lunes, 22 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 21 YA MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 21 YA MWAKA-C
Somo: 2The 2:1-3a, 14-17
Zab/Kit: 96:10, 11-12a, 12b-13
Injili: Mt 23:23-26
Nukuu
Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; aliyowaitia ninyi kwa injili yetu, ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo,” 2The 2:3a,4

Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa, ama kwa maneno, ama kwa waraka wetu,” 2The 2.15 

Na Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema,” 2The 2:16-17

 “Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia,” Mt 23:24 

Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi,” Mt 23:25 

Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi,” Mt 23:26

TAFAKARI:Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia,” Mt 23:24

Wapendwa wana wa Mungu, tulitafakari neno hili kwa undani, “Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia,” Mt 23:24. Bwana wetu Yesu Kristo alikuja ulimwenguni huku siyo tu kumkomboa mwanadamu kiroho, bali pia kimwili ikiwa ni pamoja na maisha ya mwanadamu huyu katika ujumla wake. Ndiyo maana Yesu hakuacha kukemea mila na desturi potofu, Yoh 9:1-25, ukadamizaji kisiasa na kimifumo, Lk 20:21-26, kidini, Yoh 4:4-30, na hata kiuchumi, Mt 17:24-27. Tunapo tafakari maeneo hayo tajwa, na mengine mengi katika Maandiko Matakatifu tunagundua ‘misioni’ ya Yesu hapa dunia ilikuwa kukuweka wewe na mimi huru mwili na roho, na katika kweli na haki. Na hivi ndivyo Yesu asemavyo, “Basi mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli,” Yoh 8:36

Yesu aliyaisha maisha ya kawaida ya watu wa nyakati zake, alisafiri nao katika shida na raha zao, alionja uchungu wao, na alitokwa machozi pamoja nao, Yoh 11:1-43. Yesu katika hali na mazingira haya alikuwa kweli Mwanadamu. Hapa pamoja na kulia na wanadamu, hakubaki katika hali ile ya kibinadamu tu, bali alionyesha Umungu wake, Yoh 11:44-45. Hakika Yesu anatupa mfano mzuri wa kiongozi. Kwa vile aliishi kama kiongozi wa kweli, mwenye uchungu na dhamana kubwa wa wale aliowajia, Yesu hakusita kukemea uovu aliouona kwa viongozi wa nyakati zake. Naye anasema,Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia,” Mt 23:24. Viongozi hawa walikosa sifa zifuatazo, yaani, hawakuwa nuru, hawakuwa wasimamizi na watetezi wa kweli na haki, na hawakuwa tumaini pale watu walipokoswa tumaini.

Kiongozi ni nuru kwa sababu uwaongoza watu kutoka kwenye giza, yaani, uovu ili waufikie mwanga wanaoutamani, yaani kweli, haki, tumaini na upendo. Hivyo ni sikitiko kubwa sana kwa wanaoongozwa kuona kiongozi wao kuwa sababu ya maumivu yao na mchochea uovu. Watu ukosa mwelekeo na maisha ukosa maana. Kiongozi ni msimamizi na mtetezi wa haki katika mizania ya kweli na haki. Hivyo ‘kuchuja mbu na kumeza ngamia’ kulimaanisha na kunamaanisha kutokuwa na mizania ya kweli na haki katika kutoa HAKI. Si jambo la kushangaza kuona mwizi wa kuku kufungwa gerezani, na wakwapuaji wa rasilimali za Taifa kuendelea kula raha mtaani. Licha ya kwamba wote, yaani, mwizi wa kuku na mkwapuaji wa rasilimali za Taifa wanamakosa, mizania ya kweli na haki kwa mujibu wa sheria ichukue mkondo wake. Naye Yesu anasema, Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache,” Mt 23:23. Kama tumejiwekea utaratibu kwa nini hatuufwati na mara nyingine wengine kwa madaraka yao wanakuwa juu ya ‘utaratibu?’ Hili Yesu aliliona na hakuacha kulikemea.

Jambo linguine Yesu alilolikea ni tabia ile ya kufanya mambo ili kuonekana na watu kuwa unafanya jambo fulani kumbe katika uhalisia wa jambo hilo unachofanya ni ‘maigizo’ matupu. Unafiki ni saratani mbaya sana hasa pale tunapo dhamiria  kwa dhati kubadilika na kusonga mbele. Yesu analikemea hili na kusema,  “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi,” Mt 23:25. Tusifanye vitu kama zima moto! Kama utumeamua kufanya vita dhidi ya ufisadi iwe vita kweli na siyo kufanya mlinganisho wa uovu. Jambo la ajabu ni kwamba uovu ule unaotuhusu na wakati mwingine kushiriki moja kwa moja tunaufumbia macho. Huku ndiko kusafisha kikombe kwa nje na kuacha uchafu ndani. Yesu anatoa maelekezo ya namna ya kufanya na kusema,  Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi,” Mt 23:26.

Kiongozi licha ya kuwa tumaini kwa watu, kiongozi ni mwonyesha tumaini hasa pale tumaini hilo linapotoweka. Na katika hali na mazingira haya ya kutoweka kwa tumaini Mtume Paulo anasema, msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno,” 2The 2:2a. Ndugu yangu, hapa pale tunapoona kusalitiwa kwa wale tulio waamini tusiiache kweli na haki, na kusimama imara katika kweli na haki hiyo. Hivyo, “Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; aliyowaitia ninyi kwa injili yetu, ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo,” 2The 2:3a, 4. Matumaini yetu tuyaweke kwa yule atutiaye nguvu, Flp 4:13. Kila mtu kadiri ya imani yake ayashike maadili yaliyo mema na kuupinga uovu kwa nguvu zake zote. Na hivi ndivyo Mtume Paulo anavyowafunda Wakristo wenzake na kusema, Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa, ama kwa maneno, ama kwa waraka wetu,” 2The 2.15. Na tumaini letu katika nyakati hizi za sintofahamu ndilo hili; Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema,” 2The 2:16-17. Hakuna lisilowezekana kwa Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi,” Mt 23:26


Tusali:-Ee Yesu tuongoze daima katika kweli na haki. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario