viernes, 19 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 20 YA MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 20 YA MWAKA-C

Somo: Eze 43:1-7
Zab/Kit: 85:9ab-10, 11-12, 13
Injili: Mt 23:1-12
Nukuu
na tazama, huo utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea kwa njia ya mashariki; na sauti yake ilikuwa kama mshindo wa maji mengi, nayo nchi iling'aa kwa utukufu wake,” Eze 43:2

 “Mwanadamu, hapa ni mahali pa kiti changu cha enzi, na mahali pa nyayo za miguu yangu, nitakapokaa kati ya wana wa Israeli milele; na nyumba ya Israeli hawatalinajisi jina langu takatifu tena, wao, wala wafalme wao, kwa mambo yao ya kikahaba, na kwa mizoga ya wafalme wao, katika mahali pao pa juu,” Eze 43:7

Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi, yo yote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi,” Mt 23:2-3 

Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao,” Mt 23:4 

 “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8
 “Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu,” Mt 23:11 

Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa,” Mt 23:12 

TAFAKARI:Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuwa na uwezo wa kuzaa kwa weza kukufanya mama au baba, ila siyo kigezo cha wewe kuwa Mama au Baba katika maana ya MZAZI. Wapo wengi kati yetu wenye watoto ila bado hayajawa Baba wala Mama. Kumbe kutambulika kwako kuwa Mama au Baba haijalizi uwezo ule tu ukupelekeao kuwa na familia, bali zaidi ni kutumika kwako na pasipo kujibakiza kama Mama au Baba kwa nafasi hiyo ya pekee katika familia yako. Kwa mantiki hii, huitaji kujivika ‘BANGO’ lenye maandishi “mimi ndiye mama au baba wa familia hii.” Wana familia, yaani, watoto mlio nao, na mengine mnaowajibika kwao kama walezi wao, huwatambua kwa kuwajibika kwenu kila mmoja (Baba au Mama) kwa nafasi yake.

Ni vyema tukajua kwamba, kila aliye na nafasi ya kuwa “Mzazi” ni mshiriki wa pekee kama kiumbe shirikishwa cha Mungu katika kazi takatifu ya uumbaji. Nafasi hii na upekee huu hata malaika hawakupewa na Mungu. Haya yote, yaani, ‘UUMBAJI WA MUNGU katika ujumla wake,’ na yale yote ashirikishwayo mzazi na yenye uhusiano na uumbaji wa pili, yaani, uumbaji endelevu wa Mungu, na wenye kumshirikisha mwanadamu katika ujumla wake, uifunua Furaha ya Mungu, Utukufu wa Mungu, na Uwepo wa Mungu. Na ndivyo ilivyo kama asemavyo Mzaburi kwamba, Wewe, MUNGU, Bwana wetu Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote! Wewe umeuweka utukufu wako mbinguni,” Zab 8:1.

Tukizama ndani zaidi, uumbaji huu wa Mungu katika ujumla wake waufunua Utukufu wa Mungu. Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake,” Zab 19:1. Kazi kubwa ya mwanadamu mwenye ufahamu wa kutosha na hofu ya Mungu ndani yake, hana cha kujivunia wala kujikweza, zaidi ya kumpa Mungu sifa na utukufu kadiri anavyopumua. Mpeni Bwana utukufu wa jina lake; Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu,” Zab 29:2. Lakini mbona basi tunakuwa na kiburi na majivuno ya Jogoo?  “Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa,” Mt 23:12. Jogoo bila shaka ufikiri asipowika mapema alfajiri, hakutopambazuka. Hii ni faraja tu kwa mpumbavu!

Kwa mjinga na katika maana ya kujifunza, kinywa chake mara zote kitatamka haya; Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako,” Zab 57:5. Tusipotaka kuuona utukufu huu wa Mungu, Mungu huyu huyu utuonyesha kwa namna nyingine. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwa wana wa Israeli nyakati zile za Nabii Ezekieli, na tazama, huo utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea kwa njia ya mashariki; na sauti yake ilikuwa kama mshindo wa maji mengi, nayo nchi iling'aa kwa utukufu wake,” Eze 43:2. Tukumbuke maneno ya Yesu alivyokuwa anaingia mjini Yerusalemu kabla ya saa ile ya kuteswa kwake juu ya Mafarisayo walio mtakaka Yesu awakanye wanafunzi wake wanyamaze, Lk 19:37-39. Naye “akajibu, akasema, Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele,” Lk 19:40.

Ni kwa nini basi twajitwalia mamlaka ya kuwaziba watu wengine midomo wanapotaka kuyatoa yaliyo ndani ya mioyo yao tena kwa utaratibu kubalika? Je, tunakuwa na hofu gani kama tunajiamini kwa kile tukifanyacho kama viongozi au wazazi na ndivyo tulivyo? Utukufu wa Mungu kama tokeo la Mungu kuushirikisha kwa viumbe vyake, hatutaweza kuuzuia utukufu huo hata kama tutawekeza nguvu zetu zote. Na hii ndiyo maana ya maneno haya kwamba, Na huo utukufu wa Bwana ukaingia ndani ya nyumba, kwa njia ya lango lile lielekealo upande wa mashariki,” Eze 43:4. Na hapa ndipo waja wa Mungu hujazwa na Roho ya ujasiri wa ajabu na kufanya hata yale ambayo kwa uwezo wetu wa kibinadamu hubaki kuwa fumbo. Na hili linatokea kwa Nabii Ezekieli na kusema, Kisha Roho ikaniinua, ikanichukua mpaka ua wa ndani; na tazama, utukufu wa Bwana uliijaza nyumba,” Eze 43:5. Mungu akishasema ‘NDIYO’ kwa watu wake, mwanadamu kwa ‘HAPANA’ yake, atakesha bure. 

Wapendwa katika Kristo, tuelewe kwamba, Utukufu wa mfalme ni wingi wa watu wake; Bali uchache wa watu ni uharibifu wa mkuu wao,” Mit 14:28. Kunapo tokea utengano na wenye kusababishwa na wewe binafsi ambaye ulitakiwa kuwa alama ya umoja kama kiongozi au mzazi pale ulipo, hakika lazima ujiandae kwa uharibifu. Elewa kwamba dhamana na nafasi uliyo nayo kwa ajili ya watu na kwa watu, inaufunua Furaha ya Mungu, Uwepo wa Mungu, na Utukufu wa Mungu, endapo UTATUMIKA vyema, na siyo KUTUMIKIWA. Na huu ndio ujumbe wa Mungu kwa wana wa Israeli, na kwetu leo pia; Mwanadamu, hapa ni mahali pa kiti changu cha enzi, na mahali pa nyayo za miguu yangu, nitakapokaa kati ya wana wa Israeli milele; na nyumba ya Israeli hawatalinajisi jina langu takatifu tena, wao, wala wafalme wao, kwa mambo yao ya kikahaba, na kwa mizoga ya wafalme wao, katika mahali pao pa juu,” Eze 43:7. Hiki kiburi cha kuchukua nafasi ya Mungu tunakitoa wapi?

Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, Kama kikionekana katika njia ya haki,” Mit 16:31. Na pasipo haki hakuna amani hata kama nikifoka kwa nia njema kwa watu niliopewa dhamana kwao. Ukweli ni kwamba, Haifai kula asali nyingi mno; Vile vile mtu kutafuta utukufu wake mwenyewe si utukufu,” Mit 25:27. Siwezi kamwe kuutafuta utukufu wangu binafsi na kufika kileleni kwa kutumia migongo ya watu kama ngazi. Kwa kufanya hivi nafuta kabisa dhana ile ya KUTUMIKA na siyo KUTUMIKIWA. “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Lk 10:45.

Katika Injili yetu ya leo, Yesu anatoa angalizo kwa wanafunzi wake akisema wawe macho juu ya waandishi na mafarisayo kwa kujihesabia haki na kukaa katika kiti cha Musa. Wapendwa wana wa Mungu, Musa anawakilisha sheria. Mafarisayo na waandishi kukaa katika kitu cha Musa ni kuwa juu ya Sheria za Mungu. Wanajichukulia mamlaka yasiyo yao, na kuwabebesha watu mizigo mizito isiyo bebeka.

Ushauri wa Yesu kwetu kuhusu Mafarisayo na Waandishi, ni kutenda na kuishi wasemayo, ila kwa mfano wa matendo yao tusitende. Yesu Kristo anaona kasoro ya watu hawa na anawakemea kwa kusema, “ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie,” Mt 23:13. Wanausema na kuusifia utakatifu bila kuuishi.

Badala yake, Yesu anatutaka kufanya hili, “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8. Mwalimu wetu ni Yesu Kristo, na katika Yeye sote kwa kupitia Sakramenti ya Ubatizo tumerudishiwa urithi (Ufalime ule wa Mbinguni) wetu na kuwa wana wa Mungu. Kwa tukio hili la kupatanishwa na Mungu Baba kupitia Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo, sisi sote leo ni ndugu. Kwa upatanisho huo, Yesu Kristo anayo mamlaka ya kusamehe dhambi. “Lakini mpate kujua ya kwamba Mwana wa Adamu anayo amri duniani ya kusamehe dhambi, (amwambia yule mwenye kupooza) Ondoka, ujitwike kitanda chako, uende nyumbani kwako,” Mt 9:6

Ndugu yangu, nani aliye tabibu zaidi ya Bwana wetu Yesu Kristo? Ni kwa Yesu Kristo tunaweza kuponywa na kuwa huru tukiwa na haja hiyo. “Na makutano walipojua walimfuata; akawakaribisha, akawa akisema nao habari za ufalme wa Mungu, akawaponya wale wenye haja ya kuponywa,” Lk 9:11. Je, mwenzangu humuitaji Yesu? Kuponywa huku na Yesu ni matokeo ya kuziungama dhambi na kuomba uponyaji huo. Tendo hili linatupelekea kuwa na haja ya kuponywa. “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii,” Yak 5:16. Amina

Tumsifu Yesu Kristo!

Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu,” Mt 23:8


Tusali:-Ee Yesu, tujalie unyenyekevu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario