lunes, 8 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 19 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 19 YA MWAKA-C
Somo: Eze 2:8-3:4
Zab: 119:14, 24, 72, 103, 111, 131
Injili: Mt 18:1-5, 10, 12-14
Nukuu
Bali wewe, mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe wewe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi; funua kinywa chako, ule nikupacho,” Eze 2:8 

Akalikunjua mbele yangu; nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!” Eze 2:10

Akaniambia, Mwanadamu, kula uonacho; kula gombo hili, kisha enenda ukaseme na wana wa Israeli,” Eze 3:1

 “Akaniambia, Mwanadamu, lisha tumbo lako, ulijaze tumbo lako kwa hili gombo nikupalo. Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali,” Eze 3:3

 “akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 18:3 

Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni,” Mt 18:4

 “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:10

TAFAKARI: “Kuifahamu siri ya Mungu na kutumika vyema kama chombo chake, yanipasa kujiadabisha na kujinyenyekeza.”

Wapendwa wana wa Mungu, ili tuzame vizuri katika tafakari yetu ya leo, na hasa somo letu la kwanza ni vyema tungeanza na mstari ule wa nne. Ni dhahiri leo tunahitaji viongozi kama Nabii Ezekieli aliyesimama na kusema kweli bila kupepesa macho. Mungu anasimamia haki za wanyonge wake kwa kuwatumia watu wenye hofu ya Mungu kama Nabii Ezekieli na kusema: Na wana hao wana nyuso zisizo na haya, na mioyo yao ni migumu. Mimi nakutuma kwa hao; nawe utawaambia, Bwana MUNGU asema hivi. Nao, kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia, (maana ndio nyumba ya kuasi hao), hata hivyo watajua ya kuwa nabii amekuwako miongoni mwao,” Eze 2:4-5

Siri ya hofu ya Munga aliye nayo Nabii Ezekieli ni tokeo la kulisikia neno la Mungu, kulipokea, kulitafakari, kulishirikisha, na mwisho akawa shahidi na shuhuda na neno hili, Eze 2:8; 3:1-3. Na hivi ndivyo Nabii Ezekieli alivyolisikia neno na kulipokea, Bali wewe, mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe wewe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi; funua kinywa chako, ule nikupacho,” Eze 2:8. Ili kulishirikisha neno lile la Mungu katika kufundisha na kuonya, ilimpasa kulitafakari neno hilo la Mungu kwa kina. Neno hili ambalo kwalo lipo kwenye gombo la chuo, Ezekieli anaamuriwa kulila. Kulila neno la Mungu ni kuzama ndani ya neno hilo na kuwa sehemu yake, kama vile tunavyonawiri kwa kula lishe bora.

Ni ndani ya neno tunafunuliwa mengi yaliyojificha. Ezekieli akalikunjua mbele yangu; nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!” Eze 2:10. Na hivi ndivyo Mungu alivyo mwamuru na kumwambia, Mwanadamu, kula uonacho; kula gombo hili, kisha enenda ukaseme na wana wa Israeli,” Eze 3:1. Ni pale tunaposhibishwa vizuri na neno la Mungu ndani yetu, Eze 3:2-3a, ndivyo hivyo tunakuwa imara kulishirikisha neno hili katika kulifundisha na kuonya.

Tushibishwapo vizuri na neno la Mungu, neno lile huwa na matokeo mawili. Kwanza kabisa neno linatupa furaha, katika maana ya utamu wa neno. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwa nabii Ezekieli. “Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali,” Eze 3:3b. Na pili, neno la Mungu linatupa utayari katika maana ya kulishirikisha neno la Mungu bila woga. Naye Mungu akamwambia Ezekieli, Mwanadamu, haya! Waendee wana wa Israeli ukawaambie maneno yangu,” Eze 3:4. Kuifikia hatua hii kwahitaji kujiadabisha kunakoendana na kujinyenyekeza. Wapo viongozi wengi wenye maona mazuri ila pale wanapokosa tunu hii ya ‘kujiadabisha na kujinyenyekeza,’ yote waliyo nayo husambaratika.

Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna mwanadamu aliyekamilika. Kila mmoja wetu, na hata viongozi wetu tulio nao wanamadhaifu yao kama wanadamu. Tatizo kubwa tulilonalo ni pale tunapohalalisha udhaifu wetu, na kuwasadikisha wale waliotuweka madarakani kuwa huo ndio mtindo wa maisha. Ni vyema tunapotambua udhaifu wetu iwe dawa ya kujirekebisha na kufanya vizuri zaidi. Hii ndiyo sifa mojawapo ya kiongozi, yaani “kujisahihisha.” Na hii ndiyo tunu ya kujiadabisha. Kiongozi asiyejisahihisha au kujiadabisha, ni hatari sana kwa wale anaowaongoza. Kama viongozi, katika shughuli zetu si kila mara mambo yatakwenda vema. Tunaweza kukosea hapa na pale. Basi tuwe tayari kusahihishwa na kujisahihisha. Tujisahihishe kweli. Tunajifunza kutoka makosa yetu na ya wenzetu. Zaidi ya hayo tusiyaache makosa yatokee kwa makusudi. Tujitahidi kuzuia makosa na mapungufu mengine yoyote yasitokee. Tulenge kwenye ukamilifu ingawa  udhaifu upo.

Udhaifu wenye mwono wa kujisahihisha na kusimama katika kweli, ndiyo Mtume Paulo anauzungumzia kama “Mwiba.” Mtume Paulo anamwomba Mungu mara tatu amwondolee mwiba huu.  Baada ya kulifahamu tatizo lake, Mtume Paulo anatumia tatizo hilo kujiimarisha zaidi katika kweli. Jibu la tatizo lake ni UNYENYEKEVU katika kutenda. Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi,” 2Kor 12:7. Ndugu yangu, je, unaliona jambo hili ndani yako, na kwa viongozi tulionao sasa? Tuposhindwa kufanya maamuzi yenye tija na hasa kuanzia kwako na kwangu, baada ya miaka 50 au 100 ijayo, watu wote wa Taifa hili la Tanzania tutakuwa watumwa katika nchi yetu wenyewe. Neema na baraka alizotujalia Mungu zitakuwa sababu ya mateso yetu yasiyokuwa na kikomo.

Wapendwa wana wa Mungu, mnyenyekevu husimamia haki katika kweli kwa sababu msingi wa fadhila zote ni unyenyekevu. Mnyenyekevu hawezi kudongoka katika laana ya uovu wo wote. Laana ya Bwana i katika nyumba ya waovu, Bali huibariki maskani ya mwenye haki. Hakika yake huwadharau wenye dharau, Bali huwapa wanyenyekevu neema,” Mit 3:33-34. Unyenyekevu hutujengea nidhamu ya hali ya juu. Unyenyekevu utupelekea kupokeana kama tulivyo na kusaidiana kufikia malengo tarajiwa kwa kila mmoja wetu. Unyenyekevu utufikirisha kabla ya kutenda jambo lo lote katika maisha. Unyenyekevu hutufanya kuwa watii na wapole hata pale mantiki ya ufahamu wetu inaposhindwa kukubaliana na ukweli kama ulivyo hasa katika joto la ujana wetu. Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema,” 1Pet 5:5. Unyenyekevu wa mtu ni ukweli wa Mungu ndani ya mtu huyo.

Wapendwa wana wa Mungu, ni katika mtizamo huu tunaweza kuona pale ambapo hapana unyenyekevu binadamu alijifanyia yake, na Mungu alijiweka pembeni. Kiburi cha mwanadamu ni chukizo kubwa sana kwa Mungu. Kuishi katika kiburi siyo makusudio ya uumbaji wetu. Wana wa Israeli wanatambua tatizo hili na kwa vinywa vyao wanasema,  “Tumemwasi, wala hatukuitii sauti ya Bwana Mungu wetu, kwenda katika sheria zake alizoziweka mbele yetu. Bali tulikwenda kila mtu katika mawazo ya moyo wake mbaya, kutumikia miungu ya kigeni na kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana Mungu wetu,” Bar 1: 18, 22. Hakuna neema na baraka pale tunapotawaliwa na kiburi. Mwenye kiburi ni vigumu sana kujipokea na kuupokea ukweli ambao hauendani na mfumo mzima wa kufikiri kwake.

Katika Injili ya leo, Yesu anamfananisha mtu mwenye unyenyekevu kama mtoto. Mtoto mdogo hana cha kujikuza zaidi ya kuyaona yote na katika yote kwa wazazi wake. Mtoto huweka uaminifu mkubwa sana kwa wazazi wake. Wazazi wake huwa kila kitu kwake. Ni katika mtazamo huu Mungu wetu ni kila kitu kwetu. Hatuna cha kujikweza mbele zake “kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu,” 1Kor 1:25. Ni katika ukweli huu Yesu anawaambia wanafunzi wake maneno haya mazito, akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni,” Mt 18:3. Tusipojivua kujua kwetu kusikokuwa na maana yo yote zaidi ya mbwembe zetu, hatutaweza kufunuliwa siri za mbinguni.

Unyenyekevu wenye mfano wa utoto ndio huo unaotufanya wakubwa mbele ya uso wa Mungu. Ukubwa huo siyo ule wa kufanya tutakayo sisi na kuzirithisha nafsi zetu, bali kuyafanya yote kadiri ya mpango wa Mungu. Kuujua mpango wa Mungu ni pale tu unapokuwa tayari kujinyenyekeza mbele zake. Hivyo, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni,” Mt 18:4. Katika ufalme huu wa mbinguni hakuna maguvu ya kutalawa au kutawaliwa, bali nguvu ya UPENDO wa kweli.

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, wanyenyekevu wana sauti kubwa sana mbele za Mungu. Mtu ye yote anayemdharau mtu mnyenyekevu kwa vile anayafanya yote hayo kwa kujishusha yu na hatia kubwa sana mbele za Mungu. Yesu anatuambia,  Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:10. Hivyo tujiadhari sana na jeuri yetu ya pesa, madaraka, umaarufu na kutambulika kwetu katika jamii, na kutumia hali hizo kama fimbo ya kuchapa wengine. Haya yote mwisho wa siku hayana msaada wo wote katika umilele wako. “Vivyo hivyo haipendezi mbele za Baba yenu aliye mbinguni kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee,” Mt 18:14. Hivyo basi, kwa utajiri nilio nao, kwa madaraka niliyo nayo, kwa umaarufu nilio nao, na kwa kutambulika kwangu katika jamii, iwe sababu na nguvu ya kuwa sauti ya wasio na sauti.

Tumsifu Yesu Kristo!

Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 18:10


Tusali:-Ee Bwana tujalie fadhila ya unyenyekevu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario