JUMATATU
WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 1:2-5, 24-2:1a
Zab: 149:1-2, 11-12ab, 12c-14a, 14bcd
Injili: Mt 17:21-26
Nukuu
“Kama kuonekana kwa upinde wa mvua, ulio katika mawingu siku
ya mvua, ndivyo kulivyokuwa kuonekana kwa mwangaza ule pande zote. Ndivyo kulivyokuwa
kuonekana kwake mfano huo wa utukufu wa Bwana. Nami nilipoona nalianguka
kifudifudi, nikasikia sauti ya mmoja anenaye,” Eze 1:28
“Akaniambia,
Mwanadamu, simama kwa miguu yako, nami nitasema nawe,” Eze 2:1
“Lakini
namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga,” Mt 17:21
“Nao
walipokuwa wakikaa Galilaya, Yesu akawaambia, Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa
katika mikono ya watu, nao watamwua, na siku ya tatu atafufuka. Wakasikitika sana,” Mt 17:22-23
“Naye
alipoingia nyumbani, Yesu alitangulia kumwuliza, akisema, Waonaje, Simoni?
Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au kwa
wageni?” Mt 17:25
“Naye
aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, wana ni mahuru,”
Mt 17:26
TAFAKARI: “Mwanadamu, simama kwa miguu yako,
nami nitasema nawe.”
Wapendwa wana wa Mungu, tunapolitazama somo hili la kwanza kutoka kwa
Nabii Ezekieli tunapigwa na mshangao mkubwa hasa pale Ezekieli anapojaribu
kuelezea kisichoelezeka, yaani, muonekano wa Utukufu wa Bwana. Nabii Ezekieli anaelezea
viumbe vinne, huku kila kiumbe kikiwa na sura nne na mabawa manne. Katikati ya
viumbe hivi kuna moto na mwanga uangazao. Jambo lingine la ajabu la hawa viumbe
ni kwamba kila kiumbe alikuwa na tairi ndani ya tairi. Hivyo viumbe hivi
vilipotaka kutembea na matairi nayo yalitembea navyo. Sauti za mbawa za viumbe
hawa ilikuwa kama tufani, kama sauti ya jeshi kuu. Juu ya viumbe hawa kulikuwa
na mduara na wenye kung’ara, na juu ya mduara huu kulikuwa kuna kitu kama kiti.
Na hapa ndipo alipokuwepo Bwana.
Hata hivyo Nabii Ezekieli hasemi kwamba alimwona Bwana, bali aliona Utukufu
wa Bwana, Eze 1:28. Ni kwa namna hii tunaona pasipo shaka kwamba Ezekieli
analazimika kutumia taswira hii ya ajabu kuelezea maono haya. Ugumu upo hapa;
utawezaje kuelezea kitu ambacho unachotaka kukieleza hakina nukuu ya vipimo
halisi? Ni sawa na kumwelezea kipofu juu ya rangi nyekundu ambaye hakuwahi
kuona rangi. Hili ndilo tatizo analokutana nalo Ezekieli anapojaribu kueleza
juu ya utukufu wa Mungu. Ezekieli anatumia taswira ya vitu ambavyo
tumeshaviona. Kwa maana nyingine Ezekieli anajaribu kueleza kisichoelezeka,
yaani, Utukufu wa Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu, hata kama hatuwezi kuelezea Utukufu wa Mungu
kama ulivyo, hatuwezi kupinga kwamba hakuna Utukufu huo. Mimi na wewe, pamoja
na vyote tunavyoviona na tusivyoviona vinaufunua Utukufu wa Mungu. Kumbe jambo
la msingi ni mimi kutambua Utukufu wa Mungu upo, na kwa wakati huohuo
nimezungukwa na Utukufu wa Mungu. Hapa ndipo tunapoona wajibu wa pekee wa
mwanadamu kuyatunza na kuyalinda mazingira yanayomzunguka kama wakili pekee wa
Mungu, Mwa 1:28, 2:15, na 3:17-19. Ni wajibu msingi kwako na kwangu kuifanya
dunia yetu hii mahali pazuri na salama kwa kuishi, tukitambua ndiye ‘Mama
yetu,’ atupaye kila kitu tungali hapa dunia. Nafasi na umuhimu wa kila mmoja
wetu katika kweli hii, imezungumzwa vizuri katika ‘Waraka ule maalumu’ wa Baba
Mtakatifu Francis, “Shukrani kwako, Ee Bwana wangu,”-Laudato si, mi signore,
66-70.
Hivyo ndugu zangu, kuelewa Utukufu huu wa Mungu yatupasa kujua wajibu wetu
na kuwa waaminifu kwa yale yote tunayokirimiwa bure, ikiwepo hewa hii
tunayoitumia. Na hii ndiyo maana ya maneno haya, “Mwanadamu,
simama kwa miguu yako, nami nitasema nawe,” Eze 2:1. Kusimama huku ni kujua
wajibu wako pale ulipo. Na kwa kufanya hivyo uwepo wa Mungu utaonekana. Mfano tukiendelea kukata miti hovyo tutaweza
kweli kupata hewa nzuri kwa afya yetu? Na ingekuwa ni kulipa kodi ya hewa
tunayoitumia ni wangapi kati yetu wangehimili pigo hilo?
Yesu
katika Injili yetu ya leo anatupa mfano wa kuwajibika hasa pale watozao
nusu-shekeli walipomwendea Petro na kujua kama Mwalimu wao, Yesu Kristo hulipa nusu-shekeli. Kwa mtazamo wa leo tungeweza kusema kwamba ‘mamlaka
ya mapato na ukusanyaji wa kodi, TRA,’ walitaka kujua kama Yesu/Kanisa analipa
kodi au linalipa kodi. Na kabla ya Petro kupeleka taarifa ile kwa Yesu,
alikwisha jua habari ile kabla. Na ndipo alipomuuliza Petro; “Waonaje,
Simoni? Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au
kwa wageni?” Mt 17:25. Jibu la Simon Petro
lilikuwa, ‘ushuru ama kodi hulipwa kwa wageni.’ Naye Yesu anamjibu, “basi kama
ni hivyo, wana ni mahuru,” Mt 17:26. Neno “mahuru,” la maanisha kutokutozwa
kodi au ushuru, isiyotozwa. Je, mambo yalikuwa hivyo? Jibu ni hapana! Kwa
kawaida na ndivyo ilivyokuwa, kodi walilipa wageni katika maana ya hali ile ya
kuwa utumwani. Mshangao ni kwamba pamoja na kuwa katika nchi yao wanalazimika
kulipa kodi. Na ukweli ni kwamba ikiwa Petro ni mwana wa Daudi, Mfalme wa
Israeli, alikuwa ni mmoja wa nyumba na familia ya Mfalme, na kwa heshima hii,
isingestahili kulipa kodi.
Hata hivyo wanawajibika kulipa nusu
shekeli kama tozo la kidini kuhusiana na huduma ile itolewayo kwa kuabudu
kwenye Hekalu. Hapa haikumaanisha kununua huduma bali lilikuwa swala la
uratibishaji wa shughuli za hekalu. Na mwisho wa siku Yesu ataamuru zoezi hilo
lifanyike huku akiitazama ile saa yake, yaani, mateso na kifo chake pale
msalabani, Mt 17:22-23. Ni wazi fedha zilizokuwa zinatozwa wengi walifaidika
nazo na ndiyo maana Mafarisayo na Waandishi walikuwa wakali sana Yesu alipokuwa
anaongelea juu ya Hekalu na kuwaambia, ‘Livunjeni
hekalu hili, nami katika siku tatu nitalisimamisha,’Yoh 2:19. Hapa hawakumwelewa ingawa
Yesu alikuwa anaongelea habari za mwili, Yoh 2:21. Ndugu yangu, kama kodi ni
wajibu wetu kulipa, basi kusiwe na ujanja ujanja katika wajibu huu. Hata hivyo
uzoefu waonyesha kwamba watu wenye kipata kidogo ndiyo walipaji kodi kuliko
wenye kipato kikubwa. Kwa ukubwa wao imekuwa rahisi kuwatia upofu wahusika na
nguvu yote ya kukusanyaji kodi kuwalemea wanyonge. Lazima kuwa makini sana
katika eneo hili. Na kila mtu atimize wajibu wake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Naye
aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, wana ni mahuru,”
Mt 17:26
Tusali:-Ee
Yesu, pamoja na Umungu wako, hukuacha kuwajibika kwa yale yahusuyo ubinadamu
wetu. Tukumbushe wajibu wetu kila siku. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario