JUMATATU WIKI YA 18 YA MWAKA-C
Somo:
Yer 28:1-17
Zab: 119:29, 43, 79, 80, 95, 102
Injili:
Mt 14:13-21
Nukuu:
“Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya
makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya Bwana, naam, nabii Yeremia akasema, Amina,
Bwana na atende hivi; Bwana ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa
vyombo vya nyumba ya Bwana na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hata mahali
hapa,” Yer 28:5-6
“Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, Sikia sasa, Ee
Hanania; Bwana hakukutuma; lakini unawatumainisha watu hawa maneno ya uongo,”
Yer 28:15
“Basi
Bwana asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka
huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya Bwana,” Yer 28:16
“Basi
nabii Hanania akafa, mwaka uo huo, mwezi wa saba,” Yer 28:17
“Naye
Yesu aliposikia; hayo, aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo
watu, faraghani. Na makutano waliposikia, walimfuata kwa miguu kutoka mijini
mwao,” Mt 14:13
“Yesu
akatoka, akaona mkutano mkuu, akawahurumia, akawaponya wagonjwa wao,” Mt 14:14
“Yesu
akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16
TAFAKARI:
“Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii
yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa Bwana amemtuma kweli
kweli.”
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, si jambo la ajabu leo kusikia na hata kuona mifumuko ya unabii na
hata wengine kujipambanua kama manabii. Kuwa nabii siyo kitu cha kujitwalia
wala kujinasibu, bali ni kuhesabiwa haki na Mungu mwenyewe tukijua kile
usemacho ni ujumbe wa Mungu na umetumwa na Mungu kusema hivyo na siyo kadiri ya
ndoto zako, au tafsiri zako zenye malengo binafsi. Kwa maantiki hiyo, “Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii yule
litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kuwa Bwana amemtuma kweli
kweli,” Yer 28:9. Ni katika mizania hii
tunaona nani ni nabii wa kweli kati ya Yeremia na Hanania. Hanania anatoa
utabiri wa uongo kwa lengo tu la kumfurahisha mfalme kwa sababu ndicho mfalme
atakacho kusikia, Yer 28:1-4.
Akijua unabii ule si wa
kweli, “Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya
makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya Bwana, naam, nabii Yeremia akasema, Amina,
Bwana na atende hivi; Bwana ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa
vyombo vya nyumba ya Bwana na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hata mahali
hapa,” Yer 28:5-6. Kwa kujipambanua na kuwasadikisha watu kwamba asemacho ni
kweli kutoka kwa Mungu, “nabii Hanania akaitwaa ile nira iliyokuwa juu ya
shingo ya Yeremia, akaivunja,” Yer 28:10. Tendo hili la kuivunja nira juu ya
shingo la Yeremia lilimaanisha ‘ndivyo Bwana atakavyoivunja nira ya Nebukadreza,
mfalme wa Babeli, kabla haujatimia muda wa miaka miwili mizima, na kuiondoa
shingoni mwa mataifa yote,’ Yer 28:11. Ni mbaya sana kujiinua nafsi yako, na
hasa pale utakapo kupata sifa kutoka kwa watu na kujipendekeza kwa wakubwa na
kusahau ile kweli.
Hata hivyo Mungu huwa
hamfichi mnafiki. Huyu ndiye Mungu asiye kwenda na mawimbi yetu wanadamu wala
matakwa yetu binafsi. “Ndipo
neno la Bwana likamjia Yeremia, baada ya Hanania, nabii, kuivunja ile nira
iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, kusema, Enenda
ukamwambie Hanania, ukisema, Bwana asema hivi, Umezivunja nira za mti; lakini
badala yake utafanya nira za chuma,” Yer 28:12-13. Na nira za chuma ilimaanisha
kwamba, “Bwana wa majeshi, Mungu wa
Israeli, asema hivi, Nimetia nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote,
ili wamtumikie Nebukadreza, mfalme wa Babeli nao watamtumikia; nami nimempa
wanyama wa nchi pia,” Yer 28:14. Kitendo hiki kilimaanisha kwamba, ‘wana wa
Israeli hawakutaka kulijua kosa lao lililowafanya kuwa katika hali ile ya
utumwa.’
Ingawa
Huruma na Neema ya Mungu ipo muda wote na wakati wowote, bila kufanya toba ya
kweli na majuto kumrudia Mungu, huruma na neema hiyo ya Mungu itapita tu bila
kuguswa nayo. Na wale wote wenye kuupindisha ukweli wa Mungu kama ulivyo
hawawezi kubaki salama. “Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania,
Sikia sasa, Ee Hanania; Bwana hakukutuma; lakini unawatumainisha watu hawa
maneno ya uongo,” Yer 28:15. Hii siyo maana ya kuwa Nabii wa Mungu kama mjumbe
wake mwaminifu. Na hivi ndivyo Yeremia alivyo ufikisha unabii wa kweli kwa
Hanania; “Basi
Bwana asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka
huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya Bwana,” Yer 28:16. Na unabii huu ulitimia kwa ‘nabii Hanania kwani alikufa mwaka uo huo, mwezi
wa saba,’ Yer 28:17
Kristo Yesu ndiye
ukamilifu wa nyakati na unabii wote uliyo kwisha tangulia kabla yake. “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu
alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini
ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Na Injili ya
leo tunaona hali hiyo ya kuwa wana kwa ukarimu wa Mungu kwa watu wake. Yesu anawaonea huruma wale waliokuwa wanasikiliza neno
lake la uzima. Kibinadamu wanafunzi wa Yesu wanatoa ushauri kwa Yesu kuwa watu
waachwe waende zao vijini na kutafuta chakula. Yesu anawakumbusha wajibu wao
kuwa yawapasa kuwalisha watu hao chakula. Hivyo Yesu anawaambia, “Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi
vyakula,” Mt 14:16. Wapendwa katika Kristo, kwa ubatizo wetu tunashiriki ukuhani wa Kristo, unabii,
na ufalme wake. Hivyo kila mbatizwa kadiri ya wito wake anajukumu la kuwapa
chakula watu wale aliokabidhiwa. Na zaidi chakula hiki siyo tu hiki cha leo na
kesho bali neno la uzima wa milele, ili wamjue Kristo, Mwana wa Mungu kuwa
ndiye ‘Njia ya kweli, kweli isiyo shaka, na Uzima wetu,’ Yoh 14:6
Tumsifu Yesu Kristo!
“Yesu
akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula,” Mt 14:16
Tusali:-Ee Yesu,
tuepushe na unabii na manabii wa uongo, na mara zote tubaki katika kweli yako.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario