sábado, 27 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 22 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 22 YA MWAKA-C
Somo I: YbS 3:17-20, 28-29
Zab/Kit: 68:4-5, 6-7, 10-11
Somo II: Ebr 12:18-19, 22-24
Injili: Lk 14:1, 7-14
Nukuu
“Mwanangu, wakati wa kufanikiwa uendelee katika unyenyekevu; hivyo utapendwa kuliko mwenye ukarmu,” YbS 3:17

Kadiri ulivyo mkuu uzidi kujinyenyekesha, nawe utapata kibali machoni pa Bwana; kwa maana rehema zake Bwana zi kuu, na siri yake ni kwa wanyenyekevu,” YbS 3:18-20

 “Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi,” Ebr 12:22 

mkutano mkuu na kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika,” Ebr 12:23 

 “Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9 

Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10 

TAFAKARI: Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11 

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 22 ya mwaka “C” wa Kanisa. Masomo yetu yote matatu yamebeba ujumbe wa ‘UNYENYEKEVU.’ Hakika mtu ufanikiwa katika mambo yake mengi pale anapojinyenyekeza. Unyenyekevu ni msingi wa fadhila zote. “Mwanangu, wakati wa kufanikiwa uendelee katika unyenyekevu; hivyo utapendwa kuliko mwenye ukarimu,” YbS 3:17. Kujishusha hakumaanishi ‘UJINGA,’ bali kwa kufungulia ufahamu wa mengi yanayokuzunguka kadiri ya wito na nafasi yako katika jamii husika. Ni kwa mantiki hiyo kwamba, “kadiri ulivyo mkuu uzidi kujinyenyekesha, nawe utapata kibali machoni pa Bwana; kwa maana rehema zake Bwana zi kuu, na siri yake ni kwa wanyenyekevu,” YbS 3:18-20. Watu wote walioacha nyuma mazuri na kukumbukwa ni wale waliojinyenyekeza katika yote waliyokutana nayo kama jaribu.

Kinyume chake ni kwamba, “Msiba wa mwenye kiburi hauleti kupona, mche wa uovu umepandika ndani yake,” YbS 3:28. Kushindwa kwa wengi katika maisha na hata kile walicho kadiri ya wito na nafasi zao utokana na kiburi. Mshahara wa kiburi ni anguko lako mwenyewe. Kumbe nisichoke kuiomba hekima ya Mungu kila siku ili iniongoze katika busara. Na “moyo wa busara utatambua mithali, na sikio sikivu ni tama ya mtaalamu,” YbS 3:29. Unyenyekevu utuinua pale tunapojishusha pasipo shuruti. Naye Yesu ndicho anachotuambia, kwamba, “kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11 

Leo katika somo la Injili Yesu anatupa angalizo hasa tunapoalikwa kwenye tafrija mbalimbali. Tukizama ndani zaidi tunaona kwamba uhai tulionao na maisha tunayoyaishi ni sawa na kualikwa kwenye furaha ya Mungu na utukufu wake. Basi ni vyema mimi na wewe kutambua duniani hapa tunapita tu, na tupo kwa maandalizi ya maisha ya umilele. Ukweli huu wa maisha uniweke wazi kwa haya mambo matatu; maisha ni jukumu la muda mfupi, maisha ni dhamana, na maisha ni jaribu. Na katika Injili ya leo, Yesu anatuwasa hivi kuhusu ukweli huu wa maisha, na zaidi maisha kama jaribu. Naye Yesu anatuambi hivi; Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9. Kama sote tumealikwa harusini ni wazi tumepewa mastahili yaliyo sawa na yule aliyetualika. Je, kwa maanisha nini maisha ni JARIBU?

Mwelekeo huu wa maisha, yaani, maisha ni Jaribu, huonekana katika hadithi ya Biblia yote. Wakati wote Mungu huijaribu tabia ya watu, imani yao, utii, upendo,  ukamilifu na uaminifu wao. Mungu alimjaribu Ibrahimu kwa kumwambia amtoe sadaka mwanae Isaka. Mungu alimjaribu Yakobo alipopaswa kufanya kazi miaka ya ziada ili kumpata Raheli kama mkewe.

Adamu na Hawa walishindwa jaribio katika bustani ya Edeni, na Daudi alishindwa majaribu yake kutoka kwa Mungu mara kadhaa. Lakini Maandiko Matakatifu hutupa mifano mingi ya watu walioshinda majaribu makubwa mfano Yusufu, Ruthu, Esta na Daniel.

Wapendwa wana wa Mungu, ukweli ni kwamba majaribu hukuza tabia na kuiweka wazi, na maisha yote ni majaribu. Siku zote unajaribiwa. Mungu siku zote anatazama unavyoenenda kwa watu, matatizo, mafanikio, migongano, magonjwa, mambo ya kukatisha tamaa, hata hali ya hewa!

Mungu anaangalia hata matendo rahisi sana kama vile unapofungulia mlango wengine, unapookota kipande cha takataka, unapoonyesha upole kwa karani au mhudumu, unapomsikiliza mfanyakazi wako wa nyumbani, nk.

Ndugu yangu, ukweli ni kwamba hatuyajui majaribu yote ambayo Mungu anatupa lakini tunaweza kutabiri baadhi yake, kwa kuzingatia Maandiko Matakatifu. Utajaribiwa kwa mabadiliko makubwa, kucheleweshwa  ahadi, matatizo magumu, sala zisizojibiwa, lawama zisizostahili, na hata mikasa isiyo na sababu. Ndugu, katika maisha yangu nimetambua kuwa Mungu anajaribu imani yangu kupitia matatizo, anajaribu tumaini langu kwa njia ya mali, na anajaribu upendo wangu kwa njia ya watu.

Jaribu la muhimu sana ni jinsi unavyotenda unapoacha kuhisi uwepo wa Mungu katika maisha yako. Wakati mwingine Mungu hujiondoa kwa makusudi, na hatuoni uwepo wake. Mfalme Hezekia alipatwa na jaribu hili. "Walakini kwa Habari ya wajumbe wa wakuu wa Babeli, waliotumwa kwake kuuliza ajabu iliyofanywa katika nchi, Mungu akamwacha, ili amjaribu, ili kwamba ayajue yote yaliyokuwemo moyoni mwake." 2Nya 32:31. Hezekieli akikuwa amefaidi ushirika wa karibu na Mungu,  lakini kwa wakati wa muhimu sana Mungu alimwacha peke yake ili ampime tabia yake, adhihirishe udhaifu wake, na amwandae kwa MAJUKUMU ZAIDI. Kumbe lengo la majaribu si kutuangamiza, bali tunaandaliwa kwa mambo makubwa zaidi, na kwa malengo makubwa zaidi ya Mungu.

Wapendwa katika Kristo, ukielewa kuwa maisha ni jaribu, unatambua kuwa hakuna kitu kidogo katika maisha yako. Hata tukio dogo sana lina maana kubwa katika kukuza tabia yako. Kila siku ni siku ya muhimu, na kila dakika ni wasaa wa kukua kitabia, kuonyesha upendo, au kumtegemea Mungu. Majaribu mengine hata huyatambui. Lakini yote haya yana matokeo ya milele.

Habari njema ni kwamba Mungu anakutaka ushinde mtihani huo wa maisha, kwa hiyo haruhusu majaribu unayoyapata kuwa makubwa kuliko neema anayokupatia katika kukabili majaribu hayo."Jaribu haliwapati ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili." 1Kor 10:13

Mpendwa katika Kristo, kila unaposhinda jaribu, Mungu hutambua na kupanga kukupa tuzo la milele. Mtume Yakobo anasema, "heri mtu astahimikiye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao." Yak 1:12.

Basi ndugu yangu ninaye safiri nawe katika tafakari hii, yakupasa kujua kuwa sote ni waalikwa na siyo ‘mgeni rasmi.’ Kwa utaratibu wa kawaida mbele palipoandaliwa si mastahili yangu. Na kama nitakuwa mbele nielewe nipo hapo kwa kuhesabiwa haki na yule aliyenialika. Kama ni kiongozi katika taasisi yoyote ile, nielewe nipo hapa kwa kuhesabiwa haki hiyo na Mungu kupitia watu wake. Hivyo nifanye yote kadiri ya utaratibu uliopo wakati huo huo niheshimu mara zote kiapo changu kwa nafasi ile niliyohesabiwa haki na Mungu kwa kupitia watu wake kwa utaratibu tuliojiwekea.

Hali na mazingira haya yanifanye nizame ndani zaidi na kuyaona maisha kama jukumu la muda mfupi. Wito huu unikumbushe mara zote kufanya yale yanayo mpendeza Mungu kuelekea maisha yale ya milele. Pili, nione ukweli wa maisha na nafasi niliyopewa na watu kuwa ni dhamana. Ukweli huu unikumbusha mara zote niwapo mbele nipo kwa kuhesabiwa haki kama kiongozi katika taasisi yoyote ile. Nielewe nimepewa uwakili na siku ya mwisho itanipasa kutoa hesabu yake. La sivyo na kama hili silifahamu vizuri, ni vyema na busara kutafuta nafasi nyingine. Na ndivyo Yesu anavyotuambia ili kuwa sehemu salama zaidi, Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10. Huku ndiko kwa maneno mengine kupungua ili Mungu awe na nafasi juu ya maisha yako. Na huu ndiyo unyenyekevu utakao kupandisha pale unapojishusha.

Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii utakubaliana nami kwamba kati yetu kwa nafasi tulizokuwa nazo na madaraka tuliyonayo yaliyopitiliza hututia upofu na kutufanya kuwa ndiyo fimbo ya kuchapia wengine. Jeuri hii ndugu yangu tunaipata wapi wakati Maandiko Matakatifu yanatuambia, Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara,” Zab 90:10. Jinyenyekeshe basi na kuwa kile Mungu alichokusudia katika maisha yako. Kwa nini basi wajifananisha na Mungu asiye jaribiwa? Je, wajua idadi ya nywele zako kichwani? Kama hujui mipaka yako kitazame kifo. Na kama huna hofu ya kifo kwa kiburi chako, tafakari kwa kina tendo la usingizi/kulala. Hili ni zoezi la Kifo. Wengi wetu hulala kama kawaida na mara hukosa fursa ya kuamka tena. Je, hata usingizi siyo jaribu kwako kwamba wewe si lolote wala chochote?

Na swali la kujiuliza ni hili: Je, mwisho wa hayo yote ni nini? Kama mimi na wewe sioni maisha ni JARIBU, kujishusha itakuwa vigumu sana. Pasipo unyenyekevu nitegemee anguko langu binafsi. Na huku ndiko kupoteza lengo la Maisha kuelekea ule ukamilifu, Mt 5:48-(utakatifu) kama cheo chetu, na mwisho kutokuurithi ufalme wa mbinguni. Mwenye hofu ya Mungu ataweza kuepuka anguko lake binafsi. Na huu ndio wa Mungu kwako na kwangu. Bali ninyi mmeufikilia mlima Sayuni, na mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni, na majeshi ya malaika elfu nyingi,” Ebr 12:22. Hili ndilo Kanisa la wateule yaani, watakatifu. Ni  mkutano mkuu na Kanisa la wazaliwa wa kwanza walioandikwa mbinguni, na Mungu mwamuzi wa watu wote, na roho za watu wenye haki waliokamilika,” Ebr 12:23. Ndugu yangu uwapo hapa duniani, “itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake?” Mk 8:36. Tumtazama Yesu aliye kielelezo chetu. Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili,” Ebr 12:24. Huyu ndiye kila kitu kwako na kwangu. Tujifunze kwake.

Tembo kwa umbo lake huweza kuyala majani yaliyo juu ya mti na hata yatambaayo chini ardhini. Kwa uwezo wa mdomo wake, Tembo huyafuruga maji kabla ya kuyanywa. Na sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kuvifukuza mbali vile vyote ‘atarishi’ kwa afya na maisha yake akiwemo chura.
Lakini pamoja na ukweli huu juu ya Tembo, ‘SISIMIZI’ kwa umoja wao huweza kumwangusha tembo na kumfanya kitoweo, na hata jumba la muda tu la kuishi. Kumbe pamoja na ukubwa alio nao Tembo, uwepo wa SISIMIZI umkumbusha namna ya kutembea vizuri.

Ndugu yangu, kama ilivyo kwamba hakuna lililo dogo katika maisha, ndivyo hivyo hivyo hakuna aliye mdogo kama sote tunaishi pamoja katika kweli na haki. Hawa wadogo katika udogo wao wanaweza kuwa sababu ya wewe kutolifikia lengo lako hata kama nia unayo. UNYENYEKEVU ndiyo msingi wa fadhila zote.  Na ndivyo Yesu anavyotutaka tufanye katika unyenyekevu na utu wa kweli, mwamba, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12. Tuwe tayari hata kuwaalika mahasimu wetu. Huku ndiko kukomaa kimwili na kiroho.

Na kwa namna nyingine Yesu anatuambi, Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14. Hawa ni wale wote wasio na sauti katika jamii. Nao wana haki ya kuishi kama wewe unavyoishi kwa kupenda mno starehe, anasa na tafrija. Kufikia kipimo hiki katika maisha kutakuitaji unyenyekevu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Moyo wa busara utatambua mithali, na sikio sikivu ni tama ya mtaalamu,” YbS 3:29

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie fadhila ya Unyenyekevu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario