa wale tuliowakosea. Unaposamehe kumbuka pia nawe umesamehewa mara nyingi tu.

Ni mangapi unafanya kinyume na mapenzi ya Mungu, lakini yeye amekupa muda wa kujirudi? Je, angetoa adhabu za hapo kwa hapo ungebaki salama kweli? Kwa nini wasubiri kupigiwa chetezo ndio utoe msamaha? Kwa nini tunawazungusha watu wanapotaka kusamehewa? Kwa nini tunaweka vikwazo ili tuwasemehe watu waliotukosea hata kama weshakiri makosa yao? Jumuiya ya wakristo, na Kanisa kwa ujumla lisilotoa msamaha ni wazi jumuiya hiyo na Kanisa hilo halimwakilishi Yesu Kristo. Mkusanyiko huo utakakuwa mkusanyiko usio na mwelekeo na mbele yake kuna giza kubwa sana!

Kwa Habari Njema hii ya leo, Yesu anatoa simulizi la kuvivaa viatu vya wale waliotusamehe na kujirudi ndani ya nafsi zetu kwa wale tuliowakosea. Hii ndiyo namna ya uzito na ulazima wa kusamehe. Mara nyingi Yesu ameonyesha hali hiyo, na hata umauti wake kwa ajili ya dhambi zetu walisemea jambo hili. Yesu alipoletewa mwanamke mzizi, aliyasema haya, baada ya kulitafakari tukio lile kwa kuandika chini, “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumtupia jiwe,” Yoh 8:7. Wote tunajua kilichofuata baada ya maneno haya ya Yesu.

Kuomba msamaha kama tendo la kujirudi hujenga uhusiano binafsi kati yako na Muumba wako. Mungu kamwe afurahii kuangamia kwa mtu mwovu, bali aiache njia yake mbaya na kumfuata, Eze 33:11. Kutokuwa na uhusiano mzuri na Mungu ni sawa na kuasi. Naye Mungu anasema, Mwanadamu, wewe unakaa kati ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi,” Eze 12:2. Upofu huu usababishwa na majivuno. Ni vigumu sana kwa mtu kwenye majivuno kuyaona madhaifu yake. Huu ni upofu mbaya sana kwa maisha ya kiroho.

Wapendwa wana wa Mungu, Bwana wetu Yesu Kristo ni kielelezo sahihi cha Msamaha wa Mungu. Ndugu yangu, “Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi,” Mdo 5:31. Na katika Kristo “tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi; naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Kol 1:14-15.

Ndugu yangu, msamaha ni Ukristo wetu na maisha yetu kama wafuasi wake Kristo. Msamaha ni tendo la Mungu mwenyewe na sababu ya wokovu wetu. Hakuna anayeishi kwa sababu yake mwenyewe. Hakika tusipowasamehe wale waliotukosea katika mtazamo wa Kimungu na Uwana wake tulioumbwa kwa sura na mfano wake, Mungu huyu tunayemwamini hatakuwa tayari kutusamehe makosa yetu. Yesu anaweka wazi ukweli huu anaposema, Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake,” Mt 18:35. Ndugu yangu, nani wewe usiye samehe?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini,” Mt 18:22


Tusali:-Ee Yesu, nijalie moyo wa msamaha. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario