martes, 1 de diciembre de 2015

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 1 YA MAJILIO MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 1 YA MAJILIO
2/12/2015
Somo: Isa 25:6-10a
Zab: 23:1-3a, 3b-6
Injili: Mt 15:29-37
Nukuu:
Na katika mlima huu Bwana wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana,” Isa 25:6 

Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana Bwana amenena hayo,” Isa 25:8

Katika siku hiyo watasema, Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, Ndiye tuliyemngoja atusaidie; Huyu ndiye Bwana tuliyemngoja, Na tushangilie na kuufurahia wokovu wake,” Isa 25:9

Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya,” Mt 15:30

Yesu akawaita wanafunzi wake, akasema, Nawahurumia mkutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije wakazimia njiani,” Mt 15:32 

Wanafunzi wake wakamwambia, Tupate wapi mikate mingi hapa nyikani, hata kushibisha mkutano mkuu namna hii?” Mt 15:33

Yesu akawaambia, Mnayo mikate mingapi? Wakasema, Saba, na visamaki vichache,” Mt 15:34 

akaitwaa ile mikate saba na vile visamaki, akashukuru akavimega, akawapa wanafunzi wake, nao wanafunzi wakawapa makutano,” Mt 15:36

Wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate makanda saba, yamejaa,” Mt 15:37 

TAFAKARI: “Mnayo mikate mingapi? Mungu wetu aliye hai habariki utupu.”

Wapendwa wana wa Mungu, kila mmoja wetu hupenda baraka na hata kubarikiwa na Mungu kwa yale anayoyafanya na yale anayoyatamani kuyapata. Ila ukweli ni kwamba Mungu wetu huyu aliye hai kamwe habari utupu. Lazima kuwe na ushirikiano wako na Yeye kwa kila unachokiomba naye atakibariki. Yesu anasema, Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang'anywa hata alicho nacho,” Lk 19:26. Maneno haya ya Yesu yanatimia katika Injili ya leo ambapo tunaona Yesu baada ya kuwalisha makutano kiroho kwa neno la uzima anaona uhitaji wao wa kulishwa kimwili. Yesu akawaita wanafunzi wake, akasema, Nawahurumia mkutano, kwa kuwa yapata siku tatu wamekaa pamoja nami, wala hawana kitu cha kula, tena kuwaaga wakifunga sipendi, wasije wakazimia njiani,” Mt 15:32. Huyu ndiye Mungu anayeyajua mahitaji yetu ya mwili na roho.

Wapendwa katika Kristo, maneno hayo ya Yesu yanawatia hofu wanafunzi wake. Hivyo Wanafunzi wake wakamwambia, Tupate wapi mikate mingi hapa nyikani, hata kushibisha mkutano mkuu namna hii?” Mt 15:33. Je, ni kweli kwamba Wanafunzi wake Yesu hawakuwa na chochote ili kibarikiwe? Mungu wetu aliye hai habariki utupu! Yesu akawaambia, ‘Mnayo mikate mingapi?’ Wakasema, Saba, na visamaki vichache,” Mt 15:34. Je, ndugu yangu umeelewa kwa nini baraka na neema hazikufikii? Je, umetoa hata hicho kidogo ulichokuwa nacho Mungu akibariki? Je, umefanya juhudi yoyote katika tatizo au hitaji lako ili Mungu atie mkono wake wa baraka? Pasipo chochote na utayari wowote kutoka kwako uwezi pata chochote kutoka kwa Mungu kwa sababu haujua hata kile utakacho au uombacho. Kwa maana hivyo, kama tunaomba basi tunaomba vibaya! Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3.

Mungu hubariki shughuli na juhudi zetu na siyo utupu. Ukweli huu tunauona katika muujiza wa kwanza wa Yesu kule Kana, Yoh 2:1-11. Katika muujiza huu tunaona jinsi ambavyo Yesu alivyoyabariki maji na kuwa divai baada ya Mama Bikira Maria kutoa taarifa kwa Mwanaye akiamini hata mwangusha, na baadaye kuwaamuru wale watumishi wa ile Harusi wayajaze maji yale mabalasi sita ya mawe. Mkuu wa Meza alimwita Bwana Harusi na kumwambia, Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa,” Yoh 2:10. Baraka ya Mungu haina kikomo tutimiza yale yanayotupasayo kufanya.

Wapendwa wana wa Mungu, Mungu hukibariki hata kile kidogo tulichonacho tunapokikabidhi chote kwake. Hili nalo tunaliona kule Sarepta, 1Fal 17:10-16, ambapo Mama yule mjane akiwa na mtoto wake wakisubiri kula kilichobaki na kufa. Hapa anatokea Nabii Eliya na kumwamuru mjane yule akitoe kile kilichobaki na kumwandalia “kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi,” IFal 17:14. Mwisho wa baraka na neema za Mungu ni mwanzo neema na mwendelezo wa baraka za Mungu. Ukweli huu tunauona katika Injili ya leo kwamba, wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate makanda saba, yamejaa,” Mt 15:37. Huyu ndiye Mungu atendaye maajabu kwa wale wote walimridhia pasipo shaka yoyote.

 Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, tupo kwenye kipindi cha Majilio. Bila shaka kila moja wetu anahitaji lake na mahangaiko yake ambayo yanaelekea kukuchosha. Basi ni wakati wa pekee kufanya tafiti moyo ili uweze gundua ni wapi hujatoa ushirikiano wa kutosha na Mungu. Ujio wa Masiha ni agano la kweli na haki linalotoa fursa ya kuanza upya na Mungu. Yeye, yaani Masiha, hatatazama historia yako mbaya na ukale wako, ila atatazama zaidi utayari wako wa kuanza naye katika upya. Nawe utakuwa mpya tu utakapokuwa tayari kufanya toba ya kweli na majuto. Kutana na Mungu katika Mlima huo wa Sayuni yako Mpya, yaani utayari wako wa kuanza upya naye. Na katika mlima huu Bwana wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana,” Isa 25:6. Je, inakugharimu nini ndugu yangu kufanya toba ya kweli na majuto?

Masiha tunayemsubiri ambaye kwa hakika anakuja kwa nia ya kutukomboa kutoka hali yetu duni iliyokomazwa na kuzeeshwa kwa sababu ya dhambi, ndiye atakaye meza mauti yetu na kuyafuta machozi yetu. Amemeza mauti hata milele; na Bwana MUNGU atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana Bwana amenena hayo,” Isa 25:8. Neno la Mungu ni uzima na halipotei bure unapoliamini mara alitamkapo Mungu. Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani,” Yoh 5:24. Ndugu yangu bado una mashaka?

Ikiwa ujio wa Masiha wetu ni kuujenga uhusiano ulibomolewa na dhambi zetu, yanipasa kuanza kuujenga uhusiano mwema ndani ya nafsi yangu mwenyewe, ndugu na majirani zangu, na mazingira yanayonizunguka. Masiha ajale ni mkombozi mwenye kujenga mahusiano mema na watu wote na mataifa yote. Na Katika siku hiyo watasema, Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, Ndiye tuliyemngoja atusaidie; Huyu ndiye Bwana tuliyemngoja, Na tushangilie na kuufurahia wokovu wake,” Isa 25:9. Tutashangilia na kufuraha kwa sababu kutoka kwake tutapata uzima, kuponywa maradhi yetu, tutatembea kwa kuponywa ulemavu wetu, tutaona kwa kuponywa upofu wetu, tutaongea kwa kuponywa ububu wetu, na tutasikia kwa kuponywa uziwi wetu. Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya,” Mt 15:30. Je, ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii hupendi kuongea na masiha kuhusu mkwamo wako kimaisha? Je, hupendi kutembea naye katika uzima wa milele? Je, hupendi kuona utukufu wake? Je, hupendi kuongea ukilisifu jina lake? Na, Je! Hupendi kusikia habari njema ya wokovu anayokuletea?  Mimi napenda na nitakaa naye kwani Yeye ndiye Mzabibu wa kweli nami ni tawi tu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote,” Yoh 15:5

Tumsifu Yesu Kristo!


Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake,” 1Yoh 4:16

No hay comentarios:

Publicar un comentario