sábado, 20 de agosto de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 21 YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 21 YA MWAKA-C
Somo I: Isa 66:18-21
Zab/Kit: 117:1, 2
Somo II: Ebr 12:5-7, 11-13
Injili: Lk 13:22-30
Nukuu
Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu,” Isa 66:18 

Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa,” Isa 66:19

 “Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?” Ebr 12:7 

Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani,” Ebr 12:11 

 “Mtu mmoja akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache?” Lk 13:23

Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24 

TAFAKARI: “Wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya ‘21’ ya mwaka ‘C’ wa Kanisa. Masomo ya leo yanatualika kila mmoja wetu atafakari kwa kina mwenendo wa maisha na wito wake. Mwenendo huo wa maisha ndiyo sababu na kigezo cha kuwa wa ‘kwanza au wa mwisho.’ Hata hivyo hatuwezi kusahau kwamba lengo la kuumbwa kwetu kwa sura na mfano wake Mungu, ni kuishi milele. Kwa hiyo Mungu anakutakia maisha ya milele. Mungu kama mwalimu lengo lake ni mimi na wewe tufaulu na kuwa wa kwanza. Ni mwalimu wa pekee na waajabu ambaye hufurahia kushindwa kwa wanafunzi wake.

Kwa maneno mengine, kushindwa kwa mwanafunzi kwa maana nyingine kwa weza dhihirisha pia kushindwa kwa mwalimu. Kufaulu mtihani wa maisha kwa tegemea sana maisha yanayoongozwa na malengo. Na kufikia lengo lolote lile katika maisha kunaitaji “nidhamu” kama kiungo muhimu sana. Licha ya nidhamu kukuweka katika mstari sahihi kuelekea pale unapopataka, nidhamu hiyo hiyo ukuwajibisha pia pale unaporegea. Na nidhamu hii ndiyo aizungumziayo Yesu na kusema, Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24. Hivyo hakuna yeyote kati yetu asiyependa mafanikio mazuri katika maisha. Hata hivyo kuyapata na kuyafikia mafanikio hayo mazuri kutakuitaji “nidhamu na maadili” kwa kile ukichuchumiliacho. 

Nidhamu na maadili ndicho kiongoza njia cha kufika pale unapopatamani. Nidhamu na maadili mema katika maisha hutustahimilisha hata pale tunapokata tamaa na kukosa mwelekeo kama tokeo la sintofahamu katika maisha. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?” Ebr 12:7. Nidhamu na maadili mema hukupa maana na ufahamu wa maisha unayoyaishi leo kama tokeo la jana, na kesho kama tokeo la leo. Kwa mantiki hii ya nidhamu na maadili katika maisha, Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani,” Ebr 12:11. Maisha yenye nidhamu na maadili mema humjenga mtu mwili na roho. Kumbe si vyema sana kujionea huruma na kulalama kwa mambo ambayo yapo chini ya uwezo wako kubadilika na kusonga mbele katika furaha ya kweli. Kwa hiyo inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe,” Ebr 12:12-13. Ndugu yangu, licha ya kwamba baadhi ya vidonge vya malaria ni vichungu, twawajibika kuvimeza kwa sababu tunataka kupona. 

Hivyo kwa kulifikia lengo la juu la maisha yako ya Kiroho na Kimwili, na kwa kutumia lugha ya picha ya Yesu, ni lazima wewe na mimi  kujitahidi kila siku kuingia katika mlango ulio mwembamba. Hii ni nidhamu na maadili katika maisha yenye kuongozwa na malengo. Bila shaka wembamba wa mlango huu ni mwaliko wa kuishi kadiri ya yale yanayompendeza Mungu kila mmoja kadiri ya wito wake. Ni kuishi upendo wa Mungu Baba kweli na kuwa na hofu ya Mungu kwa kushika na kuziishi vyema amri za Mungu na Kanisa lake kama familia yake. Utii katika amri za Mungu ni kumpenda Mungu pasipo shaka. Mkinipenda, mtazishika amri zangu,” Yoh 14:15. Kuzishika na kuishi katika amri zake ni pamoja na kutambua ukweli huu kwamba kwa kupitia Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo tutaiona njia ya kuelekea kwake, tunapata uzima wa kweli, na ndani na katika Kristo mwanaye ndipo penye ukweli wa Mungu Baba na maisha ya umilele.

Utabiri na ahadi ya Mungu kama tulivyosikia kutoka somo letu leo la kwanza unakamilika ndani na katika Kristo Yesu. Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu,” Isa 66:18. Utukufu huu wa Mungu ni “ISHARA” ambayo Mungu ataiweka kati yetu nyakati zitakapotimia. Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa,” Isa 66:19. Ishara hii kwa wakati utakapotimia ndiye NENO aliyefanyika mwili na kukaa kwetu, Yoh 1:14. Naye Mtume Paulo anaelezea ishara hii kwa kusema, Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Kupata kupokea hali ya kuwa wana wa Mungu, ni kuwa na uwezekano wa neema na kweli ndani na katika Kristo Yesu. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17

Yesu anathibitisha ukweli huu kwa kusema, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Hivyo, ukweli wa Kristo na Mungu tunaupata katika Maandiko Matakatifu, uzima wake tunaupata katika Masakramenti, na njia ya wokovu wetu ni Utukufu tuupatao kupitia njia aliyoichagua, yaani, Msalaba. Hivyo tunampenda Mungu tunapolishika vyema neno lake. Yesu anatuambia ukweli huu kwa kusema, “Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24. Kuishi upendo wa kweli, kuzitii na kuzishika amri za Mungu na Kanisa, na kuwa na hofu ya Mungu katika yale yote tunayofikiri, tenda, na kuishi ndiko kuchaguliwa kwetu toka asili. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza,” Rum 8:30.

Hii ndiyo sababu ya kuchagua kutuumba kwa sura na mfano wake. Mungu anapenda tuwe wakamilifu kama Yeye alivyo Mkamili. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Hii ndiyo furaha ya Mungu kwetu. Mungu hupenda kufanya kazi na wale wampendao pasipo shaka yoyote. Mtume Paulo anathibitisha jambo hili kwa kusema, Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake,” Rum 8:28. Kila mwenye hofu ya Mungu ndani yake ameitwa kwa kusudi lake. Ni vyema ukaanza sasa kuelewa ukweli huu ndani yako na kuishi kadiri Mungu apendavyo.

Katika safari hii ya kuelekea uzima wa milele tumepewa Roho wa Mungu kutuongoza katika kweli na haki na kutusaidia katika udhaifu wetu kama wanadamu.Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa,” Rum 8:26. Hatuombi jinsi ipasavyo kwa sababu tunaomba kwa ajili ya tamaa zetu na mara tupatapo kile tulichokiomba tunatumia vibaya. Ombi la mtindo huu haliwezi jibiwa kwa sababu hatumruhusu Roho atuongoze. Mtume Yakobo anatupa sababu ya kushindwa kwetu. Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3. Mungu anatupenda kweli na hutupatia yale tuombayo kadiri ya  mahitaji yetu. Hivyo hatupaswi kuwa na mashaka mara tumwendeapo na kuomba yale tunayohitaji.

Mashaka katika maishi hututia hofu na mwisho wa siku tunatawaliwa na mambo mengi na yasiyo ya msingi na kukosa dira ya malengo ya maisha yetu hapa duniani. Katika injili tunamwona mtu mmoja mwenye mashaka anamuuliza Yesu, “Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache?” Lk 13:23. Jibu la Yesu linaturudisha kwenye msingi na malengo ya maisha yetu hapa duniani kama nilivyokwisha elezea hapo mwanzo. Yesu anatujibu kwa pamoja hasa sisi tulio na mashaka, Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24. Mlango huu mwembamba unatuwajibisha kujua lengo la maisha yetu hapa duniani, namna ya kuishi ili kufikia lengo hilo, na ni mambo gani ya msingi yatupasa kuyapa umuhimu katika maisha.

Tusipozingatia jambo hilo kama nilivyokwisha elezea hapa mwanza, tusishangae siku ya mwisho kuambiwa maneno haya. Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu,” Lk 13:27. Udhalimu wa kwanza kwa mtu utakuwa hali ile ya kutokutumia muda wake vizuri na neema anazopatiwa bure na Mungu kupitia Mama Kanisa. Tutashangaa na kupigwa butwaa tutakapoona wale waliotumia vyema muda wao na neema walizojifunua kwao wakiingia katika maisha ya umilele. Wengi wao ni wale leo tunaowaona wa mwisho kwa kila kitu kwa sababu tu hawaendani na mambo ya ulimwengu huu na tamaa zake. Na tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho,” Lk 13:30. Ndugu yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, ni wakati sasa wa kuzama ndani yako na kuhoji nafsi yako kwa hili Yesu alilotuambia leo. Je, lina ukweli wowote juu ya maisha yako?

Ndugu yangu tuliosafiri sote katika tafakari hii, ngoja nikuache na kisa hiki. Pamoja na Fisi kupewa majina mengi na wakati mwingine yenye kuendana na tabia yake, kwa mfano, “Bwana usafi wa pori,” yapo mambo mengine mazuri tuwezayo kujifunza kutoka kwa fisi. Je, huamini?

Fisi amwonapo mtu akitembea huku akiirusha mikono yake mbele na nyuma, tendo hilo humjengea matumaini kwamba ukono ule upo mbioni kudondoka. Hivyo bila kukata tamaa Fisi uongozana na mtu huyu kwa kitambo kirefu.

Jambo lingine kama tabia ya Fisi ni hali ile ya kutokushindwa kwa urahisi hasa kwa yale yaliyo chini ya uwezo wake. Ukweli huu tunaupata kutoka mazungumzo ya watu wanapoonyesha hali ya mshangao wa kitu kwa njia ya swali, kuwa “mfupa ulimshinda fisi mwanadamu atauweza?”

Ni kweli kabisa wewe na mimi tuna mapungufu yetu kama mwanadamu, yaani, mwenye damu na mifupa. Hata pamoja na ukweli huo, hatupaswi kuyachukulia mapungufu hayo kama ukuta kwa kutokuona mbele na mwisho wa yote. Kumbe ni wakati wa kuyatumia yale yaliyo chini ya uwezo wetu ili kulifikia lile lengo sahihi la maisha yetu-uzima wa milele. Hapa ndipo tunapoitaji nidhamu na maadili mema. Na hivi ndivyo tupasavyo kuichagua njia ile nyembamba ili kulifikia lengo.

Ni kutumia kwa ukamilifu yale machache tuliojaliwa na Mungu licha ya udhaifu tulio nao kama wanadamu. Huku ni kulenga katika ukamilifu licha ya udhaifu. Nisipojitajidi katika hili, nijiandae kwa mshangao huu siku ya mwisho kwamba “wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa mwisho.”

Tumsifu Yesu Kristo!

Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24


Tusali:-Ee Yesu, tujalie ustahimilivu katika maisha yetu kila mmoja kadiri ya wito wake. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario