JUMATATU WIKI YA 33 YA MWAKA-B
16/11/2015
Somo: 1Mak 1:10-15, 41-43, 54-57, 62-63
Zab: 119:53, 61, 134, 150, 155, 158
Injili: Lk 18:35-43
Nukuu:
“Hata hivyo wengi katika Israeli walikaza nia zao kwa
uthabiti wasile vitu vilivyo najisi. Waliona afadhali kufa kuliko kuitiwa
unajisi kwa vyakula au kulivunja agano takatifu. Wakafa,” 1Mak 1:62-63
“Akapiga kelele, akisema, Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu,”
Lk 18:38
“Basi wale waliotangulia wakamkemea ili anyamaze; lakini
yeye alizidi sana kupaza sauti, Ee Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:39
“Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia,
alimwuliza, Wataka
nikufanyie nini? Akasema, Bwana, nipate kuona,” Lk 18:40-41
“Yesu akamwambia, Upewe kuona; imani yako imekuponya,” Lk
18:42
TAFAKARI: “Dhamiri yako iliyo hai na safi ndiyo ponya yako.”
Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na miongozo mingi
tunayokutana nayo katika jamii tunayoishi, na hata maisha yale tuliyojichagulia
kuishi iwe mlei, mtawa, mtawa na mkleri, “dhamiri yako iliyo hai na safi ndiyo
ponya yako.” Kutokana na uongozi mbaya wa Mfalme Antioko wa Israeli kipindi
kile Makabayo, walikuwepo wayahudi wachache waliosimama katika kweli
iliyoongozwa na dhamiri zao hai na safi bila kuterereka. Mfalme huyu akiwa na
nia ya kushirikiana na mataifa jirani alijikuta anaingia mikataba ya kipagani
na kumwasi Mungu aliye hai na kweli. Hivyo mila na desturi za Kiyahudi
zilipuuziwa na Torati kutokufuatwa na mwisho Sabato kunajisiwa.
Maisha ya Kiyahudi yalionekana kutiliwa mkazo kwenye mambo
makuu matatu; moja, umuhimu wa Hekalu Takatifu kama sehemu pekee ya kuabudu na
kumtokea Mungu shukrani zao na sadaka za kuteketezwa. Pili, Maandiko
Matakatifu, yaani Torati. Na mwisho milki ikiwa ni ardhi pamoja na uongozi
madhubuti uliowekwa na Mungu mwenyewe. Hivyo baada ya Mfalme Antioko kupotoka
na mwenda nje wa yale atakayo Mungu, wapo wayahudi wachache walioapa kutokwenda
kinyume na mwongozo wa Mungu. “Hata hivyo wengi katika Israeli walikaza nia zao
kwa uthabiti wasile vitu vilivyo najisi. Waliona afadhali kufa kuliko kuitiwa
unajisi kwa vyakula au kulivunja agano takatifu. Wakafa,” 1Mak 1:62-63. Hapa
ndipo tunapoona nafasi ya dhamiri hai na safi katika lile lililo kweli na haki.
Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, ni vyema
ukafahamu kuwa hakuna mtu anayeishi mwenyewe kama kisiwa. Tunahitajiana na
kusaidiana katika kukabiliana na mambo mbalimbali katika maisha. Hata hivyo
hitaji hili kamwe lisichukue kile ulicho kilicho hai na safi, yaani, dhamiri
yako, ambayo ndiyo wewe mwenyewe. Maandiko Matakatifu ambayo ni moja ya msingi
na chimbuko la mafundisho yote ya Kanisa Katoliki, yanaongelea ukweli huu kama
tusomavyo kutoka barua ya Mtume Paulo kwa Warumi, “Kwa maana watu wa
Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao
wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya
torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao,
yenyewe kwa yenyewe, yakiwashitaki au kuwatetea; katika siku ile Mungu atakapozihukumu
siri za wanadamu, sawasawa na injili yangu, kwa Kristo Yesu,” Rum 2:14-16.
Dhamiri hai na safi ndiyo ponya yako hata kwa wale ambao hawana habari kuhusu
Kristo.
Wapendwa
katika Kristo, Mungu wetu ni Mungu wa wanadamu wote licha ya tofauti zetu za
kiimani. Hakuna anayeishi katika ulimwengu huu kwa sababu yake mwenyewe. Kila
mmoja wetu anayochapa ya Mungu ndani yake. Ulimwengu huu ukiwemo na vyote
vilivyomo ni Mali yake Mungu. “Au je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu
wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; kama kwa kweli Mungu ni
mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika imani, nao wale
wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya imani iyo hiyo,” Rum 3:29-30.
Ukweli ni kwamba kila anayeongozwa na mwenye dhamiri hai na safi ataokolewa
siku ya mwisho.
Mafundisho ya Kanisa hasa tunaposoma Katekisimu ya Kanisa
Katoliki, namba 847 inafundisha juu ya dhamiri hai na safi ambapo hata wale
wasiomjua Kristo ndiyo ponya yao. Ukweli huu pia umefafanuliwa vizuri katika
mafundisho ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano, Konstitusio ya Kichungaji juu ya
Kanisa katika Ulimwengu wa leo, “Gaudium Et Spesteaches,” “Furaha na
Matumaini,” inaelezea ukweli huu kama ifuatavyo; “Jambo hilo haliwahusu wakristo tu bali pia
wanadamu wote wenye mapenzi mema, ambao neema ya Mungu hufanya kazi mioyoni
mwao, kwa namna isiyoonekana. Maana Kristo alikufa kwa ajili ya watu wote na wito halisi wa binadamu ndio mmoja,
ule wa kimungu. Kwa hiyo lazima tuwe na wazo kwamba Roho Mtakatifu anawajalia
watu wote uwezekano wa kushiriki fumbo la kipasaka, kwa jinsi anayoijua Mungu,”
(no. 22)
Miongozo ya kibinadamu na mwonekano wake unaweza kutunyamazisha hapa na
pale kwa kuikandamiza dhamiri iliyo hai na safi kuelekea lililo kweli na haki.
Kelele hizo kamwe zisiwe kizuio cha kiu na kweli iliyopo ndani ya mioyo yetu.
Leo katika Injili tunaona watu wachache wakijaribu kuzuia dhamiri iliyo hai na
safi ya mtu mmoja kipofu aliyekuwa ameketi kando ya njia wakati Yesu akipita.
Aliposikia habari ya Yesu alipiga kelele na kusema, “Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu,” Lk 18:38.
Jitihada za huyu kipofu zinajaribiwa kuzimwa na baadhi ya watu. “Basi wale waliotangulia wakamkemea ili
anyamaze; lakini yeye alizidi sana kupaza sauti, Ee Mwana wa Daudi, unirehemu,”
Lk 18:39. Dhamiri iliyo hai na safi ya Kipofu huyu ikiongozwa na imani
aliyokuwa nayo, inakuwa sababu ya uponyaji wake. “Yesu akasimama, akaamuru aletwe kwake; na alipomkaribia,
alimwuliza, Wataka
nikufanyie nini? Akasema, Bwana, nipate kuona,” Lk 18:40-41. Imani hii iliyodhabiti na yenye kuongozwa na
dhamiri hai na iliyosafi juu ya Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, inakuwa uponyaji
wake. “Yesu akamwambia, Upewe kuona; imani
yako imekuponya,” Lk 18:42. Dhamiri hai na
safi hukuzwa na kuelimishwa hasa pale tunapopenda kutenda mema kwa vile
twatambua jambo jema ni jema kama lilivyo na linastahili kutendwa kila mmoja
wetu na hasa zaidi mwenye hofu ya Mungu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa hiyo ni lazima
kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri,” Rum
13:5
No hay comentarios:
Publicar un comentario