lunes, 2 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 31 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 31 YA MWAKA-B
3/11/2015
Somo: Rum 12:5-16ab
Zab: 131:1abcde, 2, 3
Injili: Lk 14:15-24
Nukuu:
“Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha,” Rum 12:6-8

Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema,” Rum 12:9
Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani,” Rum 12:14 

Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge,” Rum 12:16

Bwana akamwambia mtumwa, Toka nje uende barabarani na mipakani, ukawashurutishe kuingia ndani, nyumba yangu ipate kujaa,” Lk 14:23

Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu,” Lk 14:24 

TAFAKARI: “Je, Mungu ana nafasi gani katika maisha yangu?”

Wapendwa wana wa Mungu, kinachochukua muda mwingi katika maisha yako ndicho hatma ya maisha yako. Jaribu kuyatazama maisha yako, hasa mzunguko wa kila siku na uchambue ni kitu gani kinachochukua muda wako wingi na upime kama kitu hicho ni kielelezo cha maisha yako ya umilele. Kama kitu hicho hakina mwelekeo wa maisha ya umilele na yenye kubeba taswira ya ufufuko, nakusihi ubadili njia na mpango mzima wa maisha yako ukitafuta yaliyo juu Kristo aliko. Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Kuyatafuta yaliyo juu Kristo aliko ni kutambua kwa undani mambo makuu mawili: kwanza, tafakari kwa undani kitu cha kufanya kwa ajili ya Yesu kama shukrani kwake kwa kukukomboa na kukuweka huru kutoka utumwa wa dhambi. Na pili, fikiria mtumizi sahihi ya vipaji alivyokujalia Mungu kwa ajili ya wengine. Bila shaka ukiyafanya haya Mungu atakuwa na nafasi ya kwanza katika maisha yako.

Kwa upande wa vipaji na karama Mungu alizokujalia, elewa kwamba karama hizo ni kwa kufaidiana. Kwa maana nyingine, yakupasa kupungua ili Kristo aongezeka. Na hiyo ndiyo furaha ya Kristo.  Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30. Kama Kristo aliyopungua ili Mungu ajulikane kwa watu kupitia yeye, nasi yatupasa kupungua ili Kristo aonekane katika maisha yetu na wale wote wanaotuzunguka na wenye hofu ya Mungu. Hivyo karama na vipaji alivyotukirimia Mungu kwa upendo wake tuvitoe kwa wengine bila ya kujibakiza.

Kama ni unabiii tuutoe kwa Imani kweli pasipo shaka bila hofu. Ndugu yangu, kama kitu ni cheupe sema waupe wake, na kama ni cheusi sema weusi wake. Mkristo aliyebatizwa na kushirikishwa mambo makuu matatu, yaani unabii, ukuhani na ufalme wa Kristo kisha akakaa kimya bila kusema chochote na kufanya chochote anapoona haki za watu zinakanyagwa anausaliti unabii wake na ukristo wake. Hatupaswa kuwa bendera fuata upepo. Tusimame imara katika kweli na haki hata kama kuna upepo au hakuna upepo. Hivyo “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha,” Rum 12:6-8. Huku ni kutoa hesabu ya karama na vipaji alivyotupa Mungu kila siku ya maisha yetu.

Wapendwa wana wa Mungu, katika maisha yetu ya kila siku yatupasa kupiga vita uovu wa aina yoyote ile. Kuupiga vita uovu ni kuwa na mahusiano mazuri;  kwanza na nafsi yako. Pili, na jirani yako. Tatu, na mazingira yako. Na nne,  na Mungu wako. Kwa kuujenga uhusiano huu epuka sana unafiki. Unafiki ni sumu katika mahusiano yetu na hayo niliyoyasema. Kweli tu ndiyo itakayokuweka huru, na upendo ndiyo staha yako. Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema,” Rum 12:9. Hakuna sababu ya kupoteza muda wako kwa mambo ya majungu na yasiyo na tija katika maisha yako. Kuwa mtu wa baraka na neema hata pale unapotendewa ndivyo sivyo kwa sababu wema huushinda uovu. Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani,” Rum 12:14. Ni vyema katika jambo kama hili ukatumia muda wako kwa wahitaji na hasa kujishughulisha na wanyonge na kuwa sauti za wasio na sauti katika jamii inayokuzunguka. Hivyo, Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge,” Rum 12:16. Kwa kufanya hivi utakuwa umetumia muda wako vizuri hapa duniani.

Ulimwengu huu tunaoishi leo ni mwaliko wa  kushiriki wema na furaha ya Mungu. Ni wito wa karamu ya Mungu. Mungu anahitaji uwepo wetu ulio hai bila ya kuwa na udhuru wowote. Kwa maana nyingine tusiyatamani mambo yale yanayowapa furaha watu kwa muda mfupi tu kwa sababu hata wakifa hawaendi nayo. Mzaburi anatuambia jambo hili na kusema, Usiogope mtu atakapopata utajiri, Na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua cho chote; Utukufu wake hautashuka ukimfuata,” Zab 49:16-17. Yakupasa kujali matumizi mazuri ya muda wako ungali hapa duniani. Wapo wengi kati yetu wanapoteza muda wao katika ufahari na mali walizonunua, Lk 14:18. Wapo wengine kati yetu shughuli zao huwa ndio muhimili wa maisha yao, Lk 14:19. Na wapo wengine kati yetu sharehe zao ndiyo kila kitu kwao, Lk 14:20. Ila tuelewe ukweli huu kwamba, nyumbani kwa Mungu wetu kuna nafasi ya kila mmoja wetu. Alituumba kwa sura na mfano wake akijua kila mmoja atakuwa na nafasi endepo tutamwelekea na kufuata maagizo yake. Hivyo kila siku Mungu anatoa mwaliko wa kushiriki naye katika karamu. Bwana akamwambia mtumwa, Toka nje uende barabarani na mipakani, ukawashurutishe kuingia ndani, nyumba yangu ipate kujaa,” Lk 14:23. Furaha ya Mungu ni kuijaza nyumba yake na kushiriki naye katika karamu aliyotuandalia, yaani maisha ya umilele.

Mwisho, Injili ya leo inatupa angalizo kubwa sana. Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu,” Lk 14:24. Maneno haya ya wazi ya Bwana wetu Yesu Kristo yanakulenga wewe na mimi ambao kwa ubatizo wetu ni wazi tumealikwa kuurithi ufalme wa Mbinguni. Ila tutapigwa butwaa kutokuiona mbingu hiyo kwa sababu hatukuishi ahadi zetu za ubatizo. Huku ni kualikwa kwenye karamu ya Mwana Kondoo na kukataa wazi wazi kwa sababu zetu binafsi na zisizo za tija. Katika Injili ya leo tunaona watu watatu walioalikwa kwenye karamu na mwisho walitoa udhuru. Mtu wa kwanza alikuwa amenunua shamba hivyo alitaka aende kulitazama. Wa pili alikuwa amenunu ng’ombe jozi tano hivyo alitaka aende kuwajaribu. Na wa mwisho alikuwa ameo na hivyo hana muda na Mungu zaidi ya mke wake. Je, ni kitu gani kinachokuzui kuwa karibu na Mungu? 

Tusifu Yesu Kristo!


“Bwana yu karibu na wote wamwitao, Wote wamwitao kwa uaminifu,” Zab 145:18

No hay comentarios:

Publicar un comentario