IJUMAA WIKI YA 33 YA MWAKA-B
20/11/2015
Somo: 1Mak 4:36-37, 52-59
Zab: 1Nya 29:10bcd, 11abc, 11d-12, 12bcd
Injili: Lk 19:45-48
Nukuu:
“sasa adui zetu wamevunjwa nguvu, basi tupande tukapatakase
mahali patakatifu na kupatabaruku,” 1Mak 4:36
“Kulikuwa na furaha kubwa kwa watu, na aibu ililetwa na
mataifa iliondolewa,” 1Mak 4:58
“Yuda na ndugu zake, na jamii yote ya Israeli, walikata
shauri ya kuwa siku za kuitabaruku
madhabahu ziadhimishwe kwa furaha na shangwe kila mwaka kwa wakati wake, muda
wa siku nane tangu ishirini na tano ya mwezi Kislevu,” 1Mak 4:59
“akiwaambia, Imeandikwa, Nyumba yangu itakuwa nyumba ya
sala; lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Lk 19:46
“Naye akawa akifundisha kila siku hekaluni. Lakini wakuu wa
makuhani, na waandishi, na wakuu wa watu walikuwa wakitafuta njia ya
kumwangamiza,” Lk 19:47
TAFAKARI: “Na kilichowekwa wakfu na kibaki kwa ajili hiyo daima.”
Wapendwa wana wa Mungu, wakfu ni hali au namna ya kujitenga
kwa ajili maalumu na yenye malengo na uhusiano na Mungu. Ni tendo la
kujisalimisha binafsi. Kwa maneno mengine ndiyo kuabudu kwenyewe. Kilichowekwa
wakfu huwa kwa ajili ya matumizi yenye uhusiano na Mungu. Kitu hicho huwa ni
kwa ajili ya Mungu. “Kila kitu kilichowekwa wakfu katika Israeli kitakuwa chako,” Hes
18:14. Hekalu au nyumba ya kuabudia na vilivyomo ndani yake huwekwa wakfu kwa
matumizi hayo tu. “Na wana wa Israeli, na makuhani na Walawi, na watu wengine
katika hao waliohamishwa, wakaiweka wakfu nyumba ya Mungu kwa furaha,” Ezr
6:16. Ni kwa mwono huu na hitaji hili
tunaona katika somo la kwanza Yuda na ndugu zake wanatambua uhumuhi wa sehemu
ya kuabudu na kutolea sadaka za kuteketezwa ambayo hawakuwa nayo walipokuwa
chini ya maadui zao. “Sasa
adui zetu wamevunjwa nguvu, basi tupande tukapatakase mahali patakatifu na
kupatabaruku,” 1Mak 4:36. Lazima wapatakase na kupatabaruku kwa sababu
walinajisiwa na kutumika visivyo.
Tendo hili la kuurudisha tena uhusiano na Mungu ni tendo la
furaha na historia. Hali hiyo inawakuta Yuda na ndugu zake. “Kulikuwa na furaha
kubwa kwa watu, na aibu ililetwa na mataifa iliondolewa,” 1Mak 4:58.
Unaporudisha uhusiano na Mungu uliopotea ni tendo la kuanza upya na Mungu na
kuweka mikakati yenye malengo ya hai na yenye kubeba umilele ndani yake. Hivyo,
“Yuda na ndugu zake, na jamii yote ya Israeli, walikata shauri ya kuwa
siku za kuitabaruku madhabahu
ziadhimishwe kwa furaha na shangwe kila mwaka kwa wakati wake, muda wa siku
nane tangu ishirini na tano ya mwezi Kislevu,” 1Mak 4:59. Kusherehekea matukia
yenye uzima wa Imani ndani yake ni kusheherekea uhai.
Umuhimu wa kile kilichowekwa wakfu na kwa ajili ya matumizi
rasmi yaliyotengwa na ajili hiyo tunaona kwenye injili ya leo. Yesu anaingia
hekaluni na kukuta yatendwayo hayaendani na kile kipasacho kutendwa kwenye
hekalu. Naye anawaambia, “Imeandikwa, Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala;
lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi,” Lk 19:46. Nyumba ya Mungu
pamoja na kutolea sadaka na shukrani zetu ni nyumba ya sala. Yote yale
yasiyokuwa na uhusiano wa sala, shukrani, sadaka, na mengine kama hayo,
hayapaswi kufanyika mahali hapa. Kabla ya kuteswa, kufa, na kufufuka kwake
Bwana Yetu Kristo alijiweka wakfu kwa ajili yetu na kutufanya kuwa viungo vyake
akiwa yeye ndiye Mwili, yaani Kanisa. “Na kwa ajili yao
najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli,” Yoh 17:19. Kanisa
kama mwili wa Kristo, ni kwa namna hiyo ya kutakaswa kupitia sakramenti ya
ubatizo nasi tunakuwa viungo vya Kristo. “Maana kama vile mwili
ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi,
ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Basi
ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake,” 1Kor 12:12,
27. Kwa maana hii, miili yetu imewekwa wakfu ndani na katika Kristo. Hivyo
matendo yote machafu katika mwili ni kwenda kinyume na kutengwa huko kuliko
wekwa kwa ajili ya Kristo. “Je! Hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi
nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha!” 1Kor 6:15.
Wapendwa wana wa Mungu,
pamoja na miili yetu kuwa ni viungo vya Kristo na kuwekwa wakfu kwa ajili ya
Kristo, mwili wa mtu ni hekalu la Roho Mtakatifu. “Au hamjui ya kuwa
mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu?
Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana
mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu,” 1Kor
6:19-20. Ndugu yangu, na kilichowekwa wakfu na
kibaki kwa ajili hiyo daima.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kama mtu akiliharibu
hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu,
ambalo ndilo ninyi,” 1Kor 3:17
No hay comentarios:
Publicar un comentario