SIKUKUU YA KUPALIZWA MBINGUNI BIKIRA MARIA
Somo I: Ufu 11: 19, 12:1-6, 10
Zab: 45:9-11, 15
Somo II: 1Kor 15:20-26
Injili: Lk 1:39-56
Nukuu:
“Na ishara kuu
ilionekana mbinguni; mwanamke aliyevikwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu
yake, na juu ya kichwa chake taji ya nyota kumi na mbili,” Ufu 12:1
Na yule
joka akasimama mbele ya yule mwanamke aliye tayari kuzaa, ili azaapo, amle
mtoto wake,” Ufu 12:4b
“Naye akazaa mtoto
mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake
akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi,” Ufu 12:5
“Kwa kuwa kama katika
Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa,” 1Kor 15:22
“Maana sharti amiliki
yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake,” 1Kor 15:25
“Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto
kichanga kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu,” Lk 1:44
“Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama,
tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa,” Lk 1:48
“Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge
amewakweza,” Lk 1:52
TAFAKARI: “Utakatifu wetu ndiyo cheo chetu, na ndiyo makusudi ya
maisha ya umilele.”
Wapendwa wana na Mungu, leo Mama Kanisa anafanya sikukuu ya
kupalizwa mbinguni kwa Mama Bikira Maria. Tendo hili la kupalizwa mbingini kwa
Bikira Maria lina vielelezo vyote vya kimazingira na kimaandiko Matakatifu.
Kimazingira, kama mwanadamu Bikira Maria alijaliwa neema za Kimungu kushirika
kwa ukaribu na undani kabisa fumbo zima la wokovu wetu. Kama Mama na Mzazi,
Bikira Maria alikumbana na shuruba nyingi sana za malezi na mahangaiko makubwa
kumlea Mtoto Yesu ambaye alikuwa na uwezo mkubwa wa Kimungu, na hata kuwapita
wazazi wake. Hakika Bikira Maria alikuwa na mahangaiko makubwa sana katika
malezi ya mtoto huyu. Ni ukweli usiotia shaka kabisa, kwa malezi haya, na kwa
kushiriki fumbo hili la wokovu tangu kutungwa mimba kwa uwezo wa Roho
Mtakatifu, kuzaliwa kwa Yesu, Kukua kwa
Yesu, Mateso yake, kifo chake, na ufufuko wake, Bikira Maria alishiriki fumbo
hili la wokovu kikamilifu. Kwa kubeba ujauzito, Mama Bikira Maria
anashirikishwa utukufu wa Yesu katika ishara hii anaposalimiana na Elizabeth: “Maana sauti ya kuamkia
kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga kikaruka kwa shangwe ndani
ya tumbo langu,” Lk 1:44. Elizabeth anatoa ushuhuda huu. Siri kubwa ya
mafanikio ya Mama Bikira Maria na mastahili yake ya kupalizwa Mbinguni yapo
kwenye unyenyekevu wake. Hivyo Bikira Maria anatambua jambo hilo na kusema, “Kwa kuwa ameutazama
Unyonge wa mjakazi wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita
mbarikiwa,” Lk 1:48. Kujinyenyekeza ni jambo la msingi sana na hasa kwa
kufunuliwa siri za Mungu. Kujiachilia huku kwa Mama Bikira Maria kuliko kwa
chini kabisa, na kubebwa kwa unyenyekevu wake kunaonekana katika maneno haya: “Amewaangusha wakuu katika
viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52. Mama Bikira Maria
anatufundisha kuhoji na kusema maneno haya: “Je, mimi ni nani Bwana hata
kuyatenda haya yote ndani mwangu?”
Kwa mtazamo huo wa kimazingira Bikira Maria anachukua
nafasi ya mkombozi mwenza. Ni kwa mantiki hiyo hiyo ushindi wa msalaba ni
ushindi wa Bikira Maria pia. Furaha za ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo ni
furaha ya Bikira Maria pia. Kupaa kwa Bwana yetu Yesu Kristo mbinguni, hakuwezi
kumzuiya mwanaye kumshirikisha furaha hiyo Mama yake kupalizwa mbinguni mwili
na roho. Je, nani kama mama? Hali hii inatupa mtazamo wa kimazingira na
ushiriki wa Mama Bikira Maria katika fumbo hili la wokovu.
Kwa upande mwingine
Maandiko Matakatifu yanatupa ukweli wa siri hii ya ajabu juu ya
kupalizwa Mbinguni kwa Mama Bikira Maria. Kwa kuanguka kwa wazazi wetu wa
mwanzo, yaani Adam una Eva, Mungu hakuacha mpango wake wa kumkomboa mwanadamu.
Hivyo ujio wa Yesu Kristo ni kielelezo cha Adamu Mpya ambaye kwa kupitia kwake
mpango mzima wa wokovu wa mwanadamu unakamilika. Bikira Maria anachukua nafasi
ya Eva ambaye kwa kupitia kwake mpango wa kwanza wa kumkomboa mwanadamu
ulikwama. Hivyo kadiri ya maandiko matakatifu, Bikira mara ndiye atakayemzaa
mtoto wa Kiume, yaani Yesu na kuendeleza mpango wa Mungu. Hivyo, “Naye akazaa mtoto mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote
kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti
chake cha enzi,” Ufu 12:5.
Mama huyu
alikuwa ndani ya mpango wa Mungu tangu mwanzo. Bikira Maria alishakwisha vikwa
taji la ushindi, hivyo ilikuwa ni jambo la wakati tu utakapotia na historia
ichukue nafasi yake. Hakuna lisilowezekana kwa Mungu. “Na ishara kuu
ilionekana mbinguni; mwanamke aliyevikwa jua, na mwezi ulikuwa chini ya miguu
yake, na juu ya kichwa chake taji ya nyota kumi na mbili,” Ufu 12:1. Hata
pamoja na ishara hii, Mama huyu anaonyeshwa ni kwa namna gani atashiriki
mahangaiko ya mtoto wake atakaye mzaa. Maandiko Matakatifu yanachukua Ishara ya
Joka, ambalo lipo ili kuzuia uhai wa mtoto huyu. Na yule joka akasimama mbele
ya yule mwanamke aliye tayari kuzaa, ili azaapo, amle mtoto wake,” Ufu 12:4b. Uwepo wa Joka hili, twaweza kuufananisha na uovu
uliokuwa umemzunguka Yesu, yaani dhambi, na hivyo Yesu itampasa kufa ili
kumshinda adui wa mwisho yaani mauti. “Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake
wote chini ya miguu yake. Adui wa
mwisho atakayebatilishwa ni mauti,” 1Kor 15:26
Ukweli ni kwama kadiri ya maandiko
Matakatifu, na kwa kupitia Adamu, wote walikufa, na kwa kupita Yesu wote
watahuishwa. Hivyo uzima wa kweli tunaupata kupitia Kristo, na kifo kinabakia
tu kama mlango wa kwenda sehemu ya pili yaani uzima wa milele. “Kwa kuwa kama katika Adamu wote
wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa,” 1Kor 15:22. Tunahuishwa
kwa fumbo zima la kifo na ufufuko wake Yesu Kristo. Mastahili haya hayatokani
na historia zetu, yaani, familia tulizotoka, koo tulizotoka, wala kabila, wala
taifa, bali ni uhaminifu wetu juu ya Kristo na utakatifu wetu ambao ndiyo cheo
chetu.
Hivyo
hapana shaka yoyote kwamba Bikira Maria kupalizwa Mbinguni. Kama alishiriki
mahangaiko na mwanaye ndiyo hivyo hivyo Bikira Maria ilimpasa kushiriki Furaha
na Utukufu pamoja na mwanaye. Hiyo ndiyo zawadi kubwa na asante ya Yesu kwa
Mama yake. Hakika hatuwezi kulipa waliyotutendea wazazi wetu, na hasa Mama
Mzazi.
Kijana
Felix aliyemaliza masomo yake ya udaktari alibahatika kumwoa mwanamke mwenye
elimu kama yake. Mwanamke huyu alijipenda sana kupita kiasi kutokana na
mazingira ya makuzi yake. Ni kweli alitoka familia yenye pesa na tajiri sana.
Felix
alitoka familia masikini sana, na soma yake ilikuwa ya shida sana. Felix
alifika hapa alipo kwa kutegemea biashara ndogo ndogo za mama yake mzazi. Baba
yake Felix alifariki muda mrefu, Felix angali darasa la pili.
Akiwa
ameajiriwa na kuwa na mji wake, mama yake mzazi alipenda kumtembelea mtoto
wake. Kwa bahati mbaya au nzuri Mama yake Felix alifika na kumkuta mke wa mtoto
wake. Kwa namna alivyokuwa mama yake Felix, mke wa Felix alikuwa na mashaka
naye kwani alionekana kama ombaomba fulani hivi. Hata kwa kujitambulisha kote
kule mke wa felix hakuweza kumpokea vizuri na kulazimika kumwifadhi moja ya
vyumba vya stoo.
Alipofika
Felix kutoka kazini mkewe alimwambia ujio wa mwanamke mmoja mchafu na waajabu
kutokea, na kusema, “eti mama huyo hapa stoo anasema kuwa wewe ni mwanaye.”
Felix kwa aibu naye hakumpokea vizuri mama yake, na ndipo ugomvi ulipoanzia.
“Kama unasema kuwa wewe ni mama yangu piga mahesabu ya gharama zote
ulizonitunza na kunilea nami nitakulipa,” Felix alimwambia mama yake kwa
hasiri.
“Naombeni
munionyeshe uhani nami nikirudi nitakupa hesabu yangu,” mama yake Felix mjibu
Felix. Baada ya muda kidogo mama yake Felix alirudi akiwa amejipaka kinyesi
chake mwili mzima na kumwambia Felix, “haya naomba uniogeshe na hii ndiyo
gharama yangu kwa siku moja tu katika utoto wako. Kutokana na harufu ile, Felix
hakuweza hata kumsogelea Mama yake. Je, Yesu angemlipa nini Mama yake kwa
mahangaiko aliyoyapata hadi chini ya msalaba alipokata roho? Yesu anamkabidhi
mama yake Kanisa na kusema, “Mama tazama mwanao.”
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Amewaangusha wakuu katika
viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza,” Lk 1:52
Tusali:-
Ee Yesu, asante kwa kutupa Mama yako mpenzi na mama yetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario