miércoles, 11 de noviembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 32 YA MWAKA-B

ALHAMISI WIKI YA 32 YA MWAKA-B
12/11/2015
Somo: Hek 7:22-8:1
Zab: 119:89, 90, 91, 130, 135, 175
Injili: Lk 17:20-25
Nukuu:
“Ufalme wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; wala hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo ndani yenu,” Lk 17:20b-21

Lakini kwanza, hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki,” Lk 17:25
“maana Mungu humpenda yeye tu akaaye na Hekima,” Hek 7:28

“Marini kuliko jua, Hekima hupita makundi ya nyote; ikilinganishwa na nuru, huonekana ya kuwa imezidi,” Hek 7:29

“maradi baada ya nuru ya mchana hufuata usiku, bali juu ya Hekima hakuna ovu liishindalo,” Hek 7:30

“Hekima huenea kwa nguvu nyingi toka pembe hii hata pembe hii ya dunia, na kuyaratibisha mambo yote kwa jinsi ya ufaa,” Hek 8:

TAFAKARI: “Ufalme wa Mungu umo ndani yenu.”

Wapendwa wana wa Mungu, maisha yako na makusudi ya kuumbwa kwako na Mungu ni kuishi milele. Ufalme wa Mungu upo ndani yetu tangu kuumbwa kwetu. Mungu kwa kutuumba kwa sura na mfano wake alianzisha rasmi ufalme wake ndani yetu. Kwa hiyo ni jukumu yako na langu kuupokea kwa uhuru ufalme huu na kuwa sehemu ya maisha mapya na Mungu au kuukataa. Hivyo pamoja na kwamba ufalme huu wa Mungu umo ndani yetu tunayohiari ya kuukataa pia kwa sababu Mungu haingilii uhuru wetu.

Ni kwa maana hii hatuwezi kusema ufalme wa Mungu waja kutoka upande gani wa maisha yetu, bali yatupasa kujibiidisha kila siku kuuelewa na kuuishi. Yesu leo anatuambia, “Ufalme wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; wala hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo ndani yenu,” Lk 17:20b-21. Hii ni sehemu ya kwanza kuhusu ufalme wa Mungu, yaani ni kufanya juu chini kuutambua na kuuishi kila siku. Sehemu ya pili kuhusu ufalme wa Mungu ni yale Kristo aliyojitolea kwa ajili yako, yaani mateso na kifo cha msalaba. Hapa ndipo tulipohesabiwa haki na Mungu kwa kumtoa mwanaye Mpendwa afe kwa ajili ya dhambi zetu nasi tuwe huru na warithi wa ufalme wake. Je, unayo sadaka ya kutoa?

Wapendwa wana wa Mungu, kama wewe ni mfuasi kweli wa Kristo elewa jambo hili: ‘hakuna utukufu pasipo msalaba, na hakuna pasaka pasipo ijumaa kuu.’ Kristo alijitoa kwa ajili yetu sisi na kukubali kuiendea njia ile ya mateso kwa ajili ya kweli na haki. Naye Yesu anatuambia hayo yote yatatokea, Lakini kwanza, hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki,” Lk 17:25. Nasi kama wafuasi wake Kristo tutaifuata njia itupelekayo kwenye utukufu na ufufuko tunaposimama katika kweli na haki na hapo tutaonya mauti yake. Kuufahamu ukweli huu twahitaji hekima ya Mungu kuyachambua yote kwa busara, na kutenda katika kweli na haki. “Maana Mungu humpenda yeye tu akaaye na Hekima,” Hek 7:28.

Ndugu yangu tuliyesafiri pamoja kwenye tafakari hii, tunahitaji sana hekima ya Mungu ili tuyaone mahangiko yetu na mateso yetu kama sehemu muhimu ya wokovu wetu ambao tayari tunao ndani mwetu. “Hekima huenea kwa nguvu nyingi toka pembe hii hata pembe hii ya dunia, na kuyaratibisha mambo yote kwa jinsi ya ufaa,” Hek 8: Tuikubali hekima ili hekima hiyo itufunulie siri za Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa,” Mt 6:31-33


No hay comentarios:

Publicar un comentario