IJUMAA WIKI YA 34 YA MWAKA-B
27/11/2015
Somo: Dan 7:2-14
Zab: Dan 3:75, 76, 77, 79, 80, 81
Injili: Lk 21:29-33
Nukuu:
“Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano
wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku,
wakamleta karibu naye,” Dan 7:13
“Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa
kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka
ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,”
Dan 7:14
“Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba
majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi
kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa
Mungu u karibu,” Lk 21:30-31
“Amin, nawaambieni,
Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote yatimie. Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno
yangu hayatapita kamwe,” Lk 21:32-33
TAFAKARI: “Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe,”
Wapendwa wana wa Mungu, bila shaka neno “WOSIA” siyo geni masikioni
mwako. Wosia ni maneno ya hekima na busara ambaya hutolewa mara chache sana na
mtu ambaye yupo mwisho wa kitu fulani, kwa faida na maarifa ya wale anaowaacha
katika hali fulani. Wosia ni tokeo la mang’amuzi mapana ya maisha ambayo kwayo
kwa pamoja ujumuisha na kutoa tathmini ya yale yaliyopita, ya sasa, na yajayo.
Wosia utolewa mara chache sana kwa sababu siyo wote katika hali yao ya mwisho,
mfano mwisho wa uhai wao, ufunuliwa umauti wao. Wengi hubaatika kutoa Wosia
kutokana na kuuugua kwa muda mrefu na kwa mateso makali, na kwa njia hiyo
ufunuliwa umauti wao. Hata hivyo wapo wengine kutokana na maisha yao ya utulivu
na tafakuri wakichukulia kila jambo na maana yake katika maisha yao, ufunuliwa
pia yale yatarajiwayo kutokea. Hawa nao utoa wosia.
Katika Injili ya leo, Yesu Kristo anatupa wosia kwa yale
yatakayojiri ikiwa ni hitimisho la nyakati. Yesu anatumia mifano ya kawaida
kulingana na mazingira ya watu wake. Katika jambo hili la kusoma alama za
nyakati, Yesu anatumia mfano wa mti aina ya Mtini. Naye anasema, “Wakati iishapo kuchipuka (Mitini), mwaona na kutambua wenyewe ya
kwamba majira ya mavuno yamekwisha kuwa karibu. Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo
yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu,” Lk 21:30-31. Ufalme huu wa Mungu ni ule aliofunuliwa katika
ndoto Nabii Danieli. Ni ufalme ambao utaushinda uovu kwa wema kama tulivyosoma
katika simulizi la ndoto ya Danieli kuhusu wale wanyama. Ni ufalme ulioshuka
kutoka mbingu, yaani, neno kufanywa mwili, kumwilishwa na kukaa kwetu, Yoh
1:14. Hivi ndivyo Danieli alivyofunuliwa katika ndoto: “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja
aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo
mzee wa siku, wakamleta karibu naye,” Dan 7:13.
Ufalme na utawala huu ushasimikwa kuanzia pale ilipoaanza
safari nzima ya wokovu wa mwanadamu, neno kufanyika mwili na kukaa kwetu,
mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu. Huu ni ukweli usiopitwa na wakati. “Amin, nawaambieni, Kizazi hiki hakitapita hata hayo yote
yatimie. Mbingu na nchi zitapita,
lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” Lk 21:32-33.
Ukweli huu wa neno kutokupitwa na wakati ulishafunuliwa pia kwa njia ya ndoto
aliyooteshwa Nabii Danieli. Hapa Danieli anamzungumzia Kristo Yesu, mmoja aliye
mfano wa mwanadamu aliyekuja na mawingu ya mbingu na kusema, “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa
kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka
ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa,”
Dan 7:14. Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii, wewe upo katika
ufalme upi?
Wapendwa katika Kristo, kuwa katika ufalme wa Kristo ni kufanana na Kristo katika
kufikiri, kuona, kutenda, na kuishi. Yesu anatuambia sote kwamba, “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane
mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate,” Lk 9:23. Zeozi au mtihani
huu wa maisha si wa mara moja tu, bali
kila siku ya maisha yetu. Na kuwa kweli mwanafunzi wa Yesu ni kuuchukua msalaba
na kumfuata Yesu. Yesu analisema jambo hili wazi kabisa bila kuficha kitu. Naye
anasema, “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu,
hawezi kuwa mwanafunzi wangu,” Lk 14:27. Je, waufahamu msalaba wako? Tazama
vilema vyako! Tazama udhaifu wako! Tazama changamoto zako katika maisha agano
unayoyaishi leo na sasa!
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa kuwa vitu vyote
vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye
milele. Amina,” Rum 11:36
No hay comentarios:
Publicar un comentario