jueves, 12 de noviembre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 32 YA MWAKA-B

IJUMAA WIKI YA 32 YA MWAKA-B
13/11/2015
Somo: Hek 13:1-9
Zab: 19:2-3, 4-5ab
Injili: Lk 17:26-37
Nukuu:
“Huenda ilikuwa kwa kupendezwa na uzuri wake walivyodhania viumbe hivyo kuwa ni miungu, basi na wajue kadiri gani Bwana, Mfalme wao, avipitavyo; kwa maana Yeye aliye asili ya uzuri ndiye aliyeviumba,” Hek 13:3

Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake Mwana wa Adamu,” Lk 17:26

Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma,” Lk 17:31 

Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya,” Lk 17:33 

 Akawaambia, Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai,” Lk 17:37b

TAFAKARI: “Je, nimejiandaa vyema?”

Wapendwa wana wa Mungu, ni kawaida kwa kila mmoja wetu kujiandaa kwa matukio mbalimbali ya maisha kutoka hatua moja na kwenda nyingine. Leo napenda tutafakari matukio matatu muhimu kwa kila mmoja wetu, na tutazame pia ni kwa namna gani tunajiandaa katika matukio hayo. Matukio hayo ni kuzaliwa, tukio agano, na kifo. Ni jambo la kawaida kusheherekea au kukumbuka kwa kusheherekea siku ya kuzaliwa. Tunasheherekea tukio hili kwa kutambua na kumshukuru Mungu kwa zawaidi ya uhai na maisha aliyotukirimia bila kipimo. Hapa tunajiandaa vyema na wakati mwingine kwa gharama za juu kabisa.

Tukio la pili katika maisha ni ‘tukio agano.’ Tukio agano ni pale mtu anapofikia wakati fulani na kuamua namna atakavyoishi na kufuata mfumo mwingine wa maisha. Kwa walei ni maisha ya ndoa, na watawa na makleri ni maisha wa wakfu. Wengi tunatumia muda mwingi sana kujiandaa katika tukio hili. Hapa pia tunatumia gharama nyingi sana na wakati mwingine tunakufuru.

Tukio la tatu na la mwisho ni kifo. Tukio hili kadiri ya tathimini lina maandalizi hafifu sana licha ya kwamba ni tukio muhimu sana, na wakati mwingine ni zito kupita matukio yote. Unaweza kujiandaa kwa tukio la kwanza bila la pili, ila huweza kujianda kwa tukio la kwanza na la pili na ukakwepa tukio hili la tatu hata kama hutaki. Si lazima kuzaliwa na si lazima kufanya ‘tukio agano,’ lakini kama umezaliwa, na hata kama hutaki kufanya ‘tukio agano,’ lazima utakufa. Si nia yangu kukuogopesha ila ndio ukweli. Kwa nini basi tunaingiwa na upofu na usahaulifu wa kuweka umuhimu wa kutosha katika tukio hili la tatu?

Masomo yetu ya leo yanatupa majibu halisi ya ukweli kuhusu tukio hili la tatu, yaani kifo. Somo la kwanza linatupa jibu la kwa nini binadamu hupuuza ukweli kuhusu kifo. Ulevi wa starehe na anasa na kudhani sisi ndio kila kitu utusahaulisha kuhusu tukio hili la tatu, na hivyo kuyafanya maandalizi yake kuwa hafifu. “Huenda ilikuwa kwa kupendezwa na uzuri wake walivyodhania viumbe hivyo kuwa ni miungu, basi na wajue kadiri gani Bwana, Mfalme wao, avipitavyo; kwa maana Yeye aliye asili ya uzuri ndiye aliyeviumba,” Hek 13:3. Hata kama tunaufurahia ulimwengu huu kwa vyovyote vile yatupasa kuelewa yupo mmiliki halali wa vitu vyote. Sisi ni wamiliki wa muda mfupi tu na tutaviacha kama waliotutangulia walivyo viacha. Tulivikuta na tutaviacha.

Kifo wakati mwingine uonekana kipo mbali sana hasa pale tunapozama katika anasa na malimwengu. Wakati wa Nuhu na hata Lutu habari za Mungu na uwepo wake hazikuonekana kama kitu cha pekee kwa wengi hasa wale walioishi katika mfumo wa “ponda mali.” Ila hata kama hatuna hisia na Mungu, Yeye hupo hai na anayaona yote tuyafanyayo. Siku ya kuzungumza na kila mmoja wetu kwa wakati wake inakuja. Hivyo, Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake Mwana wa Adamu,” Lk 17:26. Itakapofika siku hiyo tutapigwa na mshangao kwa vile hatutakuwa tumejiandaa vya kutosha kwa sababu tu ya kupuuzia kama walivyompuuzia Nuhu kuitengeneza Safina ilhali hapakuwa na dalili yoyote ya mvua, mto, ziwa wala baharí, ila Mungu aliinyeeshea duania kutoka chini.

Mshango mwingine ni kwamba tukio hili la kifo litamkuta kila mtu pale alipo kwa mshangao. Ni mara ngapi tunaondokewa na wapendwa wetu ilhali hatukuwa kumeagana vizuri au kuongea nao kwa urefu? Mara nyingi tunabakiwa na ‘ninge..’ zisizo na idadi. Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma,” Lk 17:31. Hapa ni pale tunaposema, “lo! Nilikuwa naye leo asubuhi na sana hatunaye tena!” Hata tukio kama hilo halisemi chochote kuhusu maandalizi yako?

Yesu anatupatia jibu la mkwamo huu, na kutuweka mkono salama tusijepigwa na mshangao. Naye anasema, Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya,” Lk 17:33. Kuiponya nafsi katika kuingamiza ni kuiridhia nafsi kwa yale inayoyataka. Ni pale nafsi inapoegemea katika mwili na kufanya matendo ya mwili. “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,  ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Huku ni kuiponya nafsi katika kuiangamiza.

Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, kuiangamiza nafsi katika kuiponya ni pale nafsi yako inapoegemea roho, na kutenda matendo ya roho yenye tunda la roho. “Tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23. Huku ni kuiangamiza nafsi yako katika kuiponya. Je, mzoga wako utakuwa wapi?

Baada ya mafundisho haya mazito ya Injili ya leo, watu walitaka kujua hayo yatatendeka wapi? Yesu anatujibu hivi, “Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai,” Lk 17:37b. Kwa maana nyingine mwisho wako utategemea ishi yako. Hivyo kama nafsi yako katika ishi yako itaegemea mwili, ndivyo hivyo mwisho yako itakuwa katika matendo ya mwili. Tunaoambiwa watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Vile vile kama nafsi yako itaegemea roho yako, basi mwisho wako itakuwa tunda la roho. Tunaambiwa juu ya mambo kama hayo hakuna sheria, kwani kwa kuishi hivyo ndiyo sheria yenyewe aipendayo Mungu. Ni maisha ya kweli na haki.

Tumsifu Yesu Kristo!


Ni faida gani basi mliyopata siku zile kwa mambo hayo mnayoyatahayarikia sasa? Kwa maana mwisho wa mambo hayo ni mauti,” Rum 6:21

No hay comentarios:

Publicar un comentario