JUMATATU WIKI YA 1 YA MAJILIO
30/11/2015
Somo: Isa 2:1-5
Zab: 121: 1-2, 3-4a (4b-5, 6-7), 8-9
Injili: Mt 8:5-11
Nukuu:
“Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani
kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi
tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la
Bwana katika Yerusalemu,” Isa 2:3
“Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa
kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu;
taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena
kamwe,” Isa 2:4
“Yesu akamwambia,
Nitakuja, nimponye,” Mt 8:7
“Yesu aliposikia hayo,
alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona imani
kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,” Mt 8:10
TAFAKARI: Ajaye ni Bwana wa Amani.”
Wapendwa wana wa Mungu, Mwokozi tunayemtazamia kwa hamu ni
Bwana wa Amani atakayetufundisha njia zake na kueneka katika mapito yake.
Sheria yake kuu ni UPENDO. Ni wakati wa kuyajenga upya mahusiano yetu na Bwana
huyu wa Amani. Ni Bwana wa Amani wa wataifa yote, na ulimwengu mzima. Nabii
Isaya anasema habari za Mkombozi huyu: “Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu
mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake,
nasi tutakwenda katika mapito yake maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno
la Bwana katika Yerusalemu,” Isa 2:3.
Amani ya
Mkombozi huyu inaendana pia na haki. Hivyo ajapo lazima ipite hukumu ya haki,
na ndipo atakapousimika utawala wake wa Amani, Haki, na Upendo. Ili mambo haya
yatendeke katika utawala wake yatupasa kubadili namna yetu ya kufikiri na
kutenda. Ulimwengi wa leo vita na hasa ugaidi vinashamiri kwa nguvu kubwa sana
na uhai wa mwanadamu ikiwa ni pamoja na amani vipo reheni. Nabii Isaya anasema,
“Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi,
atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki
yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala
hawatajifunza vita tena kamwe,” Isa 2:4.
Tunahitaji sana kwa sasa utawala wa Mkombozi huyu. Lengo la Mungu kuumba
ulimwengu pamoja na mambo mengine, aliuumba ili pawe sehemu salama kwa ajili ya
uhai wa viumbe vyote alivyoviumba na kwa namna ya pekee Mwanadamu aliyemuumba
kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27.
Kujenga
mahusiano mapya na Mungu ni pamoja na kuwa na imani dhabiti naye. Leo katika
Injili Yesu anakutana na mtu mmoja, Akida, aliyekuwa anauguliwa na mtumishi wake
ugonjwa wa kupooza. Akida huyu anamwomba Yesu aende kumponya mgonjwa wake. Yesu
anamjibu, “Nitakuja, nimponye,” Mt 8:7. Akida huyu akitambua uwezo wake na
nafasi aliyokuwa nayo, na ule uwezo wa Yesu, bado anatambua kuwa umbali na
uwepo wa Yesu aviweza kumzuia kumponya mtumishi wake. Akida anamtaka Yesu aseme
neno tu na mgonjwa wake atapona. Hii ndiyo imani thabiti na isiyokuwa na shaka.
“Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata,
Amin, nawaambieni, Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli,”
Mt 8:10. Je, waamini kuwa Yesu aweza kutenda
maajabu ndani yako? Jenga uhusiano mpya naya kuanzia sasa!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Kama
mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng'oka,
ukapandwe baharini, nao ungewatii,” Lk 17:6
No hay comentarios:
Publicar un comentario