viernes, 20 de noviembre de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 33 YA MWAKA-B

JUMAMOSI WIKI YA 33 YA MWAKA-B
21/11/2015
Somo: 1Mak 6:1-13
Zab: 9:2-3, 4, 6, 16, 19
Injili: Lk 20:27-40
Nukuu:
“Lakini sasa nayakumbuka mabaya niliyoyafanya Yerusalemu, jinsi nilivyoichukua vyombo vyote vya fedha na dhahabu vilivyokuwapo, na kupeleka majeshi kuwaharibu wenyeji wa Yesusalemu bila sababu,” 1Mak 6:12

“Nafahamu ya kuwa kwa sababu hiyo maovu haya yamenipata, hata, tazama, ninakufa kihoro katika nchi ya kigeni,” 1Mak 6:13

Yesu akawaambia, Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi,” Lk 20:34-35

wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:36

Naye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38 

TAFAKARI: “Mtafute Bwana ungali hai kwani anapatikana.”

Wapendwa wana wa Mungu, waswahili wanatufundisha hivi; ‘majuto ni mjukuu.’ Wahenga wanaenda mbali zaidi na kusema, ‘ndege mmoja mkoni ni bora kuliko ndege mia moja porini.’ Naye Mt. Agustino anatuambia ‘hakuna kesho kama hakuna leo.’ Kumbe leo na sasa ndiyo hatma ya kila kitu katika maisha yangu. Wengi hatupendi kufanya mabadiliko katika maisha yetu kwa sababu tunadhani bado tuna muda wa kutosha kufanya hivyo, kwa hiyo hakuna sababu ya kufanya haraka. Maandiko Matakatifu yanatuambia hivi: “Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; Na amrudie Bwana, Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa,” Isa 55:6-7. Mungu ni Huruma, Upendo, na Msahama. Kamwe hapendi kuona unaangamia katika dhambi.

Somo letu la kwanza linatufundisha matokea mabaya ya matumizi mabaya ya madaraka na nafasi tulizopewa kama dhamana katika kutumika kwa ajili ya wengine. Kweli cheo ni dhamana na uongozi ni kutumika. Somo hilo pia linatufundisha kujinyenyekesha hasa pale tunapopewa dhamana iwe kubwa au ndogo kwani mwisho wa siku yatupasa kutoa hesaba yake. Tupewapo dhamana hiyo salama yetu ipo pale tunapo yafanye yote kwa ukamilifu yanayotupasa kufanya. Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya,” Lk 17:10. Tatizo letu wengi ni pale tunapopenda kutumikiwa kuliko kutumika.

Mfalme Antioko anavuna kile alichokipanda. Utawala wake ulikuwa wa dhuluma sana na wa kutokujali haki za raia wake. Aliyafanya hayo yote kwa kujua kabisa bila kukumbuka kwamba ipo siku yote yana mwisho wake. Kwa mamlaka aliyokuwa nayo ilimpasa kuyafanya utawala wake uwe mahali pazuri pa kuishi. Kinyume chake utawala wake ulikuwa kilio cha wengi na huzuri kwa wanyonge na wasio na sauti. Wengi walilazimishwa kuishi kwa kuzisaliti dhamiri zao. Wengi wao pia walikubali kufa kuliko kutenda dhambi na kwenda kinyume cha imani yao, mila na desturi zao. Mwisho ya hayo yote mfalme Antioko anakiri na kusema, “Lakini sasa nayakumbuka mabaya niliyoyafanya Yerusalemu, jinsi nilivyoichukua vyombo vyote vya fedha na dhahabu vilivyokuwapo, na kupeleka majeshi kuwaharibu wenyeji wa Yesusalemu bila sababu,” 1Mak 6:12. Tamaa ya mali na madaraka ni janga kubwa sana hasa katika tawala za nchi masikini na zile zinazoendelea. Ukweli ni kwamba uongozi mbovu na sera mbovu chini ya mfumo mbovu kikatiba ndiyo sababu ya ugumu wa maisha ya watu licha ya utajiri walio kuwa nao kama nchi. Wakati ndiyo sasa! Kila mtu amtafute Mungu aliye hai kwani anapatikana. Sote tumeumbwa si kwa bahati mbaya, bali kwa malengo tena tuishi milele.

Jambo ambalo lipo wazi ni hili, hakuna chozi la mtu yeyote anayemlilia Mungu katika kweli na haki ambalo litapotea bure. Watendao maovu hasa wale walipewa dhamana na umma wa watu miisho yao kamwe haiwezi kuwa mizuri. Ukimya wa Mungu katika mateso ya watu wake sio kwamba Mungu huyu haoni bali huwapa nafasi pia waovu kutubu na kukiri dhambi zao.Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana,” Isa 55:8. Na kwa sababu hiyo Mungu hubaki kuwa Upendo, Huruma, na Msamaha. Mwisho wa Antioko anaueleza mwenyewe na kusema, “Nafahamu ya kuwa kwa sababu hiyo maovu haya yamenipata, hata, tazama, ninakufa kihoro katika nchi ya kigeni,” 1Mak 6:13. Je, Mungu wetu yupo mbali? Mtafute sasa kabla ya kiama. Tunaposema Mungu ndiye kila kitu tunamaanisha hivyo. Nabii Amosi anatuambia siri kubwa kuhusu Mungu wetu huyu aliye hai na kusema, mtafuteni yeye afanyaye Kilimia na Orioni, na kukigeuza kivuli cha mauti kuwa asubuhi, na kuufanya mchana kuwa giza kwa usiku; yeye ayaitaye maji ya bahari, na kuyamwaga juu ya uso wa nchi; Bwana, ndilo jina lake,” Amo 5:8. Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, jeuri yako na mbwembwe zako zinatoka wapi juu ya Mungu huyu aliye hai? Jisalimishe!

Wapendwa wana wa Mungu, yeyote yule aliyepewa dhamana kuuongoza umma wa watu wa Mungu, yampasa kusimama katika haki na kweli. Nabii Sefania anatuambia kwamba, mwenye kusimama katika unyenyekevu na kutenda haki, Mungu huificha mtu huyo katika siku ya hasira yake. Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana,” Sef 2:3. Ni kwa kutafuta haki katika unyenyekevu na kutenda haki hiyo, hatuna sababu ya kuofia hali ya ulimwengu ujao.

Yesu katika Injili ya leo anawatoa wasiwasi wale waliomuuliza juu ya nani hasa atakaye kuwa mume baada ya maisha haya ya duniani ikiwa mwanamke huyo aliolewa na kurithiwa na ndugu saba wa familia moja. Yesu anawajibu na kuwaambia, “Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa; lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi,” Lk 20:34-35. Tukiwa hapa duniani ni wakati wa kuyafanya yote katika wema na haki. Hivyo, kesho yetu ni matokeo ya leo yetu. Mahitaji yetu tuwapo hapa ulimwenguni ni tofauti na mahitaji yetu tukiwa mbingu kwenye uzima wa milele. Hivyo walioko huko kwenye uzima wa milele, wala hawawezi kufa tena; kwa sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa ufufuo,” Lk 20:36. Kwa sababu hiyo mahitaji ya kimwili hayana nafasi tena kwani tutakuwa na miili iliyotukuka. Miili ya ufufuko. Ukweli huu unathibitisha kwamba Mungu wetu, si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake,” Lk 20:38. Ndugu yangu, kesho yako katika mikono salama ya Mungu inategemea leo yako katika mikono ya Mungu iliyo salama. Hivyo mtafute Bwana ungali hai kwani anapatikana.

Tusifu Yesu Kristo!


Kutenda haki na hukumu Humpendeza Bwana kuliko kutoa sadaka,” Mit 21:3

No hay comentarios:

Publicar un comentario