ALHAMISI WIKI YA 31 YA MWAKA-B
5/11/2015
Somo: Rum 14:7-12
Zab: 27:1abcde, 4, 13-14
Injili: Lk 15:1-10
Nukuu:
“Kwa sababu hakuna mtu
miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake,” Rum
14:7
“Kwa maana kama
tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama
tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:8
“Maana Kristo alikufa
akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia,” Rum 14:9
“Lakini wewe je! Mbona
wamhukumu ndugu yako? Au wewe je! Mbona wamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi
sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu,” Rum 14:10
“Basi ni hivyo, kila
mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu,” Rum 14:12
“Basi watoza ushuru
wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia wamsikilize. Mafarisayo na waandishi
wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao,”
Lk 15:1-2
“Nawaambia, Vivyo
hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye,
kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao hawana haja ya kutubu,” Lk
15:7
“Nawaambia, Vivyo
hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja
atubuye,” Lk 15:10
TAFAKARI: “Acha njia zako ovu changua uzima nawe uishi milele.”
Wapendwa wana wa Mungu, uovu wowote ule hauendani na wema na
uzuri wa Mungu. Kama sisi wanadamu ni ufukufu na furaha ya Mungu, uovu ndani
yetu hutufifisha sisi wenyewe na kutuweka mbali kabisa na utukufu na furaha ya
Mungu. Uovu wa mwanadamu ni kujikataa mwenyewe kuliko wazi, na kuukataa utukufu
na furaha ya Mungu iliyo ndani yake, yaani ile chapa ya sura na mfano wa Mungu,
Mwa 1:26. Uovu huu ni kujihesabia haki pasipo haki. Binadamu bila Mungu ni sawa
na samaki bila maji. “Kwa sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake,
wala hakuna afaye kwa nafsi yake,” Rum 14:7.
Mtu akisha jihalalishia uovu fulani, hali ile umtia kiburi na upofu. Je,
muhimili wa maisha yako upo wapi?
Moja ya mizania ya kweli
na haki kwa viumbe vyote licha ya hali na nafasi tulizonazo ni kifo. Hata
pamoja na ukweli huu, mtu aliyepigwa upofu na kiburi kinachotokana na
kuhalalisha uovu, hakosi kujiinua. Basi ni vyema hata kama huamini hakuna Mungu
na Mbingu kwa sababu vyote vya ulimwengu huu kwa kiburi chako unavipata,
kinyenyekeshe basi kwa kujua kuwa lazima utakufa. Pamoja na maendeleo ya
sayansi na teknolojia ya leo, bado kifo hakizuiliki wala hakitabiriki. Kwa hiyo
kama umezaliwa kweli na unaishi leo na sasa kifo kipo. Kifo ni kivuli cha mwili
wako na hivyo unacho muda wote. Ni wakati tu ukifika nalo litatendeka.
Ndugu yangu, kifo chako na
hasa kama u mfuasi wa Kristo, hakitakuwa na maana bila Kristo. “Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa,
twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum
14:8. Je, bila Kristo kifo chako kina umaana yoyote? Jambo la muhimu kujua ni
hili; kufa kwako kuna maana tu kama kuishi kwako kuna maana na kulikuwa na
maana na Kristo. Kuishi katika maana ya Kristo ni kuishi kwa kufafana na
Kristo. Tunaishi kwa kufafana na Kristo tunapoishi katika ufalme wake wa kweli
na uzima, ufalme wa utakatifu na wa neema, ufalme wa haki, mapendo na amani.
Je, maisha yako ya leo na sasa yanatoa taswira katika maana niliyosema?
Licha ya
kwamba tunajua ipo siku kutakufa, ila kifo hicho kitakuwa na maana tu tukiishi
au tukifa tu mali ya Bwana. “Maana Kristo alikufa
akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia,” Rum 14:9.
Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, kesho yetu katika maisha ya
umilele na Mungu haitakuwa matokeo ya sifa zetu, madaraka yetu mabaya na ya
uonevu kwa wanyonge, akili zetu za ujanja ujanja wa kuzikanyaka haki za watu,
wala umaarufu wetu. Kesho yetu katika uzima wa milele ni matokeo ya kuishi leo
yetu katika ufalme wa kweli, utakatifu na wa neema, haki, mapendo na amani
kwetu sisi na kwa watu wote. Haya ndiyo makusudi ya Mungu kuviweka viumbe vyote
chini ya utawala wake Kristo ambaye amemtolea Mungu Mkuu ufalme wa milele na wa
ulimwengu wote.
Kama hili
nilisemalo lina sema chochote juu ya maisha yako, “Lakini wewe je! Mbona
wamhukumu ndugu yako? Au wewe je! Mbona wamdharau ndugu yako? Kwa maana sisi
sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu,” Rum 14:10. Ndugu yangu,
tutawezaje kusimama katika kiti hiki cha hukumu cha Mungu kama ishi yetu leo
siyo ishi yetu na Kristo? Tunayo nafasi moja tu kwa sasa. Ili kumrudishia Mungu
utukufu wake na furaha yake tuliyoififisha kwa uovu wetu ni kufanya toba ya
kweli na majuto. Huu ndio wito wa injili yetu ya leo.
Katika
Injili ya leo, Yesu anatoa wito huo kwa kutupatia mifano miwili yenye kuonyesha
furaha ya Mungu tunapomrudia baada ya kutambua njia ya uzima aliyotuandalia;
Mfano wa kwanza, ni mtu mwenye kondoo mia na kumpoteza mmoja. Naye Yesu
anatuambia, “Vivyo hivyo kutakuwa na furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye
dhambi mmoja atubuye, kuliko kwa ajili ya wenye haki tisini na kenda ambao
hawana haja ya kutubu,” Lk 15:7. Mfano
wa pili ni huu wa mwanamke yule mwenye shilingi kumi akapoteza moja. Naye Yesu
anatuambia, “Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya
mwenye dhambi mmoja atubuye,” Lk 15:10. Shauku
hii ya kutafuta kimoja kilichopotea itusukume kujiweka karibu zaidi na Mungu. “Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki
aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu,
Naye atamsamehe kabisa,” Isa 55:7. Mungu wetu
anamaanisha kweli hili alisemalo, yaani kutusamehe kabisa tunapofanya toba ya
kweli na majuto. Mzaburi anatuambia ukweli huu kwa kusema, “Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni;
Nawe utanijulisha hekima kwa siri, Unisafishe
kwa hisopo nami nitakuwa safi, Unioshe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji,”
Zab 51:6-7. Huyu ndiye Mungu anayependa kuanza upya nawe katika yote licha ya historia yako mbaya ya huko nyuma.
Je, upo tayari kuanza upya na Mungu?
Wapendwa katika Kristo,
usipoteze muda wako mwingi kwa kuziangalia dhambi na uovu wa wenzako ilhali
nawe upo kwenye mtego huo huo. Yesu kuwa karibu na wadhambi kwa mfano daraja na
mpatanishi wetu na Mungu, anaonekana naye mdhambi kadiri ya mitazamo ya
Mafarisayo ambao walipenda kujionyesha wasafi nje ila ndani ni ubatili mtupu. “Basi watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa
wakimkaribia wamsikilize. Mafarisayo
na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi,
tena hula nao,” Lk 15:1-2. Mimi na wewe hatuna tofauti na watoza ushuru na
wenye dhambi. Tunahitaji huruma ya Mungu na msamaha wake.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa maana, Atakaye
kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo
yake isiseme hila. Na aache mabaya, atende mema; Atafute amani, aifuate sana,”
1Pet 3:10-11
No hay comentarios:
Publicar un comentario