lunes, 16 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMANNE WIKI YA 33 YA MWAKA-B

JUMANNE WIKI YA 33 YA MWAKA-B
17/11/2015
Somo: 2Mak 6:18-31
Zab: 3:2-3, 4-5, 6-7
Injili: Lk 19:1-10
Nukuu:
“Lakini yeye aliikaza nia yake madhubuti, nia iliyostahili umri wake na jadi yake, na mvi zake stahivu, na mwendo wake wa adili tangu utoto wake katika kuzishika amri takatifu zilizotolewa na Mungu,” 2Mak 6:23a

“Na hata nikiepukana na adhabu ya wanadamu sasa, lakini sitaweza kuepukana na mikono ya Mwenyezi, nikiwa hai au nimekufa,” 2Mak 6:26

“Basi, nikitoa maisha yangu sasa kwa ushujaa, nitajionyesha kuwa nimeistahili miaka yangu mingi, na kuwaachia vijana mfano wa kufa mauti ya fahari kwa hiari na kwa uthabiti, kwa ajili ya amri takatifu zenye heshima,” 2Mak 6:27-28

“ingawa ningaliweza kuepukana na mauti, lakini ninavumilia maumivu makali mwilini mwangu; hata rohoni mwangu ninayavumilia kwa furaha kwa sababu ya kicho changu kwake,” 2Mak 6:30

“Hivyo alikufa; na kwa kufa kwake aliacha mfano wa unyofu na ukumbusho wa wema, si kwa vijana tu, ila kwa jamii yote ya taifa lake,” 2Mak 6:31

Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5

Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi,” Lk 19:7 

Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne,” Lk 19:8

Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9 

Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea,” Lk 19:10

TAFAKARI:Afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi kwa unajisi.”

Wapendwa wana wa Mungu, ingawa leo dunia inashuhudia uvunjifu mkuwa wa haki za binadamu, na matokea yake tunaona idadi kubwa ya wakimbizi ndani na nje ya nchi zao, haya hayakuwa makusudi ya Mungu katika uumbaji wetu na milki aliyotupatia. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi. Bwana Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza,” Mwa 1:28; 2:15. Lakini jambo la ajabu leo ni kwamba wapo baadhi ya binadamu wenzetu wanaojihesabia haki kuliko wengine na kwenda kinyume kabisa na mpango wa Mungu juu ya uumbaji na milki ya vile alivyo viumba.

Upofu wa ubinafsi na uchu wa madaraka umekuwa leo viatu vya kukanyagia haki za watu na hasa wanyonge. Je, katika hali kama hii yatupasa kukubaliana na udhalimu na kufa na tai shingoni? Somo letu la kwanza linatuambia hapana kwa ushuhuda wa Eleazari aliyesimama katika kweli. Kweli hiyo ndiyo inayokuweka huru. “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli,” Yoh 8:32, 36. Eleazari anakataa katu katu kula nyamba ya nguruwe kadiri ya makatazo ya Maandiko Matakatifu kama yanavyoweka wazi jambo hilo. Kuila nyama ya nguruwe ilikuwa ni najisi kwa sababu “Nguruwe amepasuliwa ukwato lakini hacheui, huyu ni najisi kwenu msile nyama zao, wala mizoga yao msiiguse,” Kumb 14:8, Law 11:7. Kwa ukweli huu, Eleazari hayupo tayari kwenda kinyume cha Maandiko Matakatifu na mila na desturi za jamii yake. Hivyo yupo tayari kwa lolote na hakuwa na woga wa kufa. “Lakini yeye aliikaza nia yake madhubuti, nia iliyostahili umri wake na jadi yake, na mvi zake stahivu, na mwendo wake wa adili tangu utoto wake katika kuzishika amri takatifu zilizotolewa na Mungu,” 2Mak 6:23a

Wapendwa wana wa Mungu, unavyoishi hapa duniani waweza kuwa moja ya ukweli huu, yaani kuwa Mhenga, au Lihoka. Mhenga ni yule anayeacha “legacy,” kitu cha kuigwa, na Lihoka, “bad spirit” ni yule asiyeacha kilicho kizuri cha kuigwa kwenye jamii. Kwa kuacha kitu cha kuigwa Eleazari anasema mbele ya watesi wake, “Basi, nikitoa maisha yangu sasa kwa ushujaa, nitajionyesha kuwa nimeistahili miaka yangu mingi, na kuwaachia vijana mfano wa kufa mauti ya fahari kwa hiari na kwa uthabiti, kwa ajili ya amri takatifu zenye heshima,” 2Mak 6:27-28. Wapo wengi sana  miongoni mwetu wanafikwa na mauti ya mtindo huu. Ni masikitiko makubwa leo kwamba kilichokuwa habari njema si habari, bali kile kisicho habari ndicho habari. Lakini historia inatuambia kwamba hakuna uovu wowote uliodumu katika umilele wake. Imani pia inatufundisha kwamba kisicho toka kwa Mungu, na kwa ajili Mungu na watu wake kamwe hakiwezi dumu katika fahari yake hata kama kikipambwa kwa mbwembwe zote za ulimwengu huu.

Je, katika hali kama hii ni vyema kuusaliti ukweli na kukumbatia mitazamo na sheria za wanadamu? Je, ni aheri nikubali ili niwe salama kumfurahisha mtesi wangu? Jibu ni hapana! Ni kusimama katika kweli na haki kama alivyo simama Eleazari na kusema, “Na hata nikiepukana na adhabu ya wanadamu sasa, lakini sitaweza kuepukana na mikono ya Mwenyezi, nikiwa hai au nimekufa,” 2Mak 6:26. Kuna faida gani kuipata nafuu ya leo na kuishi kwa kudharaulika na kuikosa mbingu kwa kuisaliti kweli na haki? Afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi kwa unajisi. Pamoja na kutengwa na washauri marafiki zake na kubaki mwenyewe, Eleazari hakuisaliti dhamiri yake hai na safi. Kwa kutunza heshima yake na uzee wake Eleazari hakubadili msimamo wake uliojijenga katika kweli na haki. Naye anasema kwa ushujaa, “ingawa ningaliweza kuepukana na mauti, lakini ninavumilia maumivu makali mwilini mwangu; hata rohoni mwangu ninayavumilia kwa furaha kwa sababu ya kicho changu kwake,” 2Mak 6:30. Pasipo njia Mungu huifanya njia hata kama kwa sasa lililo ovu litashinda. Ila Mungu wa haki na kweli atausimamisha utawala wake ulio wa kweli na haki kwa kuridhiwa na wana wa Taifa lake.

Injili ya leo tunaona simulizi la makutano ya kati ya Yesu na Zakayo. Zakayo hamwoneyi Yesu aibu pamoja na watu kuyajua madhaifu yake na ufupi aliokuwa nao. Bado anaona salama yake ipo kwa Kristo tu na siyo mitazama ya wale walikuwa wanamzunguka. Ili amwone Yesu, Zakayo alipanda juu ya mkuyu. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5. Tendo hili la Yesu linawashangaza wengi na wengine wananung’unika. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi,” Lk 19:7. Kwa utayari wa Yesu kwenda nyumbani kwa Zakayo, kwa furaha aliyokuwa nayo Zakayo hakuweza kuificha. Hivyo Zakayo anayaweka yote wazi mbele ya Yesu.  Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne,” Lk 19:8. Hii ni toba ya kweli na maungamo ya wazi mbele ya Yesu aliye sasa njia, kweli na uzima. Maungamo haya ya kweli toka moyoni mwa Zakayo yanaifunua furaha na upendo wa Mungu kupitia mwanaye Yesu Kristo na kuonyesha kile hasa Yesu alichokijia ulimwenguni. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9. Wokovu ni kwa kila mmoja na hasa pale tunapouridhia wokovu huo kwa utashi wetu wenyewe na kwa dhamiri iliyo hai na safi. Mungu anatutazama utayari wetu katika upya wa kuyaanza yote naye na siyo historia ya maisha yetu mabaya. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea,” Lk 19:10. Ndugu yangu, afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi kwa unajisi. Nafasi ndiyo sasa kusimama katika kweli na haki, na kuchukia uovu wa aina yoyote ile kwenye maisha yako na jamii inayotuzunguka.

Tumsifu Yesu Kristo!


“Mwenye haki atasitawi kama mtende, Atakuwa kama mwerezi wa Lebanoni,” Zab 92:12

No hay comentarios:

Publicar un comentario