miércoles, 17 de agosto de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 20 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 20 YA MWAKA-C

Somo: Eze 36:23-28
Zab/Kit: 51:12-13, 14-15, 18-19
Injili: Mt 22:1-14
Nukuu
Nami nitalitakasa jina langu kuu, lililotiwa unajisi katika mataifa, mlilolitia unajisi kati yao; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, asema Bwana MUNGU, nitakapotakaswa kati yenu mbele ya macho yao,” Eze 36:23 

Maana nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe,” Eze 36:24 

 “Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyemfanyia mwanawe arusi,” Mt 22:2

Akawatuma watumwa wake wawaite walioalikwa kuja arusini; nao wakakataa kuja,” Mt 22:3 

 “Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote mwaonao waiteni arusini,” Mt 22:9 

 Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache,” Mt 22:14 

TAFAKARI: Mungu hapendi upotee. ‘Maana nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe.’

Wapendwa wana wa Mungu, ikiwa wewe na mimi leo ni tokeo la upendo wake Mungu, na ndivyo ilivyompendeza kutuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27, Mungu hapendi upotee. Naye asema, ‘nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe.’ Hakika Mungu aliyaona mateso ya wana wa Israeli na kusema ‘kwa sasa inatosha.’ Nami nitalitakasa jina langu kuu, lililotiwa unajisi katika mataifa, mlilolitia unajisi kati yao; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, asema Bwana MUNGU, nitakapotakaswa kati yenu mbele ya macho yao,” Eze 36:23. Mateso ya mwenye haki ni mateso pia ya Mungu kwa sababu haki ina Yeye. Vita ya haki juu ya mwenye haki, binadamu mvunja haki na mwenye kuzikanyaga haki za wengine, hatoweza kushinda vita hiyo na hatosalimika katika mkono wa Mungu. 

Wenye haki na walio na hofu na Mungu husitawi daima katika mikono salama ya Mungu. Maana Mungu asema hivi juu yao, nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe,” Eze 36:24. Kumbe kiburi cha mwenye jeuri itokanayo na wingi wa nguvu alizonazo siyo zuiyo la Mungu kuwapigania wana wake waliodhulumiwa katika kweli na haki. Kwa nini basi twapenda wengine kuishi kama wakiwa katika ulimwengu huu ambao Mungu aliumba ili ukaliwe na watu bila kujali mila, rangi, na desturi zetu? Wewe ni nani basi usiyetaka wengine wapumue? Na haki hiyo ya kuwa wewe tu unaipata wapi, na kwa kibali cha nani? “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine,” Isa 45:18. Pamoja na historia zetu mbaya na hata wakati mwingine kumuasi Mungu kwa dhamiri zetu, bado Mungu anatupenda kama tulivyo.

Na hata katika udhaifu huu wetu wa kibinadamu Mungu anatuhaidia utakaso na upya ndani yetu, na kusema, Nami nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi; nitawatakaseni na uchafu wenu wote, na vinyago vyenu vyote,” Eze 36:25. Hakuna asiye na kinyago chake katika maana ya ‘dhambi dola’ kwake. Dhambi dola ni dhambi ile ambayo kila mara ujikuta umedondoka tena na tena. Ni dhambi ambayo bila shaka kila mara huiungama. Dhambi hiyo ni tawala kwako kama ilivyo dola ya taifa fulani. Hiki huwa kinyago kwako kwa sababu ndiyo mwonekano wako wa nje na wenye kuififisha sura ya Mungu ndani mwako. Kumbuka umeumbwa kwa sura na mfano wake Mungu, Mwa 1:27. Hivyo una chapa ya Mungu ndani yako. Hata katika hali hii Mungu yupo tayari kukutakasa na kutoka katika kinyago hicho.

Utakaso huu ni nguvu ile ya Mungu ndani yetu, yaani, “nguvu wezesha, nguvu thubutu.” Nguvu hii ndiyo anayoisema Mungu kwamba, Nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama. Nguvu hii utuwezesha kuzipokea zile neema atujaliazo Mungu kutimiza yale ya kimungu. Uwezo huu siyo kwa nguvu na bidii zetu wanadamu, bali ni Mungu mwenyewe kama asemavyo kwamba, Nami nitatia roho yangu ndani yenu, na kuwaendesha katika sheria zangu, nanyi mtazishika hukumu zangu, na kuzitenda,” Eze 36:27. Hizi ndizo neema za Mungu ndani yetu na zenye kutuwezasha kuyafanya yote ndani na katika Mungu kama wana na warithi wake. Furaha ya Mungu ni kwa kila mmoja wetu kuwa kile alichoumbwa na mwisho wa siku kufikia sababu ya kuumbwa kwake, yaani, ‘amjue Mungu, ampende Mungu, amtumikie Mungu, na mwisho arudi kwake Mbinguni.’ Ni katika maana hii Mungu anasema,  Nanyi mtakaa katika nchi ile niliyowapa baba zenu, nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu,” Eze 36:28 

Upendo huu wa Mungu na ukarimu wake kwetu wa kushirikisha kila mmoja wetu katika Furaha na Utukufu wake, Yesu anaufananisha na mfalme mmoja aliyemfanyia mwanawe arusi,” Mt 22:2. Lakini jambo la ajabu ni kwamba licha ya mfalme huyu kuwaalika watu bure na bila kadi kama ilivyo mazingira yetu ya leo, hakuna aliyeitikia mwaliko ule kati ya wale walioalikwa kuja arusini, Mt 22:3. Hata hivyo, kwa kujali sherehe ile na nafasi ya wale walioalimwa, mfalme hakuacha kusisitiza umuhimu wa sherehe ile na yale aliyoyaandaa kwa ajili ya wale walioalikwa. Naye Mfalme  “Akatuma tena watu kwa wengine, akisema, Waambieni wale walioalikwa, Tazameni, nimeandaa karamu yangu; ng'ombe zangu na vinono vimekwisha kuchinjwa, na vyote vimekuwa tayari, njoni arusini,” Mt 22:4. Mwaliko huu tunaweza kuufananisha na Sakramenti ya Ubatizo. Kwa Sakramenti hii ya ubatizo sote tunaalikwa na tunafanywa wana na warithi wa ufalme wa Mungu. Hata hivyo, bila utayari wetu wa kuziishi ahadi hizo za ubatizo tutapigwa mshangao kuikosa nafasi hiyo ya kuurithi ufalme wa Mungu.

Ni mara ngapi tunaona licha ya mtu kupokea Sakramenti hii ya ubatizo anaishi kivyake vyake? Hawa ni wale wanaozungumziwa katika Injili ya leo kwamba, Lakini hawakujali, wakaenda zao, mmoja shambani kwake, mmoja kwenye biashara yake; nao waliosalia wakawakamata watumwa wake, wakawatenda jeuri, na kuwaua,” Mt 22:5-6. Ni mara ngapi tunawaona Wakristo wenzetu na wabatizwa kutenda matendo yasiyoendana na Ukristo wao? Hii ni huzuni kubwa kwa Kristo aliyekufia pale Msalabani ili uwe huru kutoka utumwa wa dhambi, na masikitiko makubwa kwa Mungu tunaposhindwa kuthamini sadaka ya Mwanaye Mpenzi aliyoitoa pale Msalabani kwa ulimwengu mzima. Na ni kwa “jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele,” Yoh 3:16. Jionee mwenyewe Mungu asivyopenda upotee!

Hata hivyo kwa ukatili walioonyesha wale walioalikwa na kwa dhamiri zao kwenda kinyume na ukarimu ule wa mfalme kwa kuwatenda jeuri watumwa wake na kuwaua, yule mfalme akaghadhibika; akapeleka majeshi yake, akawaangamiza wauaji wale, akauteketeza mji wao,” Mt 22:7. Ni wazi kabisa kwamba kila mtu atawajibika kwa matendo yake kwa sababu ni tokeo la matumizi ya uhuru ulio ndani yako. Je, Mfalme na kwa mazingira haya anaye mwakilisha Mungu, atasitisha harusi yake kwa vile walioalikwa hawakwenda? Mt 22:8. La hasha! Ukweli ni kwamba huruma, upendo, na neema za Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Karamu ya Mungu itafanyika na wengine wataalikwa hata kama hawakuwa katika mpango mzima wa kile kilichoandaliwa. Na hivi ndivyo alivyofanya Mfalme na kuwaambia watumwa wake, Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote mwaonao waiteni arusini,” Mt 22:9. Bila shaka ndivyo Mungu atakavyofanya tunapoupuuzia mwaliko wake. Hapa ni pale Mungu anapotukusanya wote bila kujali mapungufu yetu. Kwa upande wako na mimi ni lazima nione tendo hili kuwa ni Upendo wa pekee wa  Mungu kwangu, na wakati wa kubadilika na kuthaminisha fursa hiyo ya pekee kama nafasi ya kubadilika kwa kuwa hayakuwa mastahili yangu.

Na hivi ndivyo ilivyokuwa, kwamba, Watumwa wale wakatoka wakaenda njia kuu, wakakusanya wote waliowaona, waovu kwa wema; arusi ikajaa wageni,” Mt 22:10. Kundi hili linamfanano na ‘juya lile lililotupwa baharini likakusanya samaki wa kila namna, na hata lilipojaa lilivutwa pwani na ndipo walipotengwa walio wema chomboni na wabaya wakatupwa, Mt 13:47-48.’ Na hapa ndipo tunapopata maana halisi ya hatua aliyoichukuwa mfalme alipoingia kwenye ukumbi wa sherehe. Na hali ilikuwa hivi, lakini alipoingia yule mfalme ili kuwatazama wageni wake, akaona mle mtu mmoja asiyevaa vazi la arusi,” Mt 22:11. Huyu jamaa aliyegundulika kutokuvaa vazi la arusi hakutumia vyema nafasi ile aliyokirimiwa bila mastahili yake katika kuyaondoa mapungufu yake. Huyu ni sawa na muumini aliyepata nafasi ya kuhudhuria maadhimisho ya Misa Takatifu, mazingira ambayo kabla ya Misa ile Takatifu kulikuwa na nafasi ya kupokea Sakramenti ya upatanisho, naye asiitumie nafasi hiyo ilhali anajua hakuwa mkamilifu. Na kinyume chake kutaka kushiriki meza ya Bwana katika hali hiyo ya dhambi.

Ingawa hatumuoni Kristo katika hali ya kushikika zaidi ya maumbo yale ya mkate na divai, elewa Kristo anakuambia kama mfalme huyu alivyomwambia ndugu huyu kwamba, Rafiki, uliingiaje humu nawe huna vazi la arusi?” Mt 22:12. Je, katika hali na mazingira kama hayo wataka malaika washuke na kukukumbusha wajibu wako huo kama Mbatizwa? Bila shaka alivyotendewa mtu yule nasi tutatendwa hivyo hivyo kwa amri ya mfalme na kufungwa mikono na miguu, kutolewa na kutupwa katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno,’ Mt 22:13. Na hii ndiyo maana ya maneno haya kwamba,  waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache,” Mt 22:14. Kwa Sakramenti ya Ubatizo sote tunaitwa kuwa wana na warithi wa Ufalme wa Mungu. Ila kuteuliwa kwetu na kuingia katika Ufalme huo kutategemea kuishi vyema ahadi zetu za ubatizo.

Tumsifu Yesu Kristo! 

“Rafiki, uliingiaje humu nawe huna vazi la arusi?” Mt 22:12

Tusali:-Ee Yesu, nijalie neema ya kuishi vyema ahadi zangu za ubatizo, ili mwisho wa siku zangu 
hapa duniani nisije nikapigwa na mshangao. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario