JUMAPILI
WIKI YA 34 YA MWAKA-B
Jumapili
ya Mwisho wa Mwaka
Sherehe
ya Bwana Wetu Yesu Kristo Mfalme
22/11/2015
Somo
I: Dan 7:13-14
Zab:
93:1-2, 5
Somo
II: Ufu 1:5-8
Injili:
Yoh 18:33-37
Nukuu:
“Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila
zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya
milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza
kuangamizwa,” Dan 7:14
“Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa
waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu
katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba
yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele,” Ufu 1:5-6
“Tazama, yuaja na mawingu; na kila jicho litamwona, na hao
waliomchoma; na kabila zote za dunia wataomboleza kwa ajili yake. Naam. Amina,”
Dan 7:7
“Yesu akamjibu, Wewe
wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu?” Yoh
18:34
“Yesu akajibu, Ufalme
wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu,
watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini
ufalme wangu sio wa hapa,” Yoh 18:36
“Basi Pilato
akamwambia, Wewe u mfalme basi? Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni
mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja
ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti
yangu,” Yoh 18:37
TAFAKARI:
“Kama ni wana wa Mfalme Yesu Kristo, nifanane naye na kusimama katika Haki na
Uzima, Utakatifu na Neema, Upendo na Amani.
Wapendwa wana wa Taifa
la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya “34” ya Mwaka “B” wa Kanisa.
Leo ni Dominika ya mwisho ya mwaka “B” katika mzunguko wake kadiri ya mpango wa
kiliturjia. Ni kwenye Dominika hii ya mwisho ya Mwaka, Mama Kanisa
anasheherekea Sikukuu ya Bwana wetu Yesu Kristo Mfalme. Ufalme wa Bwana wetu
Yesu Kristo ni tofauti na falme nyingine katika ulimwengu huu. Ufalme wa Kristo
ulijidhihirisha kile atakachokuwa kuanzia pale alipomwilishwa na mwisho kuyatoa
maisha yake kwa ajili ya dhambi zako na zangu, yaani kifo cha msalaba. Msalaba
Mtakatifu kwa sasa ndicho kiti chake cha hukumu ya haki na amani, utakatifu na
neema, na mapendo na Amani. Kofia yake ya kifalme ni taji lake la miiba. Hii ya
dhihirisha wazi tabia ya Ufalme wa Kristo, yaani, uvumilivu kwa kila
aliyeridhia ufalme wake, unyenyekevu katika kuyajali maslahi ya wengine kwanza
kabla ya kwako na yangu, huruma katika kuchukulia na kusamehana ikiwa kuwa
tayari kusikiliza hisia za maumivu ya wengine hata kama hayana ukweli. Hili
ndilo taji la miiba!
Kwa kumwilishwa, yaani
neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, Yesu alikubali kuchukuwa mwili na hali ya
mwanadamu bila kupoteza asili yake ya kimungu ili awe mkombozi wako na wangu.
Hakika kwa kazi hii ilipaswa azaliwe kwenye mahekalu ya dhahabu na yaliyopambwa
na nakshi za gharama kubwa. Badala yake tunaambiwa kwamba wachungaji
walikimbilia Bethlehemu baada ya kuambiwa na malaika. “Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule
mtoto mchanga amelala horini,” Lk 2:16. Mfalme huyu anazaliwa horini
kama alama na uthibitisho wa kutumika na siyo kutumikiwa. Hapa mimi na wewe
tunafundishwa unyenyekevu katika maana ya kujitoa zaidi kwa wengine kuliko
kujitazama wenyewe. Hapa mimi na wewe tunafundishwa upendo wa kweli
unaojidhihirisha katika kujishusha chini kabisa katika hali za watu. Upendo huu
unafikia kilele chake pale msalabani ambapo Mfalme huyu Yesu Kristo anautoa
uhai wake waajili ya rafiki zake ambao ni wewe na mimi. “Hakuna
aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki
zake,” Yoh 15:13. Huyu ndiye Kristo Mfalme tunayemsheherekea leo. Yesu Kristo
katika ukweli huu anadhihirisha kuwa yeye ni shahidi na mwaminifu, mazaliwa wa
kwanza wa waliokufa, aliyetayari kutuosha dhambi zetu kwa damu yake, na
kutufanya kuwa ufalme na makuhani wa Mungu. Huu ni umependo wa ajabu sana
kwetu. “Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza
wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi
zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni
Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele,” Ufu 1:5-6. Kwa nini
basi nashindwa kupenda kama Kristo alivyonipenda?
Mamlaka
ya Kristo ni ya milele na hivyo kumtenga na falme za leo na sasa. Ufalme wake
ni ufalme usioangamizwa. “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa
kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka
ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza
kuangamizwa,” Dan 7:14. Yesu akiwa kizimbani, Pilato anahoji kwa kejeri asili
ya mamlaka na ufalme wa Yesu na mwisho kumwita Mfalme. “Yesu akamjibu, Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine
walikuambia habari zangu?” Yoh 18:34. Hata
hivyo Yesu anaweka wazi alisi, mamlaka, na ufalme wake. Kwanza kabisa ufalme wa
Kristo siyo wa duniani hii. Ingekuwa hivyo kilichompata na hali na namna
alivyofanyiwa watumishi wake wangempigania na asingetiwa mikono mwa wayahudi.
Kwa maneno mengine ufalme wake ni wa milele. “Ufalme wangu sio wa
ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu
wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio
wa hapa,” Yoh 18:36.
Tendo hilo la kukubali
kudhalilishwa kiasi hicho Bwana wetu Yesu Kristo hakikumwondolea Ufalme wake,
mamlaka yake, wala Umungu wake. Ila kwa tendo hilo ni ponya yetu na kuwa huru
kwetu. Hapa ndipo pale tuliponunuliwa kwa gharama kubwa sana, yaani kwa damu
yake. Wewe na mimi leo tunathamani kubwa sana mbele ya Mungu kwa sababu
tumekombolewa kwa gharama ya damu yake Yesu. “Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa
fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba
zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na
waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 18-19. Tendo hili pia licha ya kutufanya kuwa na
thamani kubwa sana mbele ya Mungu, limetufanya na linatufanya matajiri. Kwa
tendo hili la kuutoa uhai wake kwa ajili yetu, Kristo amekubali kuwa masikini
ili wewe na mimi tuwe matajiri. “Maana mmejua neema ya
Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa
tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake,” 2Kor 8:9.
Ni kwa ajili ya mambo haya makuu Kristo ni Mfalme na alizaliwa kwa ajili hiyo.
Kuja kwake ulimwenguni ni kuusimika ufalme huu na kweli yake. Yesu anamjibu
Pilato swali lake la kejeli kuhusu kuwa yeye ni Mfalme. “Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi
nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni,
ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu,” Yoh
18:37. Ndugu yangu wasimama katika kweli? Kama sivyo, bali elewa huisikii sauti
ya Kristo.
Wapendwa
katika Kristo, Ufalme wa Kristo ni ufalme wa haki na uzima, ufalme wa
utakatitifu na Neema, ufalme wa mapendo na amani. Nasi kwa upendeleo mkubwa tu
wana wa ufalme huu kwa sakramenti ya ubatizo. Kwa sakramenti hii tu wana na
warithi wa ufalme wa Kristo na Mungu wetu hasa pale tunapoishi ahadi zetu za
ubatizo. Hivyo mimi kama mwana wa Mfalme Yesu Kristo nifanane
naye na kusimama katika Haki na Uzima, Utakatifu na Neema, Upendo na Amani.
Wapendwa wana wa Mungu
ikiwa lengo la kwanza la kuumbwa kwetu na kukombolewa kwetu lililengo kujenga
mahusiano mazuri na muumba wetu, lengo la pili tuwapo hapa duniani ni
kuudhihirisha ufalme wake. Hapa ninaudhihirisha ufalme wake Kristo kwa kuishi
na kusimamia ufalme wa haki na uzima kwa kuyafanya mazingira ninayoishi yawe ya
haki na kuchanua kwa uzima wa roho na mwili. Niudhihirishe ufalme wa Mungu kwa
kuishi maisha ya utakatifu na neema. Maisha hayo yawe chachu kwa wengine
wamwone Kristo kupitia kwangu, na kuwa barua ya kusomwa na wengine. Mtume Paulo
anawaambia wakristo wa Korintho, “Ninyi ndinyi barua
yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya
Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye
hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama,”
2Kor 3:2-3. Mwisho, nikiwa hapa duniani yanipasa kuudhihirisha ufalme wa
mapendo na Amani. Ili mazingira ninayoishi na ulimwengu ninaoishi na
kunizunguka uwe na mapendo na amani yanipasa muda wote nijihangaishe kwa ajili
kuwa mpatanishi. Yesu hasemi ‘heri wenye upendo, au heri wanaojua kupenda
wataitwa wana wa Mungu,’ bali ‘heri wapatanishi.’ “Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa
wana wa Mungu,” Mt 5:9. Hivyo kuudhihirisha ufalme wa mapendo na Amani,
yanipasa kuwa mtapatanishi na ndipo nitaiwa mwana wa Mungu na mrithi wa ufalme
wake.
Kutafuta amani siyo KUEPUKA MGOGORO, kukimbia mgogoro,
kujifanya hakuna tatizo au kuogopa kuliongelea tatizo huo ni woga kwa hakika.
Yesu, mfalme wa amani, hakuogopa kamwe migogoro. Mara nyingine aliuchochea
ukatokea kwa faida ya wote. Wakati mwingine tunatakiwa kuepuka migogoro, wakati
mwingine kuisababisha, na wakati mwingine tunahitaji kuitatua. Lengo liwe kwa
faida ya wote. Ndiyo maana tunapaswa kuomba uongozi wa Roho Mtakatifu daima.
Kuleta amani siyo KUTULIZA HASIRA. Mara nyingi
unakubaliana, unakuwa kama jamvi, na unawaruhusu wengine wakukanyage sivyo
alivyokusudia Yesu. Alikataa kuacha mambo kama yalivyo, na akachukua msimamo
mbele ya upinzani wa waovu.
Ndugu yangu uliyesafiri nami katika tafakari hii;
Ni heri kwenda Mbinguni ukiwa na suruali iliyotoboka
makalio kwa sababu ya kuhangaika kwa ajili ya kuwa mpatanishi, kuliko kwenda
jehenamu ukiwa umevalia suti na tai.
Ni kwa maana hiyo, heri kwenda mbinguni na kuufurahia
ufalme wa Mungu ukiwa na kandambili zilizo kwisha kisigino, kuliko kwenda
kwenye mateso jehenamu ukiwa umevalia mokasini zenye kisigino cha chuma.
Ni heri kwenda mbinguni ukiwa na jina la Lofa kwa sababu ya
kupigania haki za wanyonge, uzima na usalama wao, kuliko kwenda jehenamu kwa
jina la Luatani.
Ni heri kwenda mbinguni na kuufurahia ufalme wa Mungu ukiwa
mikono mitupu na maisha ye neema, kuliko kwenda jehenamu ukiwa milionea.
Ndugu yangu, hakuna dharau yoyote ili kubwa, kukashifiwa
kuliko pindukia, matusi ya kila aina ambayo Yesu hakuyapata. Aliyakubali yote
kwa kutupenda upeo ili leo mimi na wewe tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi. “Basi, kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali
akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba,
naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo,” Yoh 13:1
Tumsifu Yesu Kristo!
“Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, Na mamlaka yako ni ya
vizazi vyote,” Zab 145:13
No hay comentarios:
Publicar un comentario