IJUMAA WIKI YA 31 YA MWAKA-B
6/11/2015
Somo: Rum 15:14-21
Zab: 98:1, 2-3ab, 3cd-4
Injili: Lk 16:1-8
Nukuu:
“ ili niwe mhudumu wa Kristo Yesu kati ya watu wa Mataifa,
niifanyie Injili ya Mungu kazi ya ukuhani, kusudi Mataifa wawe sadaka yenye
kibali, ikiisha kutakaswa na Roho Mtakatifu,” Rum 15:16
“Basi, nina sababu ya kuona fahari katika Kristo Yesu mbele za
Mungu,” Rum 15:17
“Maana sitathubutu kutaja neno asilolitenda Kristo kwa kazi
yangu, Mataifa wapate kutii, kwa neno au kwa tendo, kwa nguvu za ishara na maajabu, katika
nguvu za Roho Mtakatifu,” Rum 15:18-19a
“Toa hesabu ya uwakili
wako, kwa kuwa huwezi kuwa wakili tena,” Lk 16:2b
“Yule bwana akamsifu
wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu
katika kizazi chao wenyewe huwa na busara kuliko wana wa nuru,” Lk 16:8
TAFAKARI: “Ona fahari katika Kristo
Yesu na yahesabu mambo yote yaliyofaida kwako kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.”
Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli kwamba huwezi
‘kuila keki na kuihifadhi kwa wakati ule ule.’ Kwa mantiki hiyo, ama unaila kwa
wakati ule ule kwa uhuru na kufurahia utamu wake, au unaihifadhi iwe fahari ya
macho yako. Ni kwa maani hii wapendwa, upo uhuru na furaha kupoteza yote ya ulimwengu huu
yenye mtazama wa kifaida na kumpata Kristo, kuliko kumpoteza Kristo na kuyapata
ya ulimwengu huu ambayo si yakudumu.
Kwa kumpata Kristo utakuwa na uhakika wa uzima
wa milele. “Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na
kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita
kutoka mautini kuingia uzimani,” Yoh 5:24. Kwa kuupata ulimwengu huu na faida
zake hakuna umilele ndani yake. Ni hasara isiyorekebishika. “Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu
wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” Mt 16:26. Hivyo “Ona fahari katika Kristo Yesu na yahesabu mambo yote yaliyofaida
kwako kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.”
Mtume Petro kama mimi na wewe, alipata ugumu
sana wa kuelewa maana ya maneno hayo ya Yesu. Hivyo alitaka kujua ni nini
matokeo ya sadaka yake ya kuyatoa maisha yake kwa ajili Kristo na Injili kama
njia ya wokovu wa ulimwengu mzima. Yesu anatujibu wote kwa pamoja na kusema, “Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume,
au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na
kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na
ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika
ulimwengu ujao uzima wa milele,” Mk 10:29-30. Yesu
Kristo ananitaka mimi na wewe tuwe na mtazamo mpya kuhusu vitu na fahari zake.
Yesu anatutaka pia kulinganisha vitu na fahari zake tukiyathaminisha hayo na
uzima wa milele.
Mtume Paulo alifaulu kwa
kiasi kikubwa katika mtazamo wa vitu na faida zake, na thamani ile tuipatayo
tunapoacha kushikamana na vitu hivyo na faida zake. Naye anasema, “Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa
hasara kwa ajili ya Kristo. Naam,
zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi
wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya
mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo,” Flp 3:7-8. Mtume
Paulo anaona fahari kubwa sana kumpata Kristo na kuishi kwa ajili ya Kristo
hasa kuwa mjumbe mzuri wa habari njema kwa wengine. Kwa sababu hiyo, Mtume
Paulo anasema, “ili niwe mhudumu wa Kristo Yesu kati ya watu wa Mataifa,
niifanyie Injili ya Mungu kazi ya ukuhani, kusudi Mataifa wawe sadaka yenye
kibali, ikiisha kutakaswa na Roho Mtakatifu,” Rum 15:16. Mtume Paulo kesha
gundua sababu ya furaha yake, na msukumo wa ndani wa maisha yake.
Ndugu yangu tunayesafiri zote katika tafakari hii hatuwezi
kuifikia hatua aliyoifikia Mtume Paulo kama hatujampata Kristo na kuwa sababu
ya kila kitu katika maisha yetu. Je, yanitosha kuona fahari katika Kristo kwa
vile tu nilibatizwa na leo naishi agano kama mlei kwa sakramento ya Ndoa, Mtawa
kwa maisha ya Wakfu, na Mtawa na Mkleri kwa maisha ya wakfu na sakramenti ya
Daraja Takatifu? Je, vile nilivyo leo yatosha? Ndugu yangu, Kristo anakuwa
sababu ya kila kitu katika maisha yako unapooshwa kwa kuzaliwa kwa pili na
kufanywa upya na Roho Mtakatifu. Kuzaliwa huku wa pili si tokeo la matendo yako
ya haki uyatendayo. Ila ni utayari wa kumpokea na kumruhusu Kristo na Roho Mtakatifu
kufanya kazi ndani yako. Hivyo, “wema wake Mwokozi wetu Mungu, na upendo wake
kwa wanadamu, ulipofunuliwa, alituokoa; si
kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa
kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu,” Tit
3:4-5. Tokeo la utayari huu wa kukubali
kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili katika maisha yetu huwa sababu na kielelezo cha kuhesabiwa haki na kuurithi uzima wa milele, Tit 3:7.
Mara nyingi baadhi yetu hupenda sana kujilinganisha na
kujifananisha na yale tuyafanyao na kusahau kwamba kwa kubaki tu kwenye hayo na
hali hiyo kwa yanayoonekana na yasiyodumu tunapoteza sababu na malengo ya
masisha yetu hapa duniani. Hata kama wayatenda vyema hayo uyafanyayo, kamwe
yasichukue nafasi ya Kristo katika maisha yako. “Maana sitathubutu
kutaja neno asilolitenda Kristo kwa kazi yangu, Mataifa wapate kutii, kwa neno
au kwa tendo, kwa nguvu za ishara
na maajabu, katika nguvu za Roho Mtakatifu,” Rum 15:18-19a. Ndugu yangu, chochote
kisichokuwa na kibali kutoka kwa Mungu hakidumu na hakina umilele. “Bali kama vile tulivyopata kibali kwa Mungu tuwekewe amana
Injili, ndivyo tunenavyo; si kama wapendezao wanadamu, bali wampendezao Mungu
anayetupima mioyo yetu,” 1The 2:4. Je, wajua ipo siku itakupasa kutoa hesabu
mbele ya Mungu kwa hiki unachoishi leo? Je, umejiandaa kwa lipi mbele zake
Mungu uku ukijua wazi ndani ya dhamiri yako kwamba unachokifanya na ulicho hakina kibali chake?
Wapendwa katika
Kristo, Injili ya leo inatupatia hali halisi kuhusu hesabu yetu siku ya mwisho.
Yesu analisema jambo hilo akitolea mfano wa Tajiri mmoja na Wakili wake
dhalimu. Bila kujua siku wala saa,
Wakili huyu dhalimu anatakiwa na Tajiri yake kutoa hesabu ya uwakile wake,
baada ya Tajiri yake kupata habari ya kutapanywa kwa mali zake. Alichokifanya
kwa haraka Wakili yule ni kurejesha uhusiano wa haraka na wateja zake ambao
ndio hatma ya maisha yake kwa sasa. Katika jambo hili ilimpasa kutoa msamaha wa
madeni bila kuhathiri utajiri wa Tajiri yake. Hivyo, “Yule bwana akamsifu wakili dhalimu kwa vile alivyotenda kwa
busara; kwa kuwa wana wa ulimwengu huu katika kizazi chao wenyewe huwa na
busara kuliko wana wa nuru,” Lk 16:8. Kwa kuyasema haya, Yesu anatuacha na swali
la zito la kujibu. Swali hilo ni hili: Mimi na wewe tunasubiri nini kurejesha
uhusiano wetu na Mungu kwa muda na nafasi tuliyonayo sasa tukiwa bado kwenye
nuru, yaani, kwa ubatizo wetu na agano letu katika maisha, iwapo Wakili huyu na
udhalimu wake aliweza kurejesha uhusiano wake na wateja zake? Wokovu ndiyo sasa.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Bwana asema hivi, Shikeni hukumu, mkatende haki; kwa maana
wokovu wangu u karibu kuja, na haki yangu kufunuliwa,” Isa 56:1
No hay comentarios:
Publicar un comentario