IJUMAA
WIKI YA 20 YA MWAKA-C
Somo: Eze 37:1-14
Zab/Kit: 107:2-3, 4-5, 6-7, 8-9
Injili: Mt 22:34-40
Nukuu
“Bwana
MUNGU aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi
mtaishi,” Eze 37:5
“Basi tabiri, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama,
nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu
wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli,” Eze 37:12
“Mmoja wao,
mwana-sheria, akamwuliza, akimjaribu; Mwalimu,
katika torati ni amri ipi iliyo kuu?” Mt
22:35-36
“Akamwambia,
Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili
zako zote. Hii ndiyo amri iliyo
kuu, tena ni ya kwanza,” Mt 22:37-38
“Na
ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea
torati yote na manabii,” Mt 22:39-40
TAFAKARI:
“Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu.
Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi.”
Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na maendeleo aliyoyafikia mwanadamu
leo, ikiwa ni pamoja na kuishi kwa kujiwekea vilinda uhai wake, “life securities,”
hata hivyo uhakika huo bila Mungu ni sawa na kutwanga maji katika kinu. “Kwa
sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa
nafsi yake. Kwa maana kama
tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama
tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:7-8. Ndugu yangu, pamoja na
mipango yako ya muda mfupi na mrefu uliyojiwekea, kati yetu hakuna ajuaye ni
kitu gani kitakachomtokea sekunde chachetu tu zijazo. Je, tusifanye chochote
kwa kuwa huu ndio ukweli? Hapana! Tuyafanye na kuyapanga yote katika usahihi
wake, na tufanye hivyo kwa kumshirikisha Mungu kwa kila jambo.
Mara nyingi penye
mafanikio-‘kibinadamu,’ wengi wetu hitaji na uwepo wa Mungu huwa hitaji la
nyongeza. Tunaamini yote huenda sawa bila Yeye (Mungu) kuwepo. Hiki ndicho
kiburi kikubwa sana cha mwanadamu asiye na hofu ya Mungu ndani yake. Hali na
mazingira haya yanawakuta wana wa Israeli nyakati zile za Nabii Ezekieli. Mungu anawafananisha waasi hawa wa imani kama
mifupa isiyokuwa na nyama. Na hivi ndivyo wana hawa wa Israeli
walivyofananishwa na Mungu (mifupa isiyo na nyama wala uhai) katika swala zima
la imani. “Mifupa hii ni nyumba yote ya
Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea;
tumekatiliwa mbali kabisa,” Eze 37:11. Bila mkono wa Mungu tuyafanyayo hata kama yatavuma
sana hayatakuwa na mwisho mzuri. Na hivi ndivyo Nabii Ezekieli alivyozamishwa
na Mungu katika tafakari nzito na chukuliwa nje katika roho ya Bwana.
Hata
katika hali hii ya uasi na kukosa dira katika imani, Mungu hapendi hata mmoja
wetu apotee. Yeye ndiye uhai na uzima kwa kila kipumuacho, na Yeye huweza
kubadili tabia na mienendo ya vyote alivyoviumba. “Bwana
huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye
hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7. Mungu akiwa ndiye
yote na katika yote, kwa upendo na huruma wake, “humwinua mnyonge kutoka
mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi
kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka
ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:8. Tunapomrudia Mungu katika toba na majuto ya
kweli, Mungu huyabadili maisha yetu na kutufanya wapya mbele za macho yake. Na
hivi ndivyo alivyoitoa ahadi yake kwa wana wa Israeli na kusema, “Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha
kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi
ya Israeli,” Eze 37:12. Naye Mungu asema hivi juu ya mifupa ile ikiwa ni
pamoja na hali nzima ya udhaifu wako na wangu kwamba, “Tazama,
nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi,” Eze 37:5. Hakuna jambo la kumshinda
Mungu kwa sababu namna tulivyo, na vyote tulivyonavyo vyaonyesha Furaha ya
Mungu, na kuufunua Utukufu wake.
Ni kwa
matiki hii Mzaburi anasema, “usiogope mtu
atakapopata utajiri, Na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua cho
chote; Utukufu wake hautashuka ukimfuata,” Zab 49:16-17. Ukweli ni kwamba
hatukatazwi kuwa matajiri, bali utajiri huo usiwe mwisho wa kila kitu katika
maisha yako. Utajiri wako ukuweke karibu na Mungu na jirani yako. Na hii ndiyo
maana ya amri ya mapendo, “Mpende
Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako
zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu,
tena ni ya kwanza,” Mt 22:37-38. Ulifanyalo hilo yaani, kumpenda Mungu kwa
moyo, roho, na akili zako zote, yakupasa kufaulu mtihani wake, yaani, ukaribu
wako na jirani yako, na hasa katika uhitaji wake. Hivyo, “Na
ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea
torati yote na manabii,” Mt 22:39-40. Je, utajiri wako ikiwa ni pamoja na uwe
wa kushikika au karama na vipaji ulivyopewa na Mungu, vinakuweka karibu naye
(Mungu) na jirani yako? Kama hakuna ukaribu huo, ndugu yangu utajiri huo ulio
nao ni balaa kwako.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Nanyi
mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa
ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu,” Eze 37:13
No hay comentarios:
Publicar un comentario