lunes, 30 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 1 YA MAJILIO MWAKA-C

JUMANNE WIKI YA 1 YA MAJILIO
1/12/2015
Somo: Isa 11:1-10
Zab: 72:1-2, 7-8, 12-13, 17
Injili: Lk 10:21-24
Nukuu:
Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda,” Isa 11:1 

Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana,” Isa 11:2

bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya,” Isa 11:4 

Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza,” Isa 11:6 
Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira,” Isa 11:8 

Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu,” Isa 11:10
Saa ile ile alishangilia kwa Roho Mtakatifu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:21 

Akasema, Nimekabidhiwa vyote na Baba yangu, wala hakuna amjuaye Mwana ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia,” Lk 10:22

TAFAKARI: “Kwake itasimama kweli, haki, Amani, na Upendo.”

Wapendwa wana wa Mungu, kumkomboa mwanadamu kutoka hali yake ya mateso, mahangaiko na dhambi, Mungu aliye Kweli, Haki, Amani, na Upendo kwa makusudi makubwa anapenda kuanzisha uhusiano na yule aliyemuumba kwa sura na mfano wake. Tendo hili la kuujenga uhusiano wa karibu nasi linamshusha Mungu chini kabisa katika hali ya mwanadamu. Huu ni upendo mkubwa sana kwetu. Kipindi hiki cha majilio ni kipindi cha kutafakari upendo huu wa ajabu Mungu anaokwenda kutufanyia. Ikiwa zawadi hii ni kubwa sana kwetu hatuna budi kujiandaa vizuri mwili na roho ili atakapokuja atukute tupo safi na wenye afya njema hasa roho zetu.

Kufanikisha mpango huu, Mungu huyu aliye alfa na omega atachukua hali yetu ya kibinadamu, na hivyo atazaliwa ikiwa ni moja ya kushiriki hali yetu ya kibinadamu. Jambo hili linatabiriwa na Nabii Isaya. Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda,” Isa 11:1. Je huyu atakayezaliwa ataongozwa na mamlaka gani? Hakika kwa vile anakuja kuusimika ufalme wa kweli, haki, amani, na upendo, roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana,” Isa 11:2. Hivi ndivyo vitendea kazi vyake. Ujio wake kwetu ni hukumu pia ambayo itasimama katika haki. Hivyo, kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya,” Isa 11:4 

Ujio wa mfalme huyu ni ujio wa neema na baraka. Anakuja na kusimika mfumo wema na kuufifisha mfumo wa uovu. Anakuja kuondoa sintofahumu zetu kati yetu wanadamu na viumbe vingine alivyoviumba. Huyu hakika ni mfalme wa Amani. Hakutakuwa tena na sintofahumu kati ya wanyama aliowaumba. Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza,” Isa 11:6. Mwanadamu ataishi kwa amani na hofu haitakuwepo tena. Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira,” Isa 11:8.

Uwepo wa Mfalme huyu wa kweli,  haki, amani na upendo utajidhihirisha kwa utukufu wake. Mataifa yote watamfuata alipo kwa sababu kuna utukufu. Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu,” Isa 11:10. Haya ndiyo atakayoyafanya na kuujenga tena uhusiano wetu ulioharibiwa na dhambi zetu.

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na hayo mazuri yote yaliyotabiriwa na Nabii Isaya kuhusu Mfalme huyu tunayemsubiri kwa hamasa kubwa, yatawezekana tu kama tutakuwa tayari kutoa ushirikiana naye. Mungu atukokoti kama Jemedari katili na mwenye silaha za kutisha. Utawala wake ni utawala wa Upendo. Mungu hakupenda kutuondolea uhuru na utashi wetu wa kumfuata. Ametuachia haya yote akijua kabisa kwa kuyatumia vizuri ni njia rahisi ya kumfikia, hata pale tutakapoyatumia vibari itakuwa njia rahisi pia ya kumrudia tukifanya toba ya kweli na majuto. Kwa hiyo, ‘aliyekuumba wewe pasipo wewe hawezi kukukomboa wewe pasipo wewe,’ Mt. Agustino wa Hippo.

Siri ya ukweli huu wa kutoa ushirikia na  Mungu ili kuwa sehemu salama anausema Yesu katika Injili ya leo. Siri hii ni kuwa kama watoto wachanga. Mtoto mchanga huamini yote kuwa salama anapokuwa mikono mwa wazazi wake. Mtoto mchanga kamwe hawezi kuacha kutabasamu hata kama akiwa mikononi kwa mtu mwovu. Maana yake mtoto mchanga mara zote anamtazamo chanya. Hii ndiyo hekima ilifichwa ndani ya watoto wachanga. Yesu anatutaka kuwa na unyenyekevu huu katika kuamini yote kuwa salama mikononi mwa Mungu. Naye Yesu, “Saa ile ile alishangilia kwa Roho Mtakatifu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza,” Lk 10:21. 

Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, leo Yesu anatufunulia jambo la pekee sana. Kwanza kabisa ni Yeye tu aliyebabidhiwa yote na Mungu. Pili hatuwezi kumjua Mungu Baba pasipo Yeye mwana, yaani Yesu Kristo. Kwa maana hiyo, kuwa na Yesu ni kuwa kwenye mikono salama. Naye Yesu, Akasema, Nimekabidhiwa vyote na Baba yangu, wala hakuna amjuaye Mwana ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia,” Lk 10:22. Je, ulipo na ulipojikabidhi kuna usalama?

Tumsifu Yesu Kristo!

Jina la Bwana ni ngome imara; Mwenye haki huikimbilia, akawa salama,” Mit 18:10


No hay comentarios:

Publicar un comentario