JUMANNE WIKI YA
32 YA MWAKA-B
10/11/2015
Somo: Hek
2:23-3:9
Zab: 34:2-3,
16-17, 18-19
Injili: Lk
17:7-10
Nukuu:
“Yaani, Mungu alimwumba mwanadamu ili
apate kutokuharibika, kwa mfano wake mwenyewe, ila ulimwengu uliingiwa na mauti
kwa husuda yake Shetani, nao walio wa upande wake hupata kuionja,” Hek 2:23-24
“Bali roho zao wenye haki wamo mkononi
mwa Mungu wala maumivu hayatawagusa,” Hek 3:1
“Machoni pa watu walio wajinga
walionekana kwama wamekufa, na kufariki kwao kulidhaniwa kuwa ni hasara yao, na
kusafirikwao kutoka kwetu kuwa ni uharibifu wao; bali wao wenyewe wamo katika
amani,” Hek 3:2-3
“Wakati wa kujiliwa kwao watang’aa, na
kama vimulimuli katika mabua makavu watametameta,” Hek 3:7
“Watahukumu mataifa na kuwatawala
kabila za watu, naye Bwana atawamiliki milele na milele,” Hek 3:8
“Wenye kumtumaini watafahamu yaliyo
kweli, na waaminifu watakaa naye katika upendo; mradi neema na rehema zina
wateule wake,” Hek 3:9
“Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote
mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa
kufanya,” Lk 17:10
TAFAKARI: “Kwa
unyenyekevu tenda na ishi lililo haki, simama daima katika kweli.”
Wapendwa wana
wa Mungu, matendo mema ya mtu hujionyesha katika unyenyekevu wake. Unyenyekevu
wa mtu si katika mwono wa kuyachukulia yote sawa hata pale hali siyo sawa, bali
ni unyenyekevu katika haki na kweli. Ninapotambua wajibu wajibu wangu
nitajitahiji kuutimiza katika kweli na haki. Je, kulifanya hili ni rahisi? La
hasha! Nalifanya hilo kwa sababu ndiyo njia sahihi ya kufanya na haki kwangu na
wenzangu, na hili ndilo alipendalo Mungu. Hivyo nipo tayari kuyapokea yote
katika kweli na haki bila masikitiko kwa sababu ndani yake kuna uzima wa milele
na makusudi ya Mungu katika kuniumba kwangu. Nimeumbwa ili niishi milele.
Ni katika umilele huu ndugu yangu,
“Mungu alimwumba mwanadamu ili apate kutokuharibika, kwa mfano wake mwenyewe,
ila ulimwengu uliingiwa na mauti kwa husuda yake Shetani, nao walio wa upande
wake hupata kuionja,” Hek 2:23-24. Salama yetu katika hili ipo pale tunapoishi
katika roho ya kweli na haki. “Bali roho zao wenye haki wamo mkononi mwa Mungu
wala maumivu hayatawagusa,” Hek 3:1. Ukweli ni kwamba katika ulimwengu huu wa
ushindani hakuna anayekubali kwa urahisi hali yake na kujichukulia kwa unyenyekevu
kuanza upya akijitazama nguvu na vipawa vyake. Mara nyingi tunajitazama katika
maono ya zaidi ya kile tulicho na mwisho wake tunaangukia pua. Maumivu ya
kuangukia pua ni makali sana. Ila wengi wetu tupo moyo radhi kuyapata maumivu hayo kuliko kuupokea
ukweli uliopo ndani yake kwa kujipokea katika madhaifu yetu. Huwezi kamwe
kusonga mbele kama huyaoni mapungufu yako. Licha ya kwamba kuna uwezekana wa
wewe kuwa mtakatifu, yakupasa kujua kwa sasa wewe si malaika wala mtakatifu.
Wewe ni binadamu na kwa kuishinda huo ubinadamu wako Mungu mwenyewe atakufanya
kuwa mtakatifu kwa mastahili yake.
Kwa kuupokea unyenyekevu huu wa
kuukubali ubinadamu wako, ujiandae kwa dhihaka kutoka kwa wapinzani wako.
Ukweli ni kwamba wenye kusimama katika kweli na unyonge wao, “Machoni pa watu
walio wajinga walionekana kwama wamekufa, na kufariki kwao kulidhaniwa kuwa ni
hasara yao, na kusafirikwao kutoka kwetu kuwa ni uharibifu wao; bali wao
wenyewe wamo katika amani,” Hek 3:2-3. Je, lipi lililo jema? Je, ni rafiki yako
anayekupigia makofu bila kujua undani wako au Mungu anayekuhesabia haki katika
kweli na haki? Kumbe ni vyema kusimama katika kweli na haki kwa sababu
hakimu yetu Mungu hana upendeleo.
Ndugu yangu unayesafiri nami katika
tafakari hii, elewa jambo hili; mwisho wako wa kusimama katika lililo kweli na
haki ndiyo furaha na utukufu wa Mungu wetu wa haki na kweli. Tutakuwa
wakamilifu kama Mungu alivyo mkamilifu, Mt 5:48, tukitenda yale yanayofanana na
Mungu. Hivyo kwenye kuishi katika kweli na haki, “Wakati wa kujiliwa kwao
watang’aa, na kama vimulimuli katika mabua. Hii ndiyo furaha tuipatayo kwa
Mungu wetu aliye hai, kweli na haki. Na kwa sababu hiyo, “Wenye kumtumaini
watafahamu yaliyo kweli, na waaminifu watakaa naye katika upendo; mradi neema
na rehema zina wateule wake,” Hek 3:9. Je, nifanye nini basi ili nikae katika
upendo wa Mungu?
Wapendwa wana wa Mungu, lazima nielewe
kwamba tendo lolote nilifanyalo lapaswa kuongozwa na unyenyekevu wangu. Nielewe
nayafanya haya kwa sababu yanipasa kuyafanya tena kwa umakini mkubwa nikitimiza
nafasi yangu kama initakavyo kufanya kwa sifa na utukufu wa Mungu. Ni katika
ukweli huu Yesu anatuambia, “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote
mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa
kufanya,” Lk 17:10. Tutajisikia hali hii pale tu tunaposhinda kujifananisha na
kujilinganisha na yale tuyafanyayo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Basi, kwa kuwa
mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu
wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu,” Kol
3:12
No hay comentarios:
Publicar un comentario