viernes, 27 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 34 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 34 YA MWAKA-B
28/11/2015
Somo: Dan 7:15-27
Zab: Dan 3:82-87
Injili: Lk 21:34-36
Nukuu:
Akanena hivi, Huyo mnyama wa nne atakuwa ni ufalme wa nne juu ya dunia, utakaokuwa mbali na falme zile zote, nao utakula dunia yote, na kuikanyaga, na kuivunja vipande vipande,” Dan 7:23

Naye atanena maneno kinyume chake Aliye juu, naye atawadhoofisha watakatifu wake Aliye juu; naye ataazimu kubadili majira na sheria; nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati,” Dan 7:25

Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii,” Dan 7:27 

Basi, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo,” Lk 21:34 

Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu,” Lk 21:36

TAFAKARI: “Tumeumbwa ili tunafanane na Kristo kila siku ya maisha yetu, na kwa kupitia Yeye tuurithi ufalme wa mbinguni.”

Wapendwa wana wa Mungu, licha ya kwamba Mungu alichagua kutuumba kwa sura na mfano wake kwa sifa na utukufu wake, na kutupatia heshima kubwa kuliko viumbe vyote, alipenda pia tuwe na mahusiano naye. Hivyo sababu ya tatu ya kuumbwa kwetu, Mungu anapenda tufanane na mwanaye Yesu Kristo ili kwa kupitia Yeye tuurithi uzima wa milele. Ni jukumu la kila mbatizwa kila siku ya maisha yake kufanana na Kristo kwa sababu, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:10-12. Hivyo maisha yetu hapa duniani siyo maisha ya anasa na furaha tu kwa sababu hakuna mbingu hapa duniani.

Katika Injili ya leo Yesu anatupa angalizo kuhusa maisha yetu hapa duniani. Naye anasema, jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo,” Lk 21:34. Kwa vile hatuijui siku ya kiama yetu, yatupasa kuwa macho huku taa zetu zikiwa zinawaka kama wale wanawali watano wenye busara, Mt 25:4. Katika kile kituo cha tisa katika simulizi la mateso ya Yesu, njia ya msalaba, tunaambiwa kwamba Yesu anaanguka mara ya tatu. Moja ya mateso tunayomzidishia Yesu ni dhambi hii kama sala isemavyo, “mara nyingi mno ninajibovusha kwa kupenda mno starehe, anasa na tafriji.” Maisha yetu hapa duniani ni mafupi sana ukilinganisha na maisha ya umilele. Kila mmoja wetu anapaswa kuyapa maisha haya kipaumbele akilenga maandalizi ya maisha ya umilele. Katika jambo hili Yesu anatuambia, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika haya yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu,” Lk 21:36. Kukesha huku ni kufanana na Kristo kila siku kwa kutenda mema na kuishi utakatifu ule aliouishi ukijipokea kama ulivyo binadamu. Kuishi kama Kristo ni kuishi katika maisha ya utakaso. Ni kurejesha ile sura na mfano wa Mungu ndani yetu ilipotezwa na kuchakazwa na dhambi. Huu ndio ufalme aliokuja kuusimika Yesu Kristo duniani, yaani, kurudisha taswira ile ya Mungu ndani ya mioyo ya wanadamu.

Kazi hiyo ya Yesu inafunuliwa katika ndoto ya Nabii Danieli miaka mingi kabla. Akanena hivi, Huyo mnyama wa nne atakuwa ni ufalme wa nne juu ya dunia, utakaokuwa mbali na falme zile zote, nao utakula dunia yote, na kuikanyaga, na kuivunja vipande vipande,” Dan 7:23. Kazi yake ya kwanza ni kuushinda uovu kwa wema. Nasi kila moja kwa nafasi na wito wake kama mbatizwa analo jukumu hilo, kuushinda uovu kwa kutenda mema. Hivyo kwa kushirikishwa kazi hii ya ukombozi kila mmoja kwa nafasi yake, na kuitenda kwa uaminifu na uadilifu, ndipo  utakapokuwa utakatifu wa kila mmoja wetu. Ni kutoa ushuhuda wa kweli katka maisha ya kawaida ya kila siku kwa kila mmoja kadiri ya nafasi na wito wake. Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii,” Dan 7:27.

Ndugu yangu, kwa nguvu zetu na maarifa yetu hatuwezi kamwe kuwa kama Yesu pasipo msaada ya Roho Mtakatifu. Twamwitaji Roho Mtakatifu kutuongoza na kutufunulia yale yaliyojificha katika maisha yetu. Roho huyu atatuongoza na kufanya njia pale pasipo na njia. 

Tumsifu Yesu Kristo!


Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17

No hay comentarios:

Publicar un comentario