sábado, 28 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 1 YA MAJILIO MWAKA-C

JUMAPILI YA 1 YA MAJILIO YA MWAKA C
29/11/2015
Somo I: Yer 33:14-16
Zab: 25:4-5, 8-9, 10, 14
Somo II: 1The 3:12-4:2
Injili: Lk 21:25-28, 34-36
Nukuu:
Katika siku zile, na wakati ule, nitamchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atafanya hukumu na haki katika nchi hii,” Yer 33:15 

Katika siku zile Yuda ataokolewa, na Yerusalemu utakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 33:16

Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima,” Lk 21:34-35 

Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu,” Lk 21:36

Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu,” 1The 3:12
Iliyobaki, ndugu, tunakusihini na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana,” 1The 4:1  

TAFAKARI: “Bwana ni haki yetu.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, karibuni katika tafakari ya leo ikiwa Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya kwanza ya majilio ya mwaka C wa Kanisa. Leo pia kwa namna ya pekee tunaanza mwaka C wa Kanisa. Masomo na tafakari zetu zitalenga katika kipindi hiki cha Kanisa. Kipindi hiki cha Majilio Kanisa linajifananisha na Taifa la Mungu la Agano la Kale linapotarajia kwa hamu kubwa ujio wa Mkombozi. Hivyo kipindi hiki Mama Kanisa anawaandaa wana wake kuwa tayari kumpokea Mkombozi. Hata hivyo kipindi hiki cha Majilio kina sura nyingine, ambayo inaufunua ujio wa siku ya mwisho wa Bwana. Ni kwa namna hii Kanisa limegawa kipindi hiki cha Majilio katika sehemu kuu mbili nazo ni hizi zifuatazo: Sehemu ya kwanza inaanza leo hadi hapo tarehe 16 ya mwezi Desemba. Mambo makuu katika kipindi hiki ni kutafakari juu ya ujio wa pili wa Kristo katika utukufu wake. Sehemu ya Pili, Mama Kanisa atakuwa anatafakari juu ya  matayarisho ya sikukuu ya kuzaliwa kwake Yesu Kristo. Msukumo na wazo kuu katika kipindi hiki ni “Kristo yu karibu,” Yeye ni Mkombozi na hakimu.

Hivyo basi katika kipindi hiki cha Majilio tunajitayarisha kwa furaha kumpokea Kristo tukisikia na kuifuata sauti ya mtu yule aliye nyikani: “Itengenezeni njia ya Bwana.” Matengenezo ya njia hii hubeba thana nzima ya mwili na roho. Kristo atakapokuja atukute taa zetu zinawaka nasi tupo macho. Masomo yetu yote matatu yanamwelezea Bwana wetu na Mungu wetu kama mtu kwenye haki. Haki hii haipindishwi kwa lolote lile, bali ni matokeo ya ule utayari wetu wakujifungamanisha naye kuliko kweli na haki. Kama Mungu na Bwana wetu anajua yote kuhusu sisi, basi hatuna chochote cha kumficha wala kujivunua tukijidanganya kuwa ni mali yetu wenyewe. Yeye hubadili majira na nyakati; huuzulu wafalme na kuwamilikisha wafalme; huwapa hekima wenye hekima; huwapa wenye ufahamu maarifa; yeye hufunua mambo ya fumbo na ya siri; huyajua yaliyo gizani, na nuru hukaa kwake,” Dan 2:21-22. Ndugu yangu, ni nani basi zaidi ya Mungu wetu? Bwana ni haki yetu!

Siku ya hukumu ya mwisho licha ya kwamba hatujui ni lini, hatuwezi kuipuuzia kwamba haitakuwepo. Kila kitu kitapita ila neno la Bwana litabaki milele licha ya utofauti wake kati ya kile kisemwacho na tendo lenyewe kutokea. Kuchelewa kwa tukio lenyewe kusitutie upofu na uziwi wa kutokuishi kadiri ya mapenzi ya Mungu na atakavyo. Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Lk 21:33. Nabii Yeremia anatuambia kwamba katika mpango huu wa wokovu na hukumu ya mwisho utafanywa na Mungu chini ya chipukizi la haki na katika haki hiyo kila mtu atapata mastahili yake. Katika siku zile, na wakati ule, nitamchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atafanya hukumu na haki katika nchi hii,” Yer 33:15. Kuokolewa kwetu ni tokeo la kuishi katika kweli na haki. Ni rahisi kufanya ujanja ujanja katika ulimwengu huu lakini si kwa Mungu aliye hai na mwona yote katika yote na muda wote. Hivi ndivyo atakavyofanya; Katika siku zile Yuda ataokolewa, na Yerusalemu utakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 33:16.

Wapendwa katika Kristo, kwa vile muda wetu hapa duniani ni mfupi sana, ni vyema tukawekeza kwa yale yampendezayo Mungu hakimu wetu wa haki. Lengo la maisha yako na yangu katika ulimwengu huu siyo kuyafurahia maisha kwa sababu ya kuyafurahia tu, bali kuyatazama maisha katika umilele wake. Katika Injili ya leo Yesu anatukumbusha maana halisi ya uwepo wetu katika ulimwengu huu ukiendana na yale yatupasayo kufanya. Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima,” Lk 21:34-35. Namna ufikirivyo kuhusu hali yako ndivyo kwa namna hiyo huyafinyanga maisha yako. Wapo kati yetu maisha kwao ni kufurahia kila kunapo nafasi ya kufanya hivyo. Ila Mtume Paulo anasema juu ya jambo hili; ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17. Uzima wa mtu ni zaidi ya haya ya leo na kesho.

Wapo pia kati yetu wanafikiri maisha ni kuwa na vitu na utajiri. Muda wao wote ni kuhangaika kuhusu mali na vitu, na mwisho wa siku ni huzuni na kukata tamaa. Mzaburi anatupa angalizo na kusema, “Usiogope mtu atakapopata utajiri, Na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua cho chote; Utukufu wake hautashuka ukimfuata,” Zab 49:16-17. Maisha ya utakaso ndiyo salama yetu siku hiyo ya mwisho. Utakaso huu ndiko tunakoalikwa kila siku kufanana na Yesu. Si jambo rahisi ila yakupasa kwa moyo wote uamue, ujitahidi kuishi maisha hayo, na utumudu katika maisha hayo hadi mwisho wake. Kudumu katika maisha hayo ndiko Yesu anaposema kukesha. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu,” Lk 21:36. Tunamsubiri Mwokozi wetu kwa kukesha tukiitakatifunza miili yetu na roho zetu.

Kukesha huku katika kweli na haki hujionyesha kwa kuwa na mahusiano mazuri na wale tunaoishi nao kila siku. Upendo ni tokeo la maisha ya kweli na haki, na upendo huo huo usukuma maisha ya kweli na haki. Mtume Paulo anawasihi watu wake waige kile alichokifanya kwao na wenzake. Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu,” 1The 3:12. Hili ni jambo jema la kuiga. Neno la Mungu, watu, na mazingira humfinyanga na kumkomaza mtu na kukuza tabia yake. Tabia njema ndiyo itakayotufikisha kwenye uzima wa milele, na siyo utajiri tunaouangaikia usiku na mchana. Mwisho wa haya yote twapaswa kufanana na Kristo kwa sababu ni kwa njia yake wokovu wetu uwezekana. Hivyo, Iliyobaki, ndugu, tunakusihini na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana,” 1The 4:1. Kristo Yesu ndiye kielelezo cha maisha yetu, na ufunuo halisi wa Mungu Baba. Kukesha huku Yesu anakutafsiri kama “kukaa,” katika neno lake. Kukaa huku katika neno lake ndiko kunatufanya wanafunzi wake wa kweli ambayo kweli hiyo itatufanya huru. Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh 8:31.32

Mzee Damas akiwa amelazwa hospitalini katika uzee wake wa miaka 85, chini ya uangalizi wa mjuu wake Onesmo, alikuwa na mashaka sana na huduma za Kanisa (Masakramenti), ikiwemo Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa. Onesmo akijua Babu yake alikuwa Mkristo na katika hali hii ya ugonjwa wake na mabadiliko ya mara kwa mara ilimlazimu kumwona Paroko wake kwa kupitia jumuiya yake ili Babu yake apate huduma hii ya wagonjwa.

Hivyo baada ya mawasiliano kwenda vizuri kati ya Onesmo, Jumuiya yake, na Paroko, siku ya jumatatu alfajiri ambayo ni siku rasmi ya kuwatembelea wagonjwa, Paroko alikwenda hospitalini kumwona Mzee Dismas na kumpa huduma hiyo. Jambo la ajabu na la kushtusha ambalo halikutegemewa na Paroko na wala Onesmo mjukuu wa Mzee Dismas, ni pale Mzee huyu alipomwona Padre na kujeukia ukutani uku akilivuta shuka lake kujifunika gubigubi.

Tendo hili lilimfikirisha haraka Padre na hivyo alimwomba Onesmo atoke nje kidogo ili aweze kuongea na Mzee Onesmo. Ilichukua muda kidogo hadi Mzee Onesmo kukubali kuongea na Padre na kusema kwa nini hataki huduma hiyo.

Tatizo kubwa la Mzee Dismas lilikuwa hili (nitalisema kwa lugha ya picha), ambalo aliona fika kabisa hawezi kusamehewa na Mungu. “Padre, nilivyokuwa na umri wa miaka saba hivi nilikwenda njia panda na kubadilisha vibao vile elekezi. Kibao kilichoonyesha Dar  es Salaam kuelekea Dodoma, nilikigeuza na kilisomeka Dar es Salaam Iringa. Je, ni wangapi nimewapeleka pasipo tangu nikiwa na miaka 7 hadi leo? Mungu gani anayeweza kunisamehe dhambi hii? Sipendi kumdanganya Mungu katika hili. Nipo tayari kupata adhabu yake," Mzee Dismas aliyasema haya akiwa na hofu kubwa.

Padre kwa kutambua hofu aliyokuwa nayo Mzee Dismas juu ya tatizo lake, alianza na maneno haya, “ndugu yangu Dismas, huruma ya Mungu ni kubwa kuliko dhambi zetu. Bwana anasema na anakuambia leo maneno haya mazito kwako, ‘Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,’ Isa 1:18. Je, maneno haya hayana uzima ndani yako? Sote tunahitaji huruma ya Mungu. Yatupasa sote kukubali udhaifu wetu na kutii maelekezo ya Mungu.” Baada ya maneno haya Mzee Dismas alivuta pumzi na kupumua kwa nguvu kama vile mtu aliyetua jiwe kubwa sana kifuani mwake.

Uso wa Mzee Dismas ulionekana wenye furaha na kukubali kuungana dhambi zake na kuwa tayari kupokea huduma ile ya Ekaristi Takatifu na Mpako wa Wagonjwa. Ndugu zangu, katika kipindi hiki cha majilio tunavyojiandaa kiroho yatupasa kuyatafakari maneno haya ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa undani wake. Yesu anatuambia, Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi,” Mt 11:28-30. Hakuna lisilowezekana kwa Mungu. Tujiachie kwake bila kujibakiza. Wokovu ndiyo sasa.

Ndugu zangu, niwatakieni majilio mema na yenye kumtafuta Bwana wetu na haki yetu kwa nguvu zote. Tuyarudi maisha yetu kwa kuyatazama madhaifu yetu na kuyapatia tiba ya kweli tukimtazama tabibu wetu Yesu Kristo.

Tumsifu Yesu Kristo!


Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:31-32

No hay comentarios:

Publicar un comentario