jueves, 25 de agosto de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 21 YA MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 21 YA MWAKA-C
Somo: 1Kor 1:17-25
Zab/Kit: 33:1-2, 4-5, 10ab, 11
Injili: Mt 25:1-13
Nukuu
 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu,” 1Kor 1:18

 “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu?” 1Kor 1:20

 “Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu,” 1Kor 1:25

Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi,” Mt 25:1 

Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara,” Mt 25:2 

 “Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi,” Mt 25:12 

Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa,” Mt 25:13 

TAFAKARI:Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu.”

Wapendwa wana Mungu, pamoja na ukweli kwamba maisha ni jukumu la muda mfupi, twahitaji hekima ya kutosha kuendana na jukumu hilo la muda Mfupi, yaani, maisha. Hekima hiyo iniongoze kutambua bila shaka kwamba niliukuta ulimwengu huu, na nitauacha siku moja ulimwengu huu. Hivyo nielewe ninao wajibu licha wa muda mfupi kuufanya ulimwengu huu mahali salama pa kuishi, na paendelee kuwa hivyo hata nitakapo ondoka katika ulimwengu huu. Kwa mantiki hiyo, mimi na wewe tuwe daima vyombo vya amani, na habari njema. Ingawa tunayo mengi ya kufanya, hili la kuwa ‘chombo cha amani na habari njema’ liongoze na kutafsiri yale yote tuyafanyayo. Na tusema daima kama Mtume Paulo, Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika,” 1Kor 1:17. Msalaba wa Kristo ndiyo kielelezo halisi (mti) ambacho wokovu wetu ulitundikwa juu yake.

Ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, niutazamapo Msalaba Mtakatifu na kuyatafakari matendo makuu ya Mungu na upendo wake kwetu, ni uweke mbali ubinafsi wangu, kiburi changu, na kujigamba kwangu. Msalaba uwe fahari yangu daima. Niseme na kuyaishi maneno hayo mazito kama asemavyo Mtume Paulo kwamba, Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu,” Gal 6:14. Lakini jambo la ajabu leo na kusikitisha ni kwamba, baadhi yetu na hasa waliopewa mamlaka na ummaa kwa kuutanguliza ubinafsi wao mbele, kiburi chao, kujigamba kwao na kwa kuusaka umaarufu pasipo sifa na siha, wapo tayari kuliingiza taifa hili katika machafuko. Hata hivyo wengi tunapigwa mshangao na kujiuliza swali hili kama afanyavyo Mtume Paulo; Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu?” 1Kor 1:20. Je, twataka yatokee ndipo tuanze vikao vya usuluhishi? Ni kweli kwamba jamii yetu leo haina tena wazee wenye hekima kama waleta hoja wa zamani, yaani, Baba Yetu wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na wenzake wa nyakati zake? Hakika tukiliruhusu hili tuwe tayari kuja kuhukumiwa na historia tunayoitengeneza sasa kwa mbwembwe kubwa.

Wenye hofu ya Mungu na wenye kuuthamini Msalaba Mtakatifu ambao wokovu wetu ulitundikwa juu yake, kwao Msalaba ni nguvu ya Mungu, IKor 1:18b. Ila kwa wanao potea kwa sababu ya kiburi, majigambo, umaarufu pasipo sifa na siha, Msalaba kwao utabaki kuwa ni upuzi, IKor 1:18a. Na hivi ndivyo asemavyo Mtume Paulo, Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu,” 1Kor 1:18. Tunahitaji hekima nyakati hizi kuliko zote, kwa sababu shetani katukalia kooni na macho yetu hayaoni tena uhalisi wa kitu kama kilivyo, bali twauona uhalisi wa kitu kama tulivyo katika ubinafsi wetu, majigambo yetu, na umaarufu wetu pasipo sifa na siha. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa,” 1Kor 1:19. Leo wenye hekima na akili, na hata waliokwisha kuwa wahudumu kwa nafasi mbalimbali katika taifa hili wameipiga kisogo hekima na akili yao.

Tumebaki kuisikia miluzi mingi na hata kuipiga miluzi hiyo ilhali hatujui kwamba kwa kufanya hivyo ndivyo tunavyozidi kumchanganya mbwa awindaye. Hapa ndipo Mungu anaporuhusu hekima ya dunia kuwa upumbavu, 1Kor 1:20. Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu?” 1Kor 1:20d. Leo tunajiuliza pia kwa kina, ‘Yu wapi Mwandishi wa kweli, kwenye kuiona kweli, na kuandika kweli?’ 1Kor 1:20b. Wengi wao wameyasaliti maadili yao na fani yao, na kuamua kulitumikia tumbo lisiloridhika hata lingelishwa vizuri kila siku. Hata hivyo tusilipoteze tumaini la Mungu na la kweli ndani yetu licha ya sintofahamu hizi za leo na sasa.Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa,” 1Kor 1:21. Tukilipoteza tumaini, maisha hukosa maana. Na maisha yakikosa maana, binadamu huwa hatari sana, kwani husukumwa kufanya chochote kibaya. Je, tunataka ishara zaidi kwa haya tunayoyaona leo na sasa ndiyo tuamini kesho yetu itakuwa mbaya? La hasha!

Ndugu yangu, Mtume Paulo anatuambia hivi, Wayahudi walitaka ishara, na Wayunani walitafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu,’ 1Kor 1:22-24. Na tunachohubiri kama wana wa Mungu na warithi wa ufalme wa Mungu si VITA, bali UPENDO. Na tunapo hubiri huu UPENDO tusisahau kwamba AMANI ni tunda la HAKI. Pasipo haki amani hutoweka hata kama tutaishikilia kwa makombora. Amani licha ya kuonekana kuwa ni hali ya utulivu kwa nje, yaani, kimazingira, ni tokeo la utulivu wa ndani wa kila mmoja wetu; awe mwenye hekima na akili, mjinga, masikini au tajiri. Hivyo amani siyo kitu cha kubeza hata kidogo kama milango ya HAKI itafungwa kwa kofuli la CHUMA. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu,” 1Kor 1:25

Wapendwa wana wa Mungu, Injili ya leo inatutaka tutafakari zaidi kuhusu hekima na busara tuitumiayo ilhali tukiwa duniani hapa kwa muda huo mfupi. Ni kweli kwamba maandalizi ya kuishi ufalme huo wa mbinguni yanaanza hapa hapa dunia kama sehemu muhimu ya kujiandaa. Naye Yesu anatoa mfanano wa ufalme huo wa mbinguni na kusema, Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi,” Mt 25:1. Kundi hili la wanawali kumi ndilo lenye mgawanyiko wa wapumbavu na wenye busara-hekima. Naam, Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara,” Mt 25:2. Hapa tunakumbushwa kutumia vyema karama na vipaji vyetu ili siku ya mwisho tujinyakulie ile taji, yaani UTAKATIFU ambao ndiyo cheo chako kikubwa kuliko vyote.

Kutotumia vyema vipaji vyako na badala yake kuishi kwa kuiga vya wengine ni kuwa kundi lile la wapumbavu waliozima taa zao, na kutokubeba mafuta pamoja nao. Na hii ndiyo maana ya maneno haya kwamba, Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao,” Mt 25:3-4. Ndugu yangu, bila cheo hicho, yaani utakatifu wako, hutoweza kumwona Mungu aliye Mtakatifu. Na kukifikia cheo hiki huna budi kuvitumia vyema jipaji na karama zako vizuri ungali hapa duniani kama sehemu pekee ya kujiandaa. Vipaji hivyo ulivyojaliwa na Mungu ni kwa kufaidiana.

Huo ndio ufunuo wa Roho ndani yake. Hivyo, “kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana,” 1Kor 12:7. Ingawa ni vipaji vyako, ila siyo mali yako. Si mali yako kwa sababu umejaliwa na Mungu kwa ajili ya wengine pia. Na Mungu ndiye mmiliki nawe upeazimwa kwa muda tu. Usisubiri hadi mwisho wa siku ndio uanze kuangaika navyo wakati kengele inakaribia kugogwa-mwisho wa maisha yako hapa duniani. Na hivi ndivyo ilivyokuwa, Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki,” Mt 25:6. Hapa ndipo wale wapumbavu wanagundua hawakuwa na mafuta katika taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika,” Mt 25:8. Hakuna hofu kwa wale wanao kutumika na kutumia vipaji vyao vyema, huku wakiuweka ubinafsi wao pembeni, majigambo yao, na umaarufu wao usio na sifa na siha.

Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwamba, wale wenye busara wakawajibu (wapumbavu), wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie,” Mt 25:9. Katika hali na mazingira haya ya kuchelewa, kukurupuka kwako hakutakusaidia sana. Hapa tunakumbushwa kutumia vyema rasilimali muda, na kuwa macho muda wote kwa yale tuyafanyayo na tuyatarajiayo. Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa,” Mt 25:10. Maisha ya ‘mwendo kasi’ bila umakini huu wa kutumia vizuri rasilimali muda, na umakini kwa yale tuyafanyayo na matarajio yake, matokeo yake ni kilio na kusaga meno. Ni wazi hapatakuwa na nafasi ya kujitetea. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwamba, wakaja na wale wanawali wengine (wapumbavu), wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie,” Mt 25:11. Kilio hiki hakitasaidia kwa sababu tumetumia muda wetu vibaya. Bila shaka tutajibiwa hivi na Mungu, nawaambia, siwajui ninyi,” Mt 25:12. Kumbe Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa,” Mt 25:13. Amina.

Tumsifu Yesu Kristo!

Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa,” Mt 25:13


Tusali:-Ee Yesu, tujalie utulivu wa ndani. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario